Hamia kwenye habari

JUNI 19, 2023
UGIRIKI

Kitabu cha Mathayo Chatolewa Katika Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki)

Kitabu cha Mathayo Chatolewa Katika Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki)

Juni 10, 2023, Ndugu Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kutolewa kwa Biblia—Habari Njema Kulingana na Mathayo katika Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki). Kitabu hicho cha Biblia kilitolewa katika programu ya pekee iliyofanywa kwenye ofisi ya tawi iliyo mjini Piraeus, Ugiriki. Programu hiyo ilipeperushwa kwa makutaniko yote nchini Ugiriki na nchini Saiprasi na kutazamwa na zaidi ya watu 29,000. Baada tu ya programu hiyo, kitabu hicho kingeweza kupakuliwa katika mfumo wa kielektroni. Makutaniko yatapata nakala zilizochapishwa katika miezi ijayo.

Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki) hakina sheria rasmi zinazofafanua jinsi ya kutamka maneno au kuiandika lugha hiyo basi kuitafsiri si rahisi. Kikundi cha utafsiri cha Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki) kina watafsiri kumi nao hufanyia kazi yao kwenye ofisi ya tawi ya Ugiriki. Watafsiri hao wanapata msaada mkubwa kutoka kwa ndugu na dada walio shambani.

Baada ya kusoma kitabu cha Mathayo katika Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki) dada mmoja alisema hivi: “Nilijifunza kumhusu Yehova kupitia funzo la Biblia katika lugha ya Kigiriki. Ingawa nilielewa kile nilichosoma na kusikia, kusoma Biblia katika lugha ya mama kunanigusa moyo na kunichochea kutumia mambo ninayojifunza.”

Dada mwingine alisema: “Kusoma andiko la Mathayo 26:38, 39 katika Kiromani (cha Kusini mwa Ugiriki) kuligusa moyo wangu. Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba alikuwa ‘amehuzunika sana, kiasi cha kufa.’ Hata hivyo, alimwomba Yehova ampe nguvu za kufanya mapenzi yake. Kuelewa mistari hiyo vizuri kunanionyesha kwamba si vibaya kuhuzunika wakati mwingine. Isitoshe, mistari hiyo inanikumbusha umuhimu wa kusali kwa bidii kwa Yehova na kumwomba anipe nguvu za kukabiliana na matatizo na pia inanisaidia kuwa tayari kuwaeleza ndugu na dada zangu jinsi ninavyohisi.

Tunashangilia pamoja na ndugu na dada zetu wanaozungumza Kiromani wanapoendelea kunufaika na zawadi hii ya thamani itakayowasaidia kumkaribia Yehova hata zaidi.​—Yakobo 4:8.