Hamia kwenye habari

FEBRUARI 13, 2015
UKRAINIA

Majengo ya Ibada Yatekwa Katika Maeneo ya Mashariki ya Ukrainia

Majengo ya Ibada Yatekwa Katika Maeneo ya Mashariki ya Ukrainia

Vikosi vyenye silaha vimechukua kinguvu Majumba kadhaa ya Ufalme (nyumba za ibada) ya Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia. Majengo hayo yako katika maeneo ya Donetsk na Luhansk kwenye eneo la mashariki la Ukrainia, ambapo vita vimekuwa vikiendelea kwa miezi mingi. Watu hawa wenye silaha wanawashambulia Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya ubaguzi na wanapuuza haki ya Mashahidi wa Yehova ya uhuru wa kidini na ya kushirikiana.

Kwa zaidi ya miaka 20, Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia wamefurahia uhuru wa kuabudu. Vasyl Kobel, Shahidi wa Yehova aliye kwenye ofisi ya tawi iliyoko jijini Lviv, alieleza hivi: “Tumekuwa tukikusanyika pamoja kwa ukawaida katika nyumba zetu za ibada tukisoma Biblia na kusali, na kujitahidi kuwa vielelezo vizuri katika jamii zetu. Lakini katika miezi ya karibuni, maisha ya Waukrainia yameathiriwa na machafuko yaliyoko mashariki mwa nchi. Hii ni kutia ndani Mashahidi wa Yehova; ambao pia wanakabili vitendo vya ujeuri.”

Bw. Kobel alizungumza kwa niaba ya Mashahidi 150,000 wa Yehova wanaoishi nchini Ukrainia. Miezi ya karibuni maelfu ya Mashahidi wamekimbia eneo hilo lenye vita. Hata hivyo, karibu Mashahidi 17,500 waliobaki katika maeneo ya Donetsk na Luhansk wanajitahidi kuendelea na shughuli za kila siku huku vita vikiendelea. Kwa sababu wamenyang’anywa Majumba yao ya Ufalme, maelfu ya Mashahidi hawana mahali pa kukusanyika kwa ajili ya ibada, na wanalazimika kukutana kwenye nyumba ndogo za watu binafsi. Kwa sasa Mashahidi wengine wanalazimika kusafiri kwa muda wa saa mbili hivi ili kuhudhuria ibada.

Kutekwa kwa Majumba ya Ufalme Ni Tendo la Chuki ya Kidini

Kunyang’anywa Majumba yao ya Ufalme si vitendo vya uhalifu wa kawaida tu dhidi ya Mashahidi, ni vitendo vya ubaguzi dhidi yao na imani yao ya kidini. Kamanda wa kikosi kimoja alieleza wazi nia yake ya “kuwaondolea mbali Mashahidi wa Yehova” kwa sababu anaamini kuwa Kanisa Othodoksi ndiyo dini pekee inayokubalika katika eneo hilo. Kamanda mwingine alisema hivi: “Huu ndio mwisho wa Mashahidi wa Yehova.” Licha ya vitisho hivyo, Mashahidi wa Yehova wameazimia kabisa kuendelea na utendaji wao kotekote nchini Ukrainia.

Ingawa hakuna Shahidi yeyote aliyejeruhiwa katika visa hivyo vya utekaji wa majengo, usalama na uhuru wao wa kushirikiana pamoja na waamini wenzao unahatarishwa. Katika kisa kimoja, wanaume wenye silaha walivamia Jumba la Ufalme kwenye mji wa Horlivka katika eneo la Donetsk wakati wa mikutano, na kuwatia hofu wahudhuriaji, waliotia ndani watoto na pia wazee. Katika kisa kingine, Mashahidi walishtuka walipofika katika Jumba la Ufalme kwa ajili ya ibada na kupata vitasa vimebadilishwa na jengo likitumiwa kama kambi ya wanajeshi.

Kinachofanywa Ili Kusuluhisha Tatizo Hilo

Bw. Kobel alisema hivi: “Ofisi ya tawi jijini Lviv imejulisha wizara mbalimbali za serikali na wenye mamlaka wengine kuhusu vitendo hivyo vya utekaji wa majengo. Hilo linaitahadharisha serikali kwamba kitakachotendeka katika majengo hayo na wavamizi hao haramu si daraka letu.” Zaidi ya hayo, ofisi ya tawi imewaagiza wanaume wenye mamlaka katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika maeneo ya Donetsk na Luhansk kufanya yote wawezayo kuhakikisha usalama wa kila Shahidi. Wanaume hao wamekumbushwa kuwa uhai ni wenye thamani zaidi kuliko majengo na kwamba wasichukue hatua yoyote itakayohatarisha usalama wa Shahidi yeyote.

Kwa sababu ya machafuko yanayoendelea, kwa sasa hakuna hatua yoyote ya kisheria ambayo Mashahidi wanaweza kuchukua ili kurudishiwa Majumba yao ya Ufalme. Hata hivyo, licha ya magumu ya kutokuwa na mahali pa kukutania, Mashahidi wameazimia kuendelea na utendaji wao wa kidini. Wanatazamia wakati ambapo watarudishiwa majengo yao na wakusanyike tena na waamini wenzao kwa usalama na starehe katika Majumba yao ya Ufalme.