Hamia kwenye habari

Liudmyla Mozul na Kateryna Rozdorska waliwapoteza waume zao katika vita vinavyoendelea nchini Ukrainia. Utegemezo kutoka kwa Yehova na kwa undugu wetu unawasaidia kuendelea kuvumilia

APRILI 22, 2022
UKRAINIA

“Usiku Huo, Yehova Alifanya Zaidi ya Kuushika Mkono Wangu, Alinibeba Mikononi Mwake”

Dada Wawili Nchini Ukrainia Wanaimarishwa na Ahadi za Yehova Baada ya Kufiwa na Waume Zao

“Usiku Huo, Yehova Alifanya Zaidi ya Kuushika Mkono Wangu, Alinibeba Mikononi Mwake”

Kwa msaada wa Yehova, Dada Liudmyla Mozul na Dada Kateryna Rozdorska wanavumilia maumivu na huzuni kwa sababu ya vita vinavyoendelea. Waume zao, Petro Mozul na Dmytro Rozdorskyi, walikuwa kati ya Mashahidi wa kwanza wa Yehova kufa kutokana na vita vinavyoendelea. Kwa kuhuzunisha, kufikia sasa ndugu na dada zetu 34 wamekufa kutokana na vita hivyo.

Petro na Liudmyla Mozul

Petro na Liudmyla walibatizwa mwaka wa 1994. Wenzi hao walifunga ndoa miaka 43 iliyopita.

Liudmyla anasema hivi: “Waabudu wenzangu wananitumia maneno yenye kufariji kila siku, hawachoki kunipigia simu. Pia nilitokwa na machozi nilipopata barua yenye kufariji kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Ukrainia.”

Vita hivyo vilianza Februari 24, 2022. Petro, aliyetumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko la lugha ya ishara, aliuawa Machi 1, 2022 wakati ambapo yeye na familia yake walikuwa wakijaribu kukimbia mashambulizi makali ya makombora yaliyotokea kule Kharkiv.

Baada ya siku kadhaa za mashambulizi ya mabomu, ndege za kivita zilipita juu yao na kuanza kulishambulia jiji. Familia yao ilikusanya vitu vya lazima na kuondoka ndani ya dakika 30. Petro na Liudmyla walikuwa ndani ya gari moja. Mwana wao, Oleksii, na mke wake, Maryna, walikuwa ndani ya gari lingine. Liudmyla anasema: “Tulikuwa tukiendesha gari katika eneo la makazi wakati ambapo ndege hizo zilianza kuangusha makombora kutuzunguka. Gari letu lilitikiswa vibaya kwa sababu ya milipuko hiyo.”

Petro aliyekuwa na umri wa miaka 67, alijaribu kukwepa gari la Oleksii, lakini alipatwa na majeraha mengi. Yeye na Liudmyla walipelekwa hospitali ambako baadaye Petro alikufa. Liudmyla alipata majeraha kwenye mguu na tumbo yaliyosababishwa na vipande vya chuma vilivyotokana na mabomu. Oleksii na Maryna hawakupata majeraha yoyote. Liudmyla alijulishwa kuhusu kifo cha mume wake siku tatu baadaye aliporuhusiwa kuondoka hospitali.

Liudmyla anasema: “Kadiri ninavyofikiria fadhili za Yehova na kusudi lake, ndivyo ninavyopata amani ya moyoni. Nina hakika nitamwona mume wangu tena katika ulimwengu mpya, ninatazamia kwa hamu sana jambo hilo.”

Kateryna na Dmytro Rozdorksyi

Dmytro na Kateryna walifunga ndoa miaka minane iliyopita. Maneno ya mwisho ambayo Dmytro alimwambia mke wake alipompigia simu kutoka kazini yalikuwa, “Nitarudi nyumbani hivi karibuni.”

Saa chache baadaye, mfanyakazi mwenzake alimpigia simu Kateryna na kumjulisha kwamba mume wake amekanyaga kombora lililotegwa ardhini na alikuwa amekimbizwa hospitalini. Alikufa saa tano baada ya kufanyiwa upasuaji.

Kateryna anasema hivi baada ya kupata taarifa za kifo cha Dmytro: “Usiku huo, Yehova alifanya zaidi ya kuushika mkono wangu, alinibeba mikononi mwake. Nilihisi kwamba Yehova yuko karibu sana nami.”

Dmytro aliyekuwa na umri wa miaka 28, alibatizwa mwaka wa 2006 na alitumikia akiwa mzee katika Eneo la Donetsk nchini Ukrainia.

Muda mfupi baada ya mazishi ya Dmytro, Kateryna alisafiri kwa muda wa saa 12 kwenda katika eneo salama zaidi nchini Ukrainia. “Nimetiwa moyo na akina ndugu na dada kutoka maeneo yote Ukrainia na hata kutoka nje ya nchi. Wamenionyesha upendo mwingi wa kutoka moyoni ambao umepunguza maumivu yangu.”

Anaendelea kusema: “Ninapata faraja pia kwa kushiriki katika huduma. . . . Ninapoanza kuwa na huzuni na kushindwa kujizuia, mimi husema kwa sauti mistari ya Biblia kama vile Wafilipi 4:6, 7.”

Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwa chanzo cha nguvu na faraja kwa ndugu na dada zetu wapendwa ambao wamewapoteza wapendwa wao katika vita vinavyoendelea nchini Ukrainia.​—Zaburi 61:1-3.