Hamia kwenye habari

Dada Olena mbele ya nyumba yake, ambayo iliharibiwa vibaya na kombora lililolipuka karibu nayo. Akina ndugu na dada walikuja kumsaidia bila kukawia

JULAI 4, 2022
UKRAINIA

RIPOTI YA 10 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

“Wao ni Wenye Ujasiri, Wanawatunza Wengine, na Wanategemeka”

RIPOTI YA 10 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Ndugu na dada zetu nchini Ukrainia wanaendelea kutegemezana na kuonyeshana upendo usio na ubinafsi.

Dada Olena ana umri wa miaka 81. Juni 6 kombora lililipuka karibu sana na nyumba yake. Kombora hilo liliharibu kabisa nyumba ya jirani yake, na likachimba shimo lenye kina cha mita saba. Mlipuko huo ulikuwa na nguvu sana hivi kwamba hata nyumba ya Dada Olena ilipata uharibifu mkubwa.

Dada Olena anasema hivi: “Nilikuwa nimelala na ghafula ukuta ukaanguka karibu tu na kichwa changu. Hewa ilikuwa imejaa vumbi nyeusi. Mawe na vioo vilikuwa vimetapakaa kila mahali. Nilimshukuru Yehova kwa sababu nilikuwa hai.” Ndugu na dada wanaoishi kwenye eneo hilo walikuja kumwona Dada Olena dakika chache tu baada ya mlipuko huo. Nyumba ya mmoja wa akina ndugu hao, ilikuwa pia imeharibiwa vibaya. Dada Olena anaendelea kusema: “Akina ndugu walipofika, walipigwa na butwaa hawakujua waseme nini. Nilitiwa moyo sana nilipowaona. Nilifurahi sana kwamba walikuwa pamoja nami.”

Serhii, ni mzee wa kutaniko ambaye humtembelea Dada Olena kwa ukawaida na mara nyingi anamtembelea akiwa na vijana wa kutaniko lao. Anasema hivi: “Niliposikia kwamba kuna mlipuko ambao umetokea karibu na nyumba ya Dada Olena, nilikuwa na hofu na wasiwasi mwingi. Wasiwasi wangu ulipungua nilipoona kwamba alikuwa amejeruhiwa kidogo tu. Inashangaza kwamba, kitu cha kwanza ambacho Dada Olena aliomba baada ya nyumba yake kuharibiwa, ni machapisho yanayotegemea Biblia ambayo alikuwa amepata siku kadhaa mapema.”

Inapendeza kwamba, watu wake wa ukoo wamepata mahali pengine ambapo anaweza kuishi. Kutaniko linaendelea kumsaidia Dada Olena, na wazee huwasiliana naye kila siku. Ndugu na dada walimpa Dada Olena kifaa kinachomsaidia kusikia ili aweze kunufaika na mikutano ya kutaniko. Dada Olena anasema hivi: “Wakati mwingine nguvu zinaniishia, lakini mikutano inanipa nguvu tena. Waabudu wenzangu hunipigia simu mara nyingi na ninawashukuru sana.”

Wenzi fulani wa ndoa walisimulia kuhusu mambo waliojionea walipokuwa wamejificha kwenye chumba cha chini cha Jumba la Ufalme, wakiwa pamoja na wahubiri wengine 200. Mke anasema hivi: “Niliguswa moyo sana na jinsi wazee walivyotunza wahubiri kwa upendo. Mfano wao ulinikumbusha kumhusu Daudi ambaye alihatarisha uhai wake alipopigana na simba na dubu ili kuwaokoa kondoo. Wazee tuliokuwa nao humo walihatarisha uhai wao walipoenda kutafuta chakula na maji, na pia petroli ili tuweze kuwa na mwangaza. Kwa sababu ya maandalizi hayo, tulifaulu kuwa na mikutano ya kutaniko na mikutano ya utumishi wa shambani. Hata milipuko ya makombora ilipozidi, wazee hao waliwatembelea kwa ukawaida ndugu na dada ambao walikuwa wamebaki katika nyumba zao, na kuwaletea chakula na maji na pia kuwafariji. Ninawaheshimu sana wazee hao. Kabla ya matukio haya, nilijua kwamba wazee ni walimu na wahubiri, lakini sasa ninajua kwamba wao pia ni wachungaji wenye kutegemeka. Ninathamini sana kwamba wao ni wenye ujasiri, wanawatunza wengine, na wanategemeka!”

Wahubiri wa kutaniko moja nchini Ukrainia waliiandikia ofisi ya tawi ya Ukrainia maneno haya kuwahusu wale wanaoongoza katika jitihada za kutoa msaada: “Mioyo yetu imejaa shukrani. Tunastaajabia jinsi Yehova anavyotutunza kupitia waabudu wenzetu. Kwa kweli, tumejionea utimizo wa maneno haya aliyosema Yesu: ‘Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.’”​—Yohana 13:35.

Kufikia Juni 21, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 42 wamekufa

  • Wahubiri 83 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 31,185 wameacha makao yao na kwenda sehemu zilizo salama zaidi nchini

  • Nyumba 495 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 557 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 1,429 zimepata uharibifu mdogo

  • Majumba 5 ya Ufalme yameharibiwa kabisa

  • Majumba 8 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 34 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 27 za kutoa msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Watu 52,348 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 23,433 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu