Hamia kwenye habari

Washiriki wa familia ya Falcone wakiwa katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova

MACHI 3, 2017
UJERUMANI

Mahakama za Ujerumani Zatambua Makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova Kuwa Sikukuu za Kidini

Mahakama za Ujerumani Zatambua Makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova Kuwa Sikukuu za Kidini

Aprili 2012, mtoto mwenye umri wa miaka saba anayeitwa Vivienne Falcone alipeleka barua kwenye ofisi ya mkuu wa shule kutoka kwa wazazi wake. Barua hiyo iliomba mtoto huyo aruhusiwe kutofika shuleni kwa siku moja. Familia yake ilipanga kuhudhuria kusanyiko la kidini la siku tatu la Mashahidi wa Yehova ambalo lingefanya jijini Mainz. Wasimamizi wa shule walikataa ombi la familia la kutaka Vivienne aruhusiwe kutoenda shule siku ya Ijumaa kwa ajili ya kuhudhuria kusanyiko. Hata hivyo, wazazi wa Vivienne walipofikiria elimu ya kiroho ambayo mtoto wao angepata walichochewa kwenda naye kusanyikoni licha ya kutopewa ruhusa. Wazazi wa Vivienne walikata rufaa kwenye Baraza la Taifa la Elimu (State Board of Education) kupinga uamuzi huo wa wasimamizi wa shule. Badala ya baraza hilo kutambua kwamba kusanyiko ni sikukuu za kidini, liliamuru wazazi hao walipe ada fulani.

Kukataa kwa Baraza hilo kungeweza kuwa na matokeo mabaya kwa wazazi wa Vivienne kwa sababu chini ya sheria ya Ujerumani, kutohudhuria shule bila sababu ya msingi kulionekana kuwa ni kosa la mzazi kukiuka wajibu wake wa kisheria wa kumpeleka mtoto shuleni. Mtuhumiwa katika kisa kama hicho anaweza kupewa adhabu ya kutozwa faini au hata kufungwa katika visa fulani vilivyopita kiasi. Kwa ujumla, wazazi wa Vivienne waliuona uamuzi huo kuwa unavunja uhuru wao wa kuabudu na haki yao ya kumlea mtoto wao kulingana na imani yao ya kidini.

Kesi Kuhusu Haki ya Sikukuu za Kidini

Wazazi wa Vivienne, Stefano na Elisa, walifungua kesi kwenye mahakama ya utawala kupinga uamuzi wa Baraza hilo. Walieleza kwamba kufanya ibada siku nzima kuliwapa nafasi ya kumwabudu Mungu pamoja wakiwa familia na kujenga imani. Walisema hivi: “Makusanyiko yetu yanafanyika mara moja kwa mwaka na ndiyo matukio ya pekee katika dini yetu.” a Mahakama ilitoa uamuzi uliowaunga mkono wazazi ikitambua kwamba makusanyiko hayo ya eneo ya Mashahidi wa Yehova yanayofanywa mara moja kwa mwaka ndiyo sikukuu za kidini. Baraza hilo lilikata rufaa likidai kwamba makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova si sikukuu za kidini kwa sababu ni matukio tu wanayofurahia na wala hayatambuliki kama siku za pekee ambazo zinajulikana kuwa takatifu kama vile Krismasi, Ista au sikukuu za kitaifa.

Julai 27, 2015, Mahakama Kuu ya Utawala ya Hesse iliunga mkono uamuzi wa mahakama ya chini. Mahakama hiyo kuu ilitangaza kwamba maana ya sikukuu za kidini inategemea hasa maoni ya dini yenyewe. Mahakama iliona tofauti ya wazi kati ya masuala ya dini na ya Nchi, iliposema hivi: “Nchi haipaswi kuvunja uhuru uliotolewa katika Sheria ya Msingi [yaani, Katiba ya Ujerumani] kwa makanisa na dini na mashirika ya kidini na uhuru wa kuongoza mambo yao ya kidini.” Nchi ina “wajibu wa kudumisha msimamo wa kutopinga dini yoyote na itikadi zake.”

Mahakama kuu pia ilirejelea tovuti rasmi ya Mashahidi wa Yehova, tovuti hiyo hueleza kwamba Mashahidi huyaona makusanyiko yao kuwa sikukuu za kidini. Mahakama ilieleza kwamba kwa kukataa ombi la familia ya Falcone kwa ajili ya binti yao kutohudhuria shule, Baraza hilo “lilimnyima mtoto haki ya uhuru wa ibada . . . pamoja na haki ya wazazi . . . kuwazoeza watoto wao mambo ya kidini na itikadi zake.” Mahakama ilimalizia kwa kusema kwamba maoni ya Baraza hilo “yalikuwa kinyume kabisa na msimamo wa kutopinga dini yoyote ambao Nchi inapaswa kuuzingatia.”

“Kushiriki katika tukio la sherehe ya kidini kunaweza kuwa sababu muhimu ya kuruhusiwa kutohudhuria masomo ya shule.”—Mahakama Kuu ya Utawala ya Hesse

Elimu Yenye Usawaziko

Baada ya kupokea maamuzi hayo ya hukumu yaliyowaunga mkono, wazazi wa Vivienne walisema hivi: “Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunaiona elimu inayotolewa shuleni kuwa kitu muhimu sana, na tunajaribu kuwachochea watoto wetu wapende kujifunza. Pia, tunaithamini sana elimu ya kidini kwa sababu inawafundisha watoto wetu kusitawisha upendo kwa mambo ya kiroho na kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu, ambao unawasaidia kuwa na upendo, kuwajali wengine, na kuwa wenye busara na usawaziko. Tunawashukuru sana wenye mamlaka wa kisheria kwa uamuzi wao.”

Armin Pikl, wakili wa familia ya Falcone, alisema hivi: “Uamuzi huo umeonyesha kwamba makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova yanatambuliwa kuwa matukio matakatifu sana na unathibitisha kwamba wazazi wana haki ya kuwaelimisha watoto wao kulingana na imani ya dini yao. Mashahidi wa Yehova ambao ni wanafunzi watanufaika katika miaka yote watakayokuwa shuleni kwa kupata ruhusa ya kuhudhuria siku zote za makusanyiko hayo yenye kujenga imani. Ninatumaini mahakama katika nchi nyingine zitazingatia uamuzi huu bora wanaposikiliza kesi zinazohusiana na mambo kama hayo.”

a Makusanyiko ya eneo, mwanzoni yalikuwa yakiitwa makusanyiko ya wilaya, ni matukio ya kidini ya kila mwaka yanayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Programu hiyo ya siku tatu ya elimu ya kidini huwafundisha vijana kwa wazee jinsi ya kutumia kanuni za Biblia katika maisha yao ya kila siku.