Hamia kwenye habari

Ndugu Nazar Alliyev

FEBRUARI 11, 2021
TURKMENISTAN

Ndugu Nazar Alliyev Ahukumiwa Kifungo cha Mwaka Mmoja Gerezani kwa Kukataa Utumishi wa Kijeshi kwa Sababu ya Dhamiri

Ndugu Nazar Alliyev Ahukumiwa Kifungo cha Mwaka Mmoja Gerezani kwa Kukataa Utumishi wa Kijeshi kwa Sababu ya Dhamiri

Hukumu

Februari 10, 2021, mahakama nchini Turkmenistan ilimhukumu Ndugu Nazar Alliyev kifungo cha mwaka mmoja gerezani kwa kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri.

Maelezo Mafupi Kumhusu

Nazar Alliyev

  • Alizaliwa: 2000 (Mkoa wa Lebap)

  • Maisha Yake: Anaishi Türkmenabat pamoja na mama yake na ndugu zake wawili. Anapenda kucheza mpira wa wavu na mpira wa miguu. Ana magonjwa mawili ya moyo. Anafanya kazi ya kinyozi ili kusaidia kutegemeza familia yao.

    Mama yake alimfundisha kupenda kanuni za Biblia. Alibatizwa mwaka 2015 akiwa na umri wa miaka 14. Anajulikana kuwa kijana mchangamfu, mkarimu na mnyenyekevu. Familia yake inaunga mkono uamuzi wake wa kukataa utumishi wa kijeshi

Historia ya Kesi

Mei 16, 2020, Ndugu Nazar Alliyev alipelekwa kwenye ofisi ya msajili wa utumishi wa jeshi. Maofisa walimshinikiza avae nguo za kijeshi ambazo zingeonyesha kwamba ameandikishwa jeshini, lakini alikataa. Mei 28, Nazar alikutana na maofisa wengine na kwa mara nyingine tena alikataa kujiunga na jeshi. Mwezi uliofuata, Nazar alimwandikia barua ofisa anayeandikisha watu katika wilaya yake na kumweleza kuhusu imani yake.

Januari 4, 2021, Nazar alienda pamoja na mama yake kwenye ofisi ya mwendesha mashtaka wa wilaya ya Khojambaz. Nazar akaeleza tena sababu yake ya kukataa utumishi wa kijeshi na akaomba kufanya utumishi wa badala. Licha ya jitihada zote hizi, mpelelezi alisema kwamba angefungua kesi dhidi ya Nazar.

Nazar ambaye ana umri wa miaka 20 sasa, anasema hivi: “Unapomtegemea Yehova katika hali hizo, anakupa amani ya moyoni. Kwa msaada wa Yehova, unaweza kuzungumza kwa utulivu.”

Anaongezea hivi: “Ninapokumbuka mambo yaliyonipa, ninatambua kwamba sikuzote Yehova amenitegemeza. Hilo linanipa uhakika kwamba atanisaidia wakati ujao.”

Hakuna utumishi wa badala nchini Turkmenistan. Hivyo, ndugu wanaokataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri wanakabili kifungo cha hadi miaka miwili gerezani. Kufikia sasa kuna vijana 15 gerezani nchini Turkmenistan waliofungwa kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote.

Tunajua kwamba Yehova ataendelea ‘kutenda kwa ushikamanifu’ kumwelekea Nazar pamoja na ndugu zetu wote nchini Turkmenistan.—Zaburi 18:25.