Hamia kwenye habari

Mateso dhidi ya ndugu zetu yanazidi kuongezeka katika baadhi ya maeneo ya Donetsk na Luhansk, yaliyoko mashariki mwa Ukrainia. Mei 30, 2018, mali katika Jumba la Ufalme kwenye eneo la Luhansk ziliibiwa, jumba likaharibiwa, kisha likachomwa.

OKTOBA 15, 2018
UKRAINIA

“Jamhuri ya Donetsk” Yapiga Marufuku Mashahidi wa Yehova

“Jamhuri ya Donetsk” Yapiga Marufuku Mashahidi wa Yehova

Septemba 26, 2018, Mahakama Kuu ya “Jamhuri ya Donetsk” (DPR) ilitangaza kwamba shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova ni lenye “msimamo mkali,” na hivyo likapiga marufuku utendaji wetu. Mwendesha-mashtaka mkuu, ambaye aliwasilisha mashtaka dhidi ya shirika letu la kisheria, hakumhoji Shahidi yeyote wa Yehova, wala Mahakama haikumruhusu Shahidi yeyote wa Yehova azungumze wakati wa kesi hiyo. Tendo hilo la kupiga marufuku utendaji wetu ndilo tukio la karibuni zaidi katika mfuatano wa matukio ya ukandamizaji wa kidini dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo.

Hali ya ndugu zetu katika baadhi ya maeneo ya Donetsk na Luhansk, mashariki mwa Ukrainia, imezorota sana tangu katikati ya mwaka wa 2017 wakati ambapo Mahakama Kuu ya DPR ilitangaza kwamba baadhi ya machapisho yetu ni yenye “msimamo mkali.” Katika mwaka huo, polisi waliwahoji zaidi ya Mashahidi 170. Wenye mamlaka katika maeneo hayo wamenyakua Majumba ya Ufalme kwa mpangilio hususa, moja baada ya lingine. Kufikia Agosti 29, 2018, jumla ya Majumba 16 ya Ufalme yamenyakuliwa.

Licha ya mashambulizi hayo dhidi ya ibada yao, akina ndugu na dada katika maeneo hayo wanaendelea kumtegemea “Mungu wa wokovu.”—Zaburi 18:46.