Hamia kwenye habari

Ofisi ya Jimbo la North Rhine-Westphalia

OKTOBA 10, 2017
UJERUMANI

Ujerumani Imewapa Mashahidi wa Yehova Usajili wa Pekee wa Kisheria

Ujerumani Imewapa Mashahidi wa Yehova Usajili wa Pekee wa Kisheria

Baada ya kuendesha kesi kwa miaka 26, hatimaye Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani walipata haki ya kusajiliwa kisheria kama dini nyingine kubwa katika nchi hiyo. Januari 27, 2017, jimbo la North Rhine-Westphalia ndilo lilikuwa la mwisho kati ya majimbo 16 kuwapa Mashahidi wa Yehova usajili huo wa pekee wa kisheria. Uamuzi huo una manufaa makubwa sana kwa Mashahidi kwa sababu ingawa wamekuwepo nchini Ujerumani kwa zaidi ya miaka 100, makao yao makuu ya taifa na maelfu ya makutaniko nchini humo yalikuwa yakionekana kama mashirika ya kidini yanayojitegemea ambayo hayana uhusiano wowote. Sasa, kwa kuwa Mashahidi wamepata usajili huo wa pekee wa kisheria katika kila jimbo nchini Ujerumani, wanatambuliwa kuwa shirika moja la kidini na wanafurahia faida za kutambuliwa kwa njia hiyo kisheria.

Pambano la Muda Mrefu la Kuomba Usajili wa Pekee wa Kisheria

Mwaka wa 1921, Mashahidi wa Yehova walisajiliwa kwa mara ya kwanza nchini Ujerumani chini ya sheria binafsi. Baada ya Ujerumani kuungana mwaka wa 1990, Mashahidi waliomba wapate usajili wa pekee wa kisheria kwa sababu ya manufaa ambayo mashirika ya kidini yaliyosajiliwa hupata.

Ili shirika la kidini lipate usajili wa pekee katika nchi nzima ya Ujerumani, sheria inalitaka kwanza lipate usajili wa pekee katika jimbo ambalo limeanzishwa. Halafu wanaweza kuomba usajili huo katika majimbo 15 yaliyobaki. Mwaka wa 1990, shirika la kidini la Ujerumani linaloitwa Jehovas Zeugen in Deutschland (Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani) lilituma maombi ya kupata usajili wa pekee katika jimbo la Berlin, eneo ambalo Mashahidi walitambuliwa kisheria kwa mara ya kwanza. Ingawa mashirika mengi ya kidini yanayotaka usajili wa pekee, hupatiwa usajili huo kwa muda mfupi sana, labda baada ya mwaka mmoja au miwili, lakini serikali ya jimbo la Berlin ilikataa kuwapa Mashahidi wa Yehova usajili huo wa pekeekwa miaka mingi. Sababu moja kuu ya kukataa ni kwamba Mashahidi hawapigi kura wakati wa uchaguzi mkuu. Hata hivyo, mjadala huo hauna msingi, kwa sababu sheria haiwalazimishi raia wa Ujerumani kupiga kura; kupiga kura ni suala la hiari.

Mwishowe, suala hilo lilipelekwa mahakamani. Machi 24, 2005, Mahakama Kuu ya Berlin ilitoa uamuzi kwamba Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani wanapaswa kutambuliwa kuwa “taasisi yenye usajili wa pekee wa kisheria.” Zaidi ya mwaka mmoja baadaye, jimbo la Berlin lilikubali kuwapa Mashahidi wa Yehova usajili huo wa pekee wa kisheria, baada ya mapambano ya kisheria ya miaka 16.

Baada ya hapo, Mashahidi walituma maombi ya usajili wa pekee wa kisheria katika majimbo 15 ya Ujerumani yaliyobaki. Mwaka wa 2009, majimbo 11 yaliwapa usajili wa pekee wa kisheria; na mengine 3 yalifanya hivyo katika miaka iliyofuata; na mwishowe, Januari 27, 2017 jimbo la North Rhine-Westphalia liliwapa Mashahidi wa Yehova usajili wa pekee wa kisheria. Mashahidi walijitahidi bila kuacha kutafuta usajili wa pekee wa kisheria ambao dini zote kubwa zinapata na hatimaye, baada ya miaka 26 walifanikiwa.

Faida za Usajili wa Pekee wa Kisheria

Makao makuu ya taifa na makutaniko zaidi ya 2,000 ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, sasa yana shirika moja la kisheria. Zamani kila shirika liliwakilisha kutaniko moja hivi, na kulingana na sheria ya nchi walihitaji kutoa ripoti ya shirika kila mwaka na kulipa kodi. Mabadiliko yoyote katika muundo wa shirika ambayo yalitokana na mambo kama vile kuwekwa rasmi kwa wazee wapya wa kutaniko, kununua mali, kubadili jina au kuunganishwa kwa makutaniko yalikuwa yakiripotiwa serikalini. Wakati huo, wazee wa kutaniko walitumia wakati mwingi na jitihada nyingi kutekeleza maagizo hayo ya kutoa ripoti, lakini sasa wanaweza kukazia fikira zaidi kuwatunza kiroho wahudhuriaji wa kutaniko. Pia, kutokuwa na usajili wa pekee wa kisheria kulifanya makutaniko yalipe ada ya kushughulikiwa kwa ripoti. Mzee mmoja wa kutaniko wa muda mrefu alisema hivi: “Sasa tuna uhuru zaidi wa kutumia michango kwa ajili ya kutegemeza kazi ya kuhubiri ya wahudhuriaji wa kutaniko.”

Ingawa kuna Mashahidi 274,000 hivi na watu wengine ambao wanahudhuria katika mikutano ya Mashahidi nchini Ujerumani; Mashahidi wa Yehova wasingeonwa kuwa dini kubwa ikiwa hawangepata usajili huo bora wa kisheria. Armin Pikl, wakili wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, alisema hivi: “Katika kipindi chote cha miaka zaidi ya 26 ya jitihada za kutafuta usajili wa pekee wa kisheria, vyombo vya habari vilichapisha mamia ya habari zisizo za kweli na za kutuharibia jina, wakati mwingine habari hizo zilitolewa kila juma. Sasa habari hizo za uwongo na za kutuharibia jina hazitolewi tena.” Werner Rudtke, Shahidi wa muda mrefu, alisema hivi: “Kwa kuwa shirika la kidini ambalo linataka usajili wa pekee wa kisheria linapaswa kutii sheria katika kila njia, yale madai yasiyo ya kweli kuhusu Mashahidi yanaweza kuthibitika kuwa ya uwongo.” Shahidi mwingine anayeitwa Petra, alieleza changamoto walizokabili wanafunzi shuleni. Alisema hivi: “Usajili huo wa pekee wa kisheria ni msaada mkubwa kwa wanafunzi shuleni. Mpaka sasa imekuwa tabia ya walimu kuwabagua wanafunzi ambao ni Mashahidi kwa sababu ya habari za uwongo kwamba Mashahidi ni ‘madhehebu’ si dini.”

Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani wanashukuru kwamba utendaji wao wa kidini wa unyoofu umetambuliwa na serikali kwamba unastahili usajili wa pekee wa kisheria. Wanatumaini kwamba kutambuliwa huko kutaondoa baadhi ya changamoto walizokabili zamani na watanufaika kibinafsi na kama shirika la kidini.