Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 12, 2014
UJERUMANI

Makumbusho ya Sachsenhausen kwa Ajili ya Shahidi wa Yehova Aliyeuawa na Wanazi

Makumbusho ya Sachsenhausen kwa Ajili ya Shahidi wa Yehova Aliyeuawa na Wanazi

SELTERS, Ujerumani—Septemba 16, 2014, shirika la Wakfu wa Ukumbusho wa Brandenburg litafanya tukio la pekee la kukumbuka miaka 75 tangu August Dickmann alipouawa hadharani kwenye kambi ya mateso ya Sachsenhausen. Alikuwa mtu wa kwanza kuuawa hadharani na Wanazi kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu.

August Dickmann, 1936 hivi.

Oktoba 1937, Bw. Dickmann alifungwa katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen kwa sababu ya msimamo wake akiwa Shahidi wa Yehova. Siku tatu baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuanza katika mwaka wa 1939, askari wa Gestapo alimwita Bw. Dickmann na kumtaka atie sahihi kitambulisho cha kijeshi. Kwa kufanya hivyo angekuwa amekubali kujiunga na jeshi la Ujerumani. Bw. Dickmann alipokataa kutia sahihi, alifungwa kifungo cha upweke na kamanda wa kambi hiyo akamwomba ruhusa mkuu wa askari wa SS ili amwue Bw. Dickmann mbele ya wafungwa wote. Septemba 15, 1939, mamia ya Mashahidi wa Yehova, kutia ndani Heinrich, ndugu ya Bw. Dickmann, walilazimishwa kutazama tukio hilo. Siku mbili baadaye, gazeti The New York Times liliripoti hivi kutoka Ujerumani: “August Dickmann, mwenye umri wa miaka 29, . . . amepigwa risasi na kikundi cha askari.” Gazeti hilo liliendelea kusema kwamba alihukumiwa kwa kukataa kujiunga na jeshi “kwa sababu ya msimamo wa kidini.”

Septemba 18, 1999, bamba liliwekwa kwenye ukuta wa nje wa kambi ya Sachsenhausen ili kuwakumbuka zaidi ya Mashahidi 890 wa Yehova waliofungwa kwenye kambi hiyo. Pia, jiwe la kumbukumbu lilisimamishwa kwa ajili ya Bw. Dickmann.

Maadhimisho hayo yataanza katika eneo la kumbukumbu ya Bw. Dickmann, kisha hotuba zitatolewa katika eneo lililokuwa jiko la wafungwa. Dakt. Detlef Garbe, mwanzilishi na mkurugenzi wa Makumbusho ya Kambi ya Mateso ya Neuengamme, atakuwa msemaji mkuu.

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000

Ujerumani: Wolfram Slupina, simu +49 6483 41 3110