Hamia kwenye habari

Ubatizo uliofanyika nchini Ukrainia Julai 23, 2022

AGOSTI 12, 2022
UKRAINIA

RIPOTI YA 12 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

“Hata Vita Haviwezi Kusimamisha Kazi ya Kufanya Wanafunzi”

RIPOTI YA 12 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Kuanzia Julai 23 hadi 31, baadhi ya wahubiri ambao hawajabatizwa nchini Ukrainia na pia wengine kutoka Ukrainia ambao walikimbilia nchi nyingine, walibatizwa katika Kusanyiko la “Fuatilia Amani!” Kufikia Agosti 2, jumla ya watu 1,113 kutoka Ukrainia walibatizwa. Ndugu mmoja nchini Ukrainia alisema: “Hata vita haviwezi kusimamisha kazi ya kufanya wanafunzi, ni kama tu Yesu alivyoahidi: ‘Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote.’”​—Mathayo 28:20.

Tunafurahi sana kuripoti masimulizi yafuatayo.

Natalia, mwenye umri wa miaka 63 ni mwenyeji wa mji wa Kreminna, ulio katika Eneo la Luhansk. Yeye na binti zake wawili walianza kujifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1990 hivi. Binti zake walifanya maendeleo na wakabatizwa, lakini yeye hakufanya maendeleo. Vita vilipoanza, familia moja ya Mashahidi wa Yehova walikimbia pamoja na Natalia kwenda kwenye eneo lenye usalama zaidi. Natalia alikaa kwa muda kwenye Jumba moja la Ufalme lililo Ivano-Frankivsk.

Natalia anasema: Baada ya kuona uharibifu mwingi uliosababishwa na makombora, ni kana kwamba nilisahau jinsi ya kutabasamu. Ndugu na dada walinionyesha upendo wa kweli. Sikutarajia kwamba wangenitunza vizuri kiasi hicho. Wakati huo, upendo wangu kwa Yehova uliamshwa tena. Nilisoma sana Biblia, na dada mmoja akajitolea kujifunza nami kupitia kitabu Furahia Maisha Milele! Nilimwona dada huyo kuwa zawadi kutoka kwa Yehova.” Natalia anaendelea kusema: “Ninafurahi sana kwamba nimebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Ninataka kuishi kupatana na amri kuu zaidi: kumpenda Yehova Mungu wangu ‘kwa moyo wangu wote na kwa nafsi yangu yote na kwa akili yangu yote.’”​—Mathayo 22:37.

Olia, akiwa Poland, akiwa ameshika bango lililotengenezewa nyumbani lenye kichwa cha kusanyiko: “Fuatilia Amani”!

Olia kutoka Cherkasy alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa vita vilipoanza. Machi 6, yeye pamoja na binti yake na mjukuu wake walikimbilia Poland. Anasema hivi: “Tulifika tukiwa na mikoba yetu ya dharura tu, lakini ndugu na dada zetu wa kiroho walitutunza sote watatu. Mambo hayo yalinihakikishia kwamba tengenezo la Yehova lina umoja na linaongozwa na roho yake. Baada ya kujionea mambo hayo yote, niliazimia kutoka moyoni kujiweka wakfu kwa Yehova. Alinisaidia katika kipindi kigumu zaidi maishani mwangu, na sasa ningependa kumtumikia na kumwonyesha kwamba ninashukuru kwa yote aliyonifanyia.

Yulia kutoka Eneo la Donetsk ana umri wa miaka 18. Alilelewa katika familia ya Mashahidi lakini hakufanya maendeleo na kubatizwa. Anasimulia jambo lililofanyika muda mfupi baada ya vita kuanza. Anasema: “Nilikuwa nimelala sakafuni na nilijua ninaweza kufa wakati wowote. Mtaa ambao familia yetu iliishi uliharibiwa kabisa, lakini sisi tuliokoka. Baada ya kujionea jambo hilo na pia kusali na kutafakari kuhusu sifa za Yehova, nilimkaribia zaidi Yehova na nikaacha kuwa na shaka ikiwa nitajiweka wakfu kwa Yehova au la. Yehova alionyesha kwamba ananipenda kwa kujibu sala zangu. Nilikuwa na ujuzi tu kumhusu Mungu, lakini sasa ninampenda.” Yulia alibatizwa Julai 23.

David, mwenye umri wa miaka 11, kabla ya kubatizwa nchini Ujerumani

Vita vilipoanza, David mwenye umri wa miaka 11, pamoja na familia yao walikimbilia Ujerumani. Alikuwa ametumikia akiwa mhubiri ambaye hajabatizwa tangu alipokuwa na miaka tisa. Sasa anatazamia kwa hamu kufuatilia miradi yake ya kiroho. Anasema hivi: “Niliamua kubatizwa kwa sababu ninampenda Yehova na ningependa kuwa rafiki yake. Nilipobatizwa, nililia machozi ya furaha kwa sababu ya kuwa sehemu ya familia nzuri ya Yehova. Ninapenda kuwaambia watu kumhusu Yehova na kusudi lake kwa ajili ya wanadamu, kwa hiyo mradi wangu unaofuata ni kuwa painia. Ningependa pia kutumikia ndugu na dada zangu kutanikoni na ninatumaini siku moja nitakuwa mtumishi wa huduma. Mradi wangu mkuu ni kutumikia Betheli. Hiyo imekuwa ndoto yangu tangu nilipotembelea ofisi ya tawi jijini Lviv mwaka wa 2018.”

Olena kutoka Kyiv alianza kutumikia akiwa mhubiri ambaye hajabatizwa mwaka wa 2011. Alipoa kwa miaka kumi. Mwaka wa 2020, wazee waliwasiliana naye na wakampa broshua Mrudie Yehova. Anasema hivi: “Nilianza tena kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano. Hata hivyo, baada ya muda, niliacha tena. Vita vilipokuwa vikiendelea, Yehova alijibu sala zangu, nami nilitambua kwamba Yehova alikuwa amenilinda, alikuwa amenionyesha upendo, na alinikuwa amenipa amani ya moyoni. Nilikimbilia Rumania na huko niliwapata Mashahidi. Akina ndugu walinitunza na walinionyesha upendo, nilihisi kana kwamba Yehova ananifunika kwa blanketi lenye joto.” Olena alibatizwa Julai 23. Anamalizia kwa kusema: “Ninamshukuru sana Yehova kwa kunionyesha subira. Sasa ninajua kwamba ‘kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.’”​—Wafilipi 4:13.

Kufikia Agosti 2, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 43 wamekufa

  • Wahubiri 97 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 22,568 wameacha makao yao na kwenda sehemu zilizo salama zaidi nchini

  • Nyumba 586 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 613 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 1,632 zimepata uharibifu mdogo

  • Majumba 5 ya Ufalme yameharibiwa kabisa

  • Majumba 10 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 37 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 27 za kutoa msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Watu 53,836 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 24,867 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu