Hamia kwenye habari

Majengo ya mahakama nchini Uingereza yaliyo na Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa ya Uingereza na Wales

MEI 12, 2020
UINGEREZA

Uingereza Yatetea Haki ya Kuamua Nani Anastahili Kuwa Mshiriki wa Dini

Uingereza Yatetea Haki ya Kuamua Nani Anastahili Kuwa Mshiriki wa Dini

Machi 17, 2020, Mahakama ya Rufaa ya Uingereza na Wales ilikataa ombi la kukata rufaa dhidi ya uamuzi uliofanywa na Mahakama Kuu kuhusu haki yetu ya kufuata miongozo ya Biblia kuhusu kutenga na ushirika.

Katika uamuzi uliotia ndani mambo mengi, Mahakama Kuu ilikuwa imeamua kwamba si kinyume na sheria wala si kuharibu jina la mtu, kwa kutaniko kutangaza kwamba mtu fulani si Shahidi wa Yehova tena. Richard Spearman, Q.C, hakimu wa Mahakama Kuu, alisema hivi alipokuwa akisoma hukumu yake: “Ni jambo la kawaida kwamba kikundi cha kidini kinachojaribu kutii kanuni za Biblia kiwe na uwezo wa kumwondoa mtenda-dhambi. Hilo ni jambo linalopatana na akili, na la lazima, kwa sababu ikiwa mtu hawezi au hataki kutii kanuni za Maandiko, mbali na kwamba hastahili kuwa mshiriki wa kikundi kama hicho, asipoondolewa, anaweza kuwaathiri wengine walio waaminifu.”

Mlalamishi katika kesi hiyo alikata rufaa uamuzi huo kwenye Mahakama ya Rufaa ili kuomba ikiwa uamuzi huo wa mahakama unaweza kubadilishwa. Mahakama ya Rufaa ilikataa ombi lake, na kusema kuwa “halina msingi kabisa,” na ikasema kwamba uamuzi ulifanywa na mahakama kuu ulikuwa “sahihi kabisa” na kwamba “haki ya kumwondoa mtu inastahili kuwepo katika kikundi chochote cha kidini.”

Shane Brady, wakili wa Mashahidi wa Yehova, alisema hivi kuhusu uamuzi huo: “Uamuzi huo unapatana na maamuzi mengi sana yaliyofanywa katika mahakama za Uingereza, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, na mahakama za rufaa nchini Kanada, Barani Ulaya, na Marekani. Maamuzi yote hayo yanathibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova wana haki ya kuamua kuhusu masuala yanayohusiana na dini.”

Tunafurahi kwamba Mahakama hiyo ilitambua haki yetu ya kufuata Maandiko ili kulinda hali ya kiroho na ya kiadili ya makutaniko.—1 Wakorintho 5:11; 2 Yohana 9-11.