Hamia kwenye habari

Wahubiri wawili wakishiriki mahubiri ya hadharani nchini Ukrainia

JULAI 18, 2022
UKRAINIA

RIPOTI YA 11 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

“Kufanya Mema” Katika Nchi ya Vita

RIPOTI YA 11 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Ndugu na dada nchini Ukrainia wamepata shangwe kwa sababu wamepata nafasi ya kushiriki tena katika mahubiri ya hadharani, na hata wamejionea mambo mbalimbali yenye kupendeza. Waangalizi wa mzunguko na wazee wa makutaniko wanaripoti kwamba watu wengi wamefurahi kuona kwamba tumerudia tena utendaji wetu, wanafurahi kuona vigari vya machapisho, hata kuna waliosema kwamba walipenda kuwaona Mashahidi wa Yehova kwenye ujirani wao na walikosa hilo sana.

Tatiana kutoka kutaniko la Serhiivka lililo kwenye eneo la Odesa aliamua kuwatembelea wale aliokuwa amewahubiria kabla ya janga. Anaeleza hivi, “Tangu mwanzo, nimeona baraka za Yehova katika jitihada zetu za kurudia utumishi huu.” Pindi moja, alimtembelea mwanamke aliyeacha kujifunza kabla ya janga. Wakati huu, mwanamke huyo alitamani sana kuzungumzia mambo ya kiroho na alikuwa tayari kujifunza Biblia. Tatiana anamalizia kwa kusema, “Ninahitaji kutembelea marudio yangu yote na kuwaalika kujifunza Biblia tena!”

Yevheniy na Lilia ni wahubiri waliokimbia jiji la Mariupol. Walilazimika kuacha makazi yao na sasa wanaishi katika eneo salama nchini Ukrainia. Wote wawili wanashiriki katika kazi ya kuhubiri kwa ukawaida. Wanaeleza kwamba kuhubiri kumewasaidia kuacha kufikiria kuhusu matatizo yao. Wanasema: “Tunajua kwamba maisha yetu hayawezi kurudia tena hali yake ya kawaida. Si rahisi kuanza maisha mapya, lakini tunakumbuka kwamba sikuzote Yehova atawatunza watumishi wake. Tuna roho yake, na ndugu zetu wapo tayari kutusaidia kuanza maisha mapya kwenye eneo jipya.”

Kwenye maeneo mengine ya nchi hiyo, ndugu zetu wanatoa ushahidi pia kwa kazi zao njema. Kwa mfano, kikundi cha akina ndugu katika jiji la Mykolaiv kilisaidia shirika moja la kimataifa la kutoa misaada kukarabati na kupanga ghala linalotumika kuhifadhia misaada. Akina ndugu walirekebisha mfumo wa maji, walitengeneza makabati yasiyo na milango, na kupanga tani kadhaa za bidhaa. Mwakilishi wa shirika hilo la kimataifa la kutoa msaada alipokagua kazi zilizofanywa, alitokwa na machozi. Alisema, “sikutarajia kazi ingefanya vizuri namna hii.”

Ingawa waabudu wenzetu wanapitia nyakati ngumu nchini Ukrainia, wanapata shangwe inayotokana na kushiriki katika huduma kwa ukawaida na kwa “kufanya mema.”​—Wagalatia 6:9.

Kufikia Julai 13, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 42 wamekufa

  • Wahubiri 97 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 28,683 wameacha makao yao na kwenda sehemu zilizo salama zaidi nchini

  • Nyumba 524 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 588 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 1,554 zimepata uharibifu mdogo

  • Majumba 5 ya Ufalme yameharibiwa kabisa

  • Majumba 10 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 36 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 27 za kutoa msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Watu 52,947 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 23,863 wamekimbilia nchi nyingine na wamesaidiwa na waamini wenzetu