Hamia kwenye habari

Familia nchini Ubelgiji ikihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo wa mwaka wa 2021

APRILI 16, 2021
UBELGIJI

2021 Mwadhimisho wa Ukumbusho—Mashahidi wa Yehova Nchini Ubelgiji Waripoti Hudhurio Kubwa Zaidi Katika Miaka Mingi

2021 Mwadhimisho wa Ukumbusho—Mashahidi wa Yehova Nchini Ubelgiji Waripoti Hudhurio Kubwa Zaidi Katika Miaka Mingi

Katika mwaka wa 2021, jumla ya watu 49,040 nchini Ubelgiji walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo—mwadhimisho muhimu zaidi katika mwaka kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova. Hilo ndilo hudhurio kubwa zaidi la Ukumbusho nchini Ubelgiji tangu 1995. Ni karibu mara mbili ya idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini humo.

Hudhurio hilo kubwa kwa ajili ya mwadhimisho wa Kikristo linapendeza sana kwa sababu watu wengi zaidi nchini Ubelgiji wameacha kupendezwa na mambo ya dini. Kwa mfano, mwaka wa 1970 zaidi ya asilimia 90 ya Wabelgiji walijitambulisha kuwa Wakristo na asilimia 6 hivi ndio waliosema hawapendezwi na dini. Hata hivyo, ripoti za karibuni zinaonyesha kwamba idadi ya Wakristo nchini Ubelgiji imepungua kufikia chini ya asilimia 60 ya idadi ya watu nchini humo. Wanaojitambulisha kuwa hawapendezwi na dini wameongezeka kufikia zaidi ya asilimia 40.

Katika miaka ya karibuni, vyombo vya habari nchini Ubelgiji vimekuwa vikitangaza habari zinazowapinga Mashahidi wa Yehova, na nyakati nyingine vinatangaza habari za uwongo. Licha ya matangazo hayo yasiyofaa, idadi kubwa ya Wabelgiji wamekuwa wakitafuta habari sahihi kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Wengi wa wanaopendezwa wamejionea moja kwa moja upendo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova na kujionea furaha katika maisha yao kwa sababu ya kufuata mafundisho ya Biblia.—Yohana 13:35.

Dada akiongoza funzo la Biblia kwa kutumia kitabu Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu pamoja na dada aliyebatizwa hivi karibuni ambaye alihudhuria Ukumbusho wa 2021

Februari 2021, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ubelgiji iliripoti kilele kipya cha watu 11,804 wanaojifunza Biblia—watu 1,000 hivi kuliko wale waliokuwa wakijifunza mwaka wa utumishi uliotangulia. Katika miaka mitano iliyopita, wastani wa watu 450 wameamua kubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova kila mwaka.

Maendeleo hayo nchini Ubelgiji ni mifano michache tu ya jinsi Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanavyoendelea kujionea utimizo wa unabii huu wa Biblia: “Mdogo atakuwa elfu na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu.”—Isaya 60:22.