Hamia kwenye habari

Kushoto: Ndugu na dada nchini Ukrainia wakipakia maboksi ya msaada kutoka Poland ndani ya gari litakaloenda kuisambaza. Kulia: Nyumba ya ndugu iliyoharibiwa na kombora huko Hostomel

APRILI 13, 2022
UKRAINIA

RIPOTI YA 6 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

RIPOTI YA 6 | Upendo wa Kindugu Unaendelea Kuonyeshwa Licha ya Mashambulizi Nchini Ukrainia

Kwa kusikitisha, wengi zaidi kati ya ndugu na dada zetu wamekufa kutokana na vita vinavyoendelea nchini Ukrainia. Jumla ya Mashahidi 28 wa Yehova wamekufa.

Kama ilivyoripotiwa katika habari za kimataifa, miji iliyo karibu na Kyiv ilikumbwa na vita vikali katika majuma ya kwanza ya vita hivyo. Kati ya wahubiri 4,900 ambao waliishi katika eneo hilo, zaidi ya 3,500 wamekimbilia maeneo salama zaidi.

Masimulizi yafuatayo yanaonyesha jinsi ambavyo ndugu zetu katika maeneo hayo wanadumisha imani isiyotikisika licha ya majaribu makali.

Oleksandr, mzee katika mji wa Makariv, alikimbilia eneo salama katikati ya Ukrainia. Hata hivyo, kwa sababu ya kuwajali wahubiri wanne katika kikundi chake cha utumishi ambao hakuweza kuwasiliana nao, alirudi katika eneo la vita ili kuwatafuta. Anasema hivi: “Ninajua kwamba watumishi wa Yehova ni muhimu sana kwake. . . . Nilipofika kwenye nyumba ya mhubiri mmoja niliona kwamba ilikuwa imepigwa na kombora. Mlango wa chumba cha chini ya ardhi ulikuwa umefungwa na hakuna mtu aliyejibu nilipoita. Hilo lilinipa wasiwasi mwingi.” Oleksandr alivunja mlango huo na akaona kikundi cha watu wakimtazama. Ndani kulikuwa na wahubiri aliokuwa akiwatafuta, pamoja na jirani zao ambao si Mashahidi waliokuwa wamekaribishwa na wahubiri hao ili kujificha.

Yaroslav na mke wake (katikati) na Oleksandr na mke wake wakila mlo baada ya kufika eneo salama

Mhubiri mmoja katika chumba hicho, Yaroslav, alieleza kwamba walikuwa wamejificha humo kwa siku nane. Alisema hivi: “Kila mtu alikula biskuti chache na glasi moja tu ya maji kwa siku. Lakini tulisoma Biblia na machapisho yetu, tukasali, na kutiana moyo. Nilipomsikia Oleksandr akiita jina langu, nilifikiri wanajeshi walikuwa wamekuja kunikamata. Nilifikiri ningekufa. . . . [Badala yake,] alituokoa sisi sote. Tunamshukuru Yehova sana kwa familia ya kiroho yenye upendo mwingi, watu ambao wanasali kwa ajili yetu na hata kuhatarisha uhai wao ili kutuokoa.”

Pylyp

Pylyp na ndugu mwingine waliamua kuwapelekea chakula wale waliobaki katika mji wa Borodianka. Machi 17, walipokuwa wakiendesha gari mjini, wanajeshi walilikamata gari la Pylyp na kuchukua chakula walichokuwa nao. Wanajeshi hao waliwakamata ndugu wote wawili, wakawafunga pingu, na kuwafumba macho, kisha wakawapeleka kwenye chumba kidogo cha chini ya ardhi ambamo kulikuwa na wanaume wengine saba. Siku mbili baadaye, waliwahamishia kwenye jela ambapo walinzi waliwashambulia usiku. Pylyp anasema hivi: “Sikuwa na uhakika ikiwa ningeokoka. Nilisali kwamba niendelee kuwa mshikamanifu.”

Pindi moja Pylyp alipokuwa akipigwa, alianza kusali kwa sauti kwa ajili ya akina dada wenye umri mkubwa ambao hawakuwa na chakula, na pia kwa ajili ya usalama wa familia yake, kisha akamshukuru Yehova kwa miaka mingi aliyokuwa amemtumikia kwa furaha. Mlinzi alimrudisha kwenye jela yake, ambako aliendelea kusali kwa ajili ya wanajeshi hao na kuomba waelewe kuwa ndugu hao si hatari. Kisha ndugu wote wawili wakaanza kuwahubiria walinzi hao. Kwa siku mbili, waliwahubiria walinzi wa zamu zote. Isitoshe, mmoja kati ya wanaume waliofungwa alionyesha upendezi katika ujumbe wa Biblia. Aliwashukuru akina ndugu hao. Machi 27, ndugu hao pamoja na mwanamume aliyeonyesha upendezi waliachiliwa.

Svitlana, dada mseja katika eneo la Bucha, asingeweza kuondoka katika eneo la vita kwa majuma mawili. Alisimulia hivi: “Zaidi ya wakati mwingine, ninaelewa umuhimu wa amani ambayo Yehova anatupa. Kuwa na amani ya Mungu hakumaanishi sikuzote tutajua jambo la kufanya. Lakini wakati ambapo hatuoni suluhisho la matatizo yetu, tunamtegemea Yehova kikamili.”

Svitlana alipokuwa akisafiri kuelekea eneo salama zaidi nchini Ukrainia, alimhubiria mwanamke fulani pamoja na mpwa wake. Wote walifika salama katika eneo hilo na wakakaribishwa na familia ya Mashahidi. Familia hiyo ya Mashahidi ilimkaribisha Svitlana pamoja na mwanamke huyo na mpwa wake walale nyumbani kwao usiku huo. Siku iliyofuata, mwanamke huyo aliomba kuhudhuria mkutano wa kutaniko na akaomba Biblia na machapisho yetu. Svitlana anaendelea kuwasiliana naye.

Kufikia Aprili 12, 2022, hizi ndizo takwimu zilizotufikia kutoka Ukrainia. Takwimu hizo zinategemea ripoti za uhakika tulizopata kutoka kwa ndugu walio katika maeneo hayo. Hata hivyo, huenda idadi halisi ikawa kubwa zaidi kwa sababu ni vigumu kudumisha mawasiliano mazuri katika maeneo yote nchini.

Athari Ambazo Ndugu na Dada Zetu Wamepata

  • Wahubiri 28 wamekufa

  • Wahubiri 48 wamejeruhiwa

  • Wahubiri 40,778 wameacha makao yao na kwenda sehemu zilizo salama zaidi nchini.

  • Nyumba 278 zimeharibiwa kabisa

  • Nyumba 268 zimepata uharibifu mkubwa

  • Nyumba 746 zimepata uharibifu mdogo

  • Jumba 1 la Ufalme limeharibiwa kabisa

  • Majumba 9 ya Ufalme yamepata uharibifu mkubwa

  • Majumba 26 ya Ufalme yamepata uharibifu mdogo

Jitihada za Kutoa Msaada

  • Halmashauri 27 za kutoa msaada zinashughulikia hali nchini Ukrainia

  • Wahubiri 41,974 wamesaidiwa moja kwa moja na halmashauri hizo kupata makao salama zaidi

  • Wahubiri 18,097 wamekimbilia nchi nyingine na wanasaidiwa na waamini wenzetu