Hamia kwenye habari

NOVEMBA 16, 2022
UKRAINIA

RIPOTI YA 13 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Kazi ya Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba Yaanza Tena

RIPOTI YA 13 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Katika mwezi wa Agosti 2022, ilitangazwa kwamba ndugu na dada wanaweza kuanza tena kuhubiri nyumba kwa nyumba katika maeneo ya Ukrainia ambayo ni salama. Ndugu na dada zetu walikuwa na hamu ya kushiriki katika utumishi huo. Wamefurahi kuona kwamba watu wengi wanataka kusikiliza ujumbe wa Biblia. Mtu mmoja aliyekubali kujifunza Biblia alisema: “Baada ya kujionea mateso na maumivu ya vita vinavyoendelea, ninaamini kwamba ni Mungu tu anayeweza kutatua matatizo ya wanadamu.” Ndugu na dada zetu wamejionea mambo yafuatayo katika huduma:

Ruslan kutoka kutaniko la Lanivtsi, alikuwa na wasiwasi mwanzoni kuhusu kurejea katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Yeye na mke wake walisali na kumwomba Yehova awape ujasiri na pia awaongoze kwa watu wanaotaka kupata tumaini la wakati ujao. Wenzi hao wa ndoa walishangaa sana kwa sababu ndani ya saa mbili za kwanza walizungumza na watu nane, na wote walikubali kujifunza Biblia.

Olha kutoka kutaniko la Kremenets alikuwa katika huduma pamoja na mwandamani wake, mwanamume mmoja alipowakimbilia na kuwauliza ikiwa walikuwa wakizungumza na watu kuhusu Neno la Mungu. Kisha mwanamume huyo akasema: “Mimi huvuta sigara na pia ninatumia kileo kupita kiasi. Ninajua kwamba hivi karibuni nitasimama mbele za Mungu ili kuhukumiwa. Singependa wakati huo ufike nikiwa katika hali hii.” Mipango imefanywa ili mwanamume huyo ajifunze Biblia na ndugu wanaoishi katika eneo hilo.

Vasyl kutoka kutaniko la Lviv-Riasne-Skhidnyi alipokuwa akihubiri pamoja na kikundi chake cha utumishi katika kijiji kimoja aliona nyumba fulani na akaikumbuka. Alikuwa amemhubiria mama mwenye nyumba hiyo miaka mingi iliyopita. Alikumbuka kwamba mwanamke huyo alizungumza naye kwa ukali na hakutaka kuwaona Mashahidi wa Yehova. Vasyl aliamua kubisha mlango huo tena na kumweleza atakayefungua kuhusu mpango wetu wa kujifunza Biblia. Alishangaa mwanamke yuleyule alipofungua mlango na kusema kwamba alitaka kuelewa Maandiko Matakatifu. Alikubali kujifunza Biblia na mipango ikafanywa ili kufuatilia upendezi huo.

Serhii aliye katika kutaniko la Illintsi alibatizwa mwaka 2021 na hakuwa ameshiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Alikuwa na wasiwasi hivyo alitumia muda mwingi ili kujitayarisha vizuri. Serhii alisema hivi: “Nilitazama mara nyingi video za mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo. Baada ya kufanya hivyo, kitu nilichohitaji ni kuwa jasiri tu.” Mwishowe, alisema kwamba wasiwasi wake ulibadilika na kuwa shangwe kubwa kwa sababu alipata fursa ya kuwaeleza wengine habari njema.

Nikol kutoka kutaniko la Rozdil aliwekwa rasmi kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa Agosti 2022. Anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi mwingi na niliogopa kushiriki kazi ya kuhubiri uso kwa uso. Lakini baada ya kufanya hivyo, nilijionea jinsi inavyoburudisha kuwa na mazungumzo ya uso kwa uso kumhusu Yehova!”

Dada wawili wakishiriki katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba

Kufikia Novemba 11, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 46 wamekufa

  • Wahubiri 97 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 12,569 wamelazimika kuacha makao yao

  • Nyumba 590 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 645 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 1,722 zimepata uharibifu mdogo

  • Majumba 6 ya Ufalme yameharibiwa kabisa

  • Majumba 19 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 63 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 27 za kutoa msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Watu 53,948 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 25,983 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu