Hamia kwenye habari

Ndugu Shamil Khakimov akisalimiwa na ndugu na dada anapoondoka gerezani

MEI 16, 2023
TAJIKISTAN

Ndugu Shamil Khakimov Mwenye Umri wa Miaka Sabini na Miwili Aachiliwa Kutoka Gerezani Nchini Tajikistan

Ndugu Shamil Khakimov Mwenye Umri wa Miaka Sabini na Miwili Aachiliwa Kutoka Gerezani Nchini Tajikistan

Mei 16, 2023, Ndugu Shamil Khakimov aliachiliwa kutoka gerezani nchini Tajikistan. Alirudi nyumbani baada ya kutumikia kifungo cha zaidi ya miaka minne gerezani kwa sababu ya imani yake.

Hata kabla ya kukamatwa mwaka wa 2019, Shamil alikuwa na ugonjwa wa shinikizo la damu, ugonjwa wa moyo, na magonjwa mengineyo. Licha ya kuwa na matatizo ya afya, Shamil hakupewa matibabu yanayofaa alipokuwa gerezani. Kwa sababu hiyo, afya yake ilizorota na hata sehemu fulani ya mguu na wayo ikaanza kuoza kwa sababu ya ukosefu wa damu.

Lakini, licha ya magumu na maumivu aliyopata gerezani, Shamil alidumisha mtazamo mzuri kwa kutafakari mistari hususa ya Neno la Mungu.

Shamil anapokelewa nje ya gereza na marafiki waliobeba ishara inayosema “Tunakupenda, Shamil!”

Mara nyingi, katika sala zake Shamil alitia ndani maneno ya Zaburi 141:8: “Macho yangu yanakutazama wewe, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Nimekukimbilia wewe.” Kwa kuongezea, alifarijiwa sana na maneno ya Isaya 49:13, 16, ambayo inasema kwamba majina ya wanaoteseka ‘yamechongwa’ kwenye viganja vya Yehova. Maneno hayo yalimhakikishia Shamil kwamba hata ingawa alikuwa amefungwa gerezani, Yehova hangemsahau.

Kwa sababu ya faraja aliyopata katika Neno la Yehova, Shamil alidumisha shangwe yake na hata aliweza kuwatia moyo wengine. Ndugu mmoja ambaye aliwasiliana kwa ukawaida na Shamil alipokuwa gerezani, anasema hivi: “Mara ya kwanza nilipompigia simu, nilitarajia kusikia sauti ya mtu aliyevunjika moyo sana. Lakini alisikika akiwa na nguvu. Alikuwa na mtazamo mzuri katika hali zote zile na mara nyingi yeye ndiye aliyetuchangamsha.”

Maombolezo 3:25: “Yehova ni mwema kwa yule anayemtumaini, kwa mtu anayeendelea kumtafuta.” Tunasali tukiwa na uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwa “mwema” kwa Shamil na ndugu na dada zetu wengine wote wanaovumilia kwa shangwe nchini Tajikistan.