Hamia kwenye habari

Ndugu Ihlosbek Rozmetov

JANUARI 22, 2021
TURKMENISTAN

Ndugu Ihlosbek Rozmetov Amehukumiwa kwa Mara ya Pili kwa Kukataa Kujiunga na Jeshi kwa Sababu ya Dhamiri

Ndugu Ihlosbek Rozmetov Amehukumiwa kwa Mara ya Pili kwa Kukataa Kujiunga na Jeshi kwa Sababu ya Dhamiri

Hukumu

Januari 19, 2021, mahakama ya chini ya Turkmenistan ilimhukumu Ndugu Ihlosbek Rozmetov. Alihukumiwa kifungo cha miaka miwili katika gereza lenye ulinzi mkali kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Hii ndiyo mara yake ya pili kufungwa kwa sababu ya msimamo wa kutounga mkono upande wowote.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Ihlosbek Rozmetov

  • Alizaliwa: 1997 (Andalib)

  • Maisha Yake: Katika familia yao wamezaliwa watoto watatu. Alipokuwa na umri wa miaka kumi alianza kufanya kazi baada ya shule ili kusaidia kutegemeza familia yao. Anafurahia kucheza michezo, kusoma vitabu, na kusikiliza muziki. Mama yake alianza kujifunza Biblia katika mwaka wa 2010, naye akaanza kujifunza mwaka mmoja baada ya hapo

Historia ya Kesi

Julai 11, 2018, Ihlosbek Rozmetov, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 20, alihukumiwa mwaka mmoja katika kambi ya kazi ngumu ya Seydi kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Aliachiliwa baada ya kutumikia kifungo chake chote. Kulingana na sheria ya Turkmenistan, anaweza kuhukumiwa mara mbili kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.

Novemba 25, 2020, Ihlosbek aliagizwa ajiunge na jeshi kwa mara nyingine. Kwa heshima alieleza imani yake ya Kikristo. Hata hivyo, wenye mamlaka walimfungulia kesi ya uhalifu, hivyo akapewa kifungo kirefu zaidi kwa kuwa ilikuwa mara yake ya pili kufungwa kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.

Ihlosbek anasema kwamba kifungo chake cha kwanza gerezani kilikuwa “kigumu sana.” Kilichomsaidia kuvumilia ni mistari ya Biblia aliyokuwa amesoma na kukariri kabla ya kwenda gerezani. Ihlosbek anasema alifaidika hasa alipotafakari Wafilipi 4:6, 7. Mistari hiyo ilimkumbusha ‘asihangaike kuhusiana na jambo lolote,’ asali ili apate “amani ya Mungu,” na aendelee kuwa mtulivu anapokuwa katika hali ngumu. Ihlosbek anasema hivi: “Nilisali mara nyingi sana kwa Yehova nilipokabili majaribu hayo na nikahisi kwamba alikuwa karibu nami.”

Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kumwimarisha Ihlosbek na wote wanaomtumaini Yehova.—Isaya 40:29-31.