Hamia kwenye habari

Ndugu zetu nchini Ugiriki walipelekwa uhamishoni au wakafungwa gerezani kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. Hata hivyo, walijitahidi kadiri walivyoweza kuendelea na utendaji wao wa kitheokrasi kama vile kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo

DESEMBA 22, 2022
UGIRIKI

Miaka Mia Moja ya Kutojifunza Vita Tena

Miaka Mia Moja ya Kutojifunza Vita Tena

Nikos na Eleni Abatzis

Mwaka wa 2022 umekuwa mwaka muhimu kwa Mashahidi wa Yehova nchini Ugiriki kwa angalau sababu mbili. Kwanza, miaka 100 imepita tangu Mashahidi wa kwanza walipokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, na pili, miaka 25 imepita tangu utumishi wa badala wa kiraia ulipoanzishwa.

Katika miaka ya 1900, vita vilizuka nchini Ugiriki. Kwa sababu ya hali hizo, ndugu zetu walikabili tena na tena suala la kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. Ndugu Nikos Abatzis na Ndugu Nikolaos Rebebos walikuwa Mashahidi wa Yehova (wakati huo waliitwa Wanafunzi wa Biblia) wa kwanza nchini Ugiriki kukataa kwenda jeshini kwa sababu ya dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia.

Ndugu Abatzis alikataa kupigana katika vita vya Wagiriki dhidi ya Waturuki vya mwaka wa 1919-1922. Akizungumza kuhusu wakati huo Ndugu Abatzis alisema: “Nilitumwa kwenye kambi ya kijeshi [iliyokuwa Asia Ndogo] . . . Nikiwa huko nilipata ujasiri na nikaanza kuwahubiria [wanajeshi] na kuwaeleza kwamba vita havipatani na ujumbe ulio kwenye vitabu vya Injili kwani vinatuambia kwamba tunapaswa kuwapenda adui zetu.” Vita vilipokwisha, Ndugu Abatzis aliendelea kuhubiri ujumbe wa Biblia katika sehemu mbalimbali za Ugiriki.

Nikolaos Rebebos na mke wake

Nikolaos Rebebos alikuwa mwanajeshi na alipigana katika vita hivyo vya Wagiriki na Waturuki. Lakini aliposoma Maandiko na trakti aliyokuwa amepewa na Wanafunzi wa Biblia, maoni yake kuhusu vita yalibadilika. Hatimaye, aliwaambia wakubwa wake kazini kwamba hangepigana tena, hata ingawa alijua kwamba kufanya hivyo kungemletea adhabu ya kuuawa kwa kupigwa risasi na kikosi cha wanajeshi. Kwa ujasiri Nikolaos alitangaza kwamba ‘kwa msaada wa Mungu, hakuna hata unywele mmoja wa kichwa chake ambao ungeangamia.’ Vita vilipokwisha, aliwatafuta Wanafunzi wa Biblia na akabatizwa mwaka wa 1925.

Ndugu Abatzis na Ndugu Rebebos walikuwa wa kwanza kati ya ndugu wengi kutoka Ugiriki ambao walikataa kuwa wanajeshi licha ya kushurutishwa kufanya hivyo. Katika Vita vya Pili vya Ulimwengu na katika Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Ugiriki vya mwaka wa 1946-1949, ndugu zetu walikataa kata kata kujiunga na jeshi au makundi ya waasi, na hata baadhi yao waliuawa. Akina ndugu hawakuruhusu mateso yawazuie, bali waliendelea kuhubiri ujumbe wenye amani wa Biblia, na idadi ya Mashahidi nchini Ugiriki iliendelea kuongezeka kutoka 178 katika mwaka wa 1940 hadi 2,808 katika mwaka wa 1949.

Leo, Mashahidi wanahubiri habari njema kwa bidii nchini Ugiriki

Wale waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri waliendelea kutupwa gerezani. Kwa ujumla akina ndugu 3,788 walifungwa gerezani kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. Hatimaye katika mwaka wa 1997, Ugiriki ilipitisha sheria iliyoidhinisha utumishi wa badala wa kiraia. Kwa sasa, akina ndugu 100 wamekubali kufanya utumishi wa badala wa kiraia.

Katika mwaka wa utumishi wa 2022, Ugiriki ilikuwa na kilele cha wahubiri 27,995 na watu 420 walibatizwa.

Miaka mia moja ambayo imepita inaonyesha wazi kwamba Yehova amekuwa akiwategemeza ndugu zetu nchini Ugiriki wanaposonga mbele katika azimio lao la kutojifunza vita tena.​—Isaya 2:4.