Hamia kwenye habari

JUNI 23, 2022
UKRAINIA

Safari Yangu ya Kutafuta Usalama

Anastasia Khozyainova Asimulia Jinsi Alivyokimbia Kutoka Ukrainia

Safari Yangu ya Kutafuta Usalama

Asubuhi ya Februari 24, 2022, kelele nyingi ziliniamsha. Mwanzoni nilifikiri kwamba itakuwa ni ngurumo za radi kwa sababu kulikuwa kunanyesha, lakini haikuwa hivyo. Nilikuwa nimesikia mabomu yakilipuka.

Nilitambua kwamba nilipaswa kuondoka na kuacha nyumba yangu iliyokuwa katikati ya jiji la Mariupol. Siku iliyofuata, nilienda kwa nyanya yangu, Iryna, anayeishi nje ya jiji. Baada ya muda fulani, mama yangu pia alikuja basi tukawa wanne, yaani, mimi, mama, nyanya, na binamu yangu. Tulipata usalama katika nyumba ya nyanya kwa muda fulani ingawa tulilazimika kulala katika chumba cha chini ya ardhi kwa siku kadhaa.

Siku moja, kombora lilianguka kwenye bustani yetu ya mboga. Tulikuwa tumejificha katika chumba cha chini tuliposikia kishindo hicho kikubwa. Nilisali kwa bidii. Baada ya juma moja, tuligundua kwamba hatutakuwa salama tukiendelea kuishi katika nyumba ya nyanya yangu, kwa hiyo tuliamua kurudi jijini ili kutafuta namna ya kukimbia. Nilimsihi Yehova atulinde na kutusaidia kukimbia jiji hilo.

Machi 4, asubuhi, tulikosa treni zinazoenda nje ya jiji la Mariupol kwa sababu jiji hilo lilikuwa limezingirwa. Kwa hiyo, tulijificha katika jumba la sinema pamoja na mamia ya watu kwa siku kumi zilizofuata. Kulikuwa na watu wengi sana hivi kwamba tulilazimika kulala sakafuni. Mazingira hayakuwa mazuri, na ilikuwa vigumu kupata chakula na maji moto. Tulilazimika kusubiri kwa saa nyingi kwenye foleni.

Siku moja, kombora lililipuka karibu tu na jumba hilo la sinema. Mlipuko huo ulikuwa na kishindo kikubwa hivi kwamba madirisha mengi ya jumba hilo yalipasuka na kukawa na baridi kali sana.

Anastasia akiwa na nyanya yake, Iryna pamoja na binamu yake, Andrii

Ni nini kilichonisaidia kuvumilia katika kipindi hicho kigumu? Nilitafakari simulizi la Ayubu. Nilipoona watu wakichanganyikiwa baada ya kusikia mlipuko, ningefungua Biblia yangu na kusoma simulizi la Ayubu. Nilihisi vizuri baada ya kufanya hivyo. Nilihisi kana kwamba Ayubu alikuwa pamoja nami katika jumba hilo, na nilikuwa nikimwambia: “Sasa ninaelewa jinsi ulivyohisi!” Ayubu alipoteza kila kitu: familia yake, hali yake nzuri ya kiafya, na mali zake. Mimi nilipoteza vitu vya kimwili tu. Nilikuwa pamoja na familia yangu, nasi sote tulikuwa hai na tulikuwa na afya njema. Nilipofikiria hayo, nilitambua kwamba hali yangu haikuwa mbaya kama ya Ayubu. Nami nilihisi vizuri.

Machi 14, tulisikia kwamba kikundi cha watu kilikuwa kimefanikiwa kukimbia jiji. Kwa hiyo, sisi pia tuliamua kukimbia. Tulifanikiwa kupata usafiri pamoja na baadhi ya watu waliokuwa katika jumba lile la sinema.

Msafara wa magari 20 uliondoka kwenye jiji. Tulibanana watu kumi na nne ndani ya gari dogo la mizigo. Mabomu yalikuwa yakianguka kutuzunguka tulipokuwa tukisafiri. Nilisali bila kuacha. Tulipofanikiwa tu kutoka nje ya jiji la Mariupol, dereva wetu alishuka nje ya gari na kulia machozi. Alikuwa ameepuka mabomu yote yaliyotegwa barabarani. Tulisikia kwamba siku mbili baada ya sisi kuondoka lile jumba la sinema lilipuliwa kwa bomu na watu 300 hivi walikufa.

Baada ya saa 13, tulifika Zaporizhia. Na siku iliyofuata asubuhi, tulipanda treni na kusafiri hadi Lviv. Kulikuwa na watu 16 katika kila behewa ambalo kwa kawaida hukaliwa na watu wanne. Kulikuwa na joto sana. Nilisimama kwenye korido karibu safari nzima ili angalau nipate hewa safi. Machi 16, tulifika jijini Lviv, ambako tulipokewa kwa uchangamfu na ndugu na dada zetu. Tulilala katika Jumba la Ufalme kwa siku nne. Niliguswa moyo na jinsi ndugu na dada walivyotutunza hivi kwamba nililia machozi. Hilo lilikuwa zawadi kutoka kwa Yehova.

Machi 19, mama, nyanya, binamu yangu pamoja na mimi tuliamua kuhama Ukrainia na kwenda Poland. Tulifurahi sana kwa sababu Mashahidi wenzetu walitupokea. Walituandalia kila kitu tulichohitaji. Tulionyeshwa upendo kila mahali.

Nina umri wa miaka 19 tu, lakini baada ya kupitia majaribu yote haya, nimejifunza umuhimu wa kujenga imani yetu mambo yakiwa bado shwari. Imani humsaidia mtu kuyashinda majaribu. Ikiwa singefanya funzo langu la kibinafsi kabla ya vita kutokea, hali ingekuwa ngumu zaidi.

Yehova ni Baba anayetujali. Katika kipindi chote hicho, nilihisi kana kwamba aliushika mkono wangu wa kulia na kuniongoza hadi nilipo sasa. Ninahisi siwezi kumshukuru Yehova kikamili kwa mambo yote aliyonifanyia.​—Isaya 41:10.