Hamia kwenye habari

DESEMBA 12, 2019
UKRAINIA

Mahakama Kuu ya Ukrainia Yatetea Haki ya Kutumia Jumba la Ufalme

Mahakama Kuu ya Ukrainia Yatetea Haki ya Kutumia Jumba la Ufalme

Baada ya mapambano ya kisheria yaliyoendelea kwa miaka minne, Mashahidi wa Yehova walio katika mji wa Tetiiv, Ukrainia wameruhusiwa kutumia Jumba lao la Ufalme kwa ajili ya ibada. Ingawa ndugu zetu walimaliza kujenga Jumba lao la Ufalme Desemba 2014, mara kwa mara Baraza la Ujenzi la Nchi (SABC) liliwakataza kutumia jumba hilo: katika pindi sita tofauti lilikataa kuwapa kibali cha kulitumia, limekuwa likitoza kutaniko hilo faini kubwa, na hata lilifuta kibali chao cha kujenga, licha ya kwamba ujenzi ulikuwa umeshakamilika.

Oktoba 10, 2018, Mahakama Kuu ya Ukrainia iliwaunga mkono ndugu zetu kwa kuwa walitii sheria za ujenzi. Pia mahakama hiyo ilisisitiza kwamba haki ya kujenga jengo kwa ajili ya ibada inalindwa na Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu. Machi 28, 2019, mkurugenzi mpya wa SABC aliwapatia ndugu zetu kibali walichohitaji ili kutumia jumba hilo. Kutaniko hilo lilifanya mkutano wake wa kwanza katika Jumba hilo mwezi huohuo.

Novemba 2, 2019, ndugu hao waliwakaribisha wenyeji wa eneo hilo kutembelea Jumba lao. Wakuu wa jiji na wilaya pamoja na majirani wengine walihudhuria tukio hilo. Anatoliy Fedorovych Zavalniuk, Msanifu Majengo Mkuu wa Wilaya ya Tetiiv, alisema hivi: “Mmefuata sheria zote na matakwa yote ya nchi yanayohusu ujenzi na hata mmefuata mipango ambayo imepitishwa na Uongozi wetu. Nyumba hii ya ibada inafanya sehemu hii ya mji ivutie. Ninashukuru kwa kazi yenu”

Ushindi huu unatupa sababu ya kushangilia na ndugu zetu walio Tetiiv. Tunafurahi sana kujua kwamba sasa wanaweza kutumia Jumba lao la Ufalme kumsifu na kumtukuza Yehova.—Zaburi 69:30.