Hamia kwenye habari

NOVEMBA 20, 2020
UKRAINIA

Mahakama ya ECHR Yatoa Uamuzi Unaotetea Mashahidi wa Yehova Nchini Ukrainia

Mahakama ya ECHR Yatoa Uamuzi Unaotetea Mashahidi wa Yehova Nchini Ukrainia

Mahakama yashutumu kitendo cha Ukrainia kutochukua hatua dhidi ya uhalifu wa chuki ya kidini wanaofanyiwa ndugu zetu

Novemba 12, 2020, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR), ilitoa uamuzi mara tatu unaotetea Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia. Kesi hizo ni Zagubnya and Tabachkova v. Ukraine, Migoryanu and Others v. Ukraine, na Kornilova v. Ukraine. Kesi hizo zilipelekwa Mahakamani mwaka wa 2014 na 2015. Kila kesi ilihusisha visa ambapo maofisa wa usalama walishindwa kuchukua hatua yoyote baada ya Mashahidi wa Yehova kushambuliwa vibaya sana. ECHR ilitangaza kwamba wenye mamlaka nchini Ukrainia hawakulinda kikamili haki za ndugu zetu na ikaagiza kwamba ndugu hao walioshambuliwa walipaswa kulipwa fidia ya kiasi cha euro 14,700 (dola 17,400 za Marekani).

Kesi ya Zagubnya and Tabachkova v. Ukraine: Aprili 20, 2009, Dada Zagubnya na Tabachkova walikuwa wakishiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba katika kijiji cha Novi Mlyny. Wakati ambapo Mykola Lysenko, kasisi wa Kanisa la Othodoksi, alipokutana na dada hao barabarani na kisha kuwapiga vibaya sana kichwani na mgongoni kwa kutumia fimbo ya mbao. Mshambuliaji huyo hakuchukuliwa hatua yoyote ijapokuwa kasisi huyo alikiri kwamba alitaka “kuwaogopesha” dada zetu ili “waache kazi yao.”

Kesi ya Migoryanu and Others v. Ukraine: Aprili 5, 2012, Mashahidi wa Yehova ishirini na moja pamoja na wageni wao, walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo wakati ambapo kundi la watu lililoongozwa na Kasisi O. Greku wa Kanisa la Othodoksi la Moscow, lilipovuruga mkutano huo. Kundi hilo lilitoa matusi na kuwatisha wahudhuriaji waliotia ndani watoto na wanawake wenye umri mkubwa.

Baada ya muda, kasisi huyo na watu wake waliendelea kuwashambulia Mashahidi wa Yehova kwa kuwapiga akina ndugu, wakachoma moto gari la ndugu mmoja, na kurusha bomu la mkono walilotengeneza katika nyumba iliyokuwa na Mashahidi waliokuwa wamelala. Baada ya kutendewa kwa jeuri, waathiriwa walitoa taarifa polisi na kupeleka ushahidi. Katika visa fulani, washambuliaji hao walirekodiwa katika video. Hata hivyo, polisi walikataa kutambua kwamba mashambulizi hayo yalichochewa na chuki ya kidini na walidai kwamba hawakuweza kuwatambua washambuliaji katika video. Kasisi na watu wake hawakuchukuliwa hatua yoyote.

Kesi ya Kornilova v. Ukraine: Machi 7, 2013, katika mji wa Nosivka, Dada Kornilova na Serdiuk walikuwa wakiwaalika jirani zao wahudhurie Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Mwanamume mmoja akaanza kuwatukana na kukashifu imani ya dada zetu. Kisha akampiga Dada Kornilova ngumi ya uso kwa nguvu sana hivi kwamba alipata jeraha baya. Dada alilazwa hospitalini kwa siku 11. Polisi walikataa kukubali kwamba shambulizi hilo lilichochewa na chuki ya kidini badala yake walisema kwamba dada yetu alishambuliwa kwa sababu ya “chuki binafsi.” Mahakama ilitoa uamuzi wa kumtoza faini ndogo aliyemshambulia dada yetu.

Kuanzia kushoto hadi kulia: Dada Tetyana Kornilova, Dada Tetiana Zagubnya, Dada Maria Tabachkova, na Ndugu Vasyl Migoryanu. Mashahidi wa Yehova wanne kati ya wengi walioshambuliwa kati ya 2009 na 2013, na watu waliochochewa na chuki ya kidini nchini Ukrainia

Wawakilishi wa ofisi ya tawi ya Ukrainia walikutana mara nyingi na wenye mamlaka kuanzia ngazi ya chini, taifa, na kimataifa ili kuzungumzia mateso hayo. Baada ya kutumia njia zote hizo, akina ndugu walianza kufungua kesi katika mahakama ya ECHR mwaka wa 2014. Inashangaza kwamba, mwaka mmoja kabla, maofisa walianza kuweka rekodi ya uhalifu kwa sababu ya dini nchini Ukrainia. Ripoti ya mwaka wa 2013 iliyotolewa na Mchunguzi wa Malalamiko ya Wananchi wa Ukrainia ilisema hivi: “Kwa kuwa upelelezi wa makosa ya uhalifu haukukamilika, wahalifu hao waliachiliwa wafanye vitendo hivyo.” Pia, katika ripoti yake ya mwaka wa 2013 kuhusu Ukrainia, Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa ilisema kwamba ilikuwa na wasiwasi sana kwamba uhalifu unaochochewa na chuki, kutia ndani dhidi ya Mashahidi wa Yehova, unaonekana kuwa uhalifu usiostahili adhabu kali nchini Ukrainia. Kamati hiyo ilifikia mkataa kwamba serikali ya Ukrainia inapaswa “kuongeza jitihada zake ili kuhakikisha kwamba tuhuma za uhalifu unaochochewa na chuki zinafanyiwa upelelezi wa kutosha, wahusika wanashtakiwa . . . na, ikiwa watahukumiwa, basi wapewe adhabu wanayostahili, na kwamba waathiriwa wanalipwa fidia inayostahili.”

Katika miaka ya hivi karibuni, serikali ya Ukrainia imeanzia kuchukua hatua ili kuboresha hali. Ingawa Mashahidi wa Yehova wanafurahia uhuru wa kuabudu katika nchi hiyo, tunatumaini kwamba maamuzi ya ECHR katika kesi hizo tatu yatachochea vyombo vya usalama nchini Ukrainia na nchi nyingine kuendelea kulinda uhuru wa ibada wa ndugu na dada zetu. Tunatazamia kwa hamu wakati ambapo Yehova, ambaye “njia zake zote ni haki,” atakomesha mateso yote wanayopata waabudu wake.—Kumbukumbu la Torati 32:4.