Hamia kwenye habari

Jumba la Ufalme kwenye mji wa Brianka, eneo la Luhansk, lilitekwa Machi 26, 2015

DESEMBA 13, 2016
UKRAINIA

Kuzuiwa kwa Ibada Kwaendelea Kwenye Maeneo ya Mashariki Mwa Ukrainia

Kuzuiwa kwa Ibada Kwaendelea Kwenye Maeneo ya Mashariki Mwa Ukrainia

Watu wanaoishi kwenye maeneo ya mashariki mwa Ukrainia wanakabili kila siku hali ambazo zinavuruga maisha yao na kuwaletea wasiwasi na hofu. Pia, mapigano yanayoendelea huko yanawaongezea mahangaiko Mashahidi wa Yehova. Mbali na kuenea kwa ukosefu wa usalama pia kuna uwezekano wa kuenea kwa ubaguzi wa kidini. Vikosi vya wanaume wenye silaha vimeteka na kumiliki baadhi ya Majumba ya Ufalme ya Mashahidi (majengo ya ibada). Wamewaambia Mashahidi kwamba dini ya Othodoksi pekee ndiyo iliyokubaliwa na kwamba wanakusudia “kuwaondoa Mashahidi wa Yehova” kutoka katika maeneo ya mashariki mwa Ukrainia.

Kutekwa kwa Majumba ya Ufalme

Kati ya Juni 2014 na Novemba 2016, vikundi vya wanaume wenye silaha waliteka kwa nguvu Majumba ya Ufalme 18 ili kuyatumia ama kama kambi au kwa matumizi mengine yanayotegemeza shughuli zao. Ingawa mali nyingi zilitekwa wakati mapigano yalipopamba moto mwaka 2014, lakini pia, katika kipindi cha hivi karibuni Majumba ya Ufalme yameendelea kutekwa.

Jumba la Ufalme lililopekuliwa lililopo kwenye Mtaa wa 9 Simferopolska, Horlivka

Asubuhi ya Julai 22, 2016, Mashahidi wa Yehova jijini Horlivka walikuwa wamekusanyika ili kufanya ibada katika Jumba la Ufalme lililopo kwenye Mtaa wa 105-A Vitchyzniana wakati wanaume wenye silaha walipoingia ndani na kuamuru kila mtu aondoke mara moja. Wanaume hao walipekua-pekua jengo hilo na kuondoa samani na vifaa vyote. Jumba hilo liliwahi kutekwa Novemba 29, 2014, lakini baada ya muda lilitelekezwa. Mashahidi walilitumia tena kwa ajili ya mikutano yao ya kidini mpaka lilipotekwa kwa mara nyingine Julai 22.

Siku tatu baadaye, wanaume wenye silaha waliingia kwenye Jumba lingine la Ufalme jijini Horlivka, lililopo Mtaa wa 9 Simferopolska. Wanaume hao walichukua kila kitu kutoka katika jengo hilo, hata rejeta na wakaondoa uzio wa nje. Makutaniko yaliyokuwa yakifanya ibada katika jengo hilo yamefanya mipango mingine kwa ajili kufanya ibada.

Kuendelea Kukutana Pamoja Kwa Ajili ya Ibada

Baadhi ya makutaniko ambayo Majumba yao ya Ufalme yametekwa wanakutana wakiwa vikundi vidogo kwa ajili ya ibada ili kuepuka kukaziwa uangalifu na vikosi vyenye silaha. Mashahidi wengine wanasafiri kwenda kwenye Majumba mengine ya Ufalme yaliyo nje ya eneo la mapigano kwa ajili ya mikutano yao ya kidini, wakikabili changamoto ya usafiri na kupanda kwa gharama ya usafiri. Wale ambao hushindwa kusafiri kwa sababu ya matatizo ya umri mkubwa na matatizo ya afya wanasikiliza mikutano kwa njia ya simu.

Inakuwa vigumu zaidi kukusanyika pamoja kwa sababu ya hali ya migogoro na hali nyingine ngumu zilizopo. Illia Kobel, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia, anasema hivi: “Kama majirani wao, Mashahidi wanaoishi kwenye maeneo yaliyo karibu na mapigano wamechoshwa kihisia kwa sababu ya kusikia kila mara milio ya risasi na milipuko. Wanakabili hali ngumu za kiuchumi zinazosababishwa na kupanda kwa bei za vitu na kupungua kwa mapato. Licha ya changamoto hizo, Mashahidi wanaendelea kukusanyika kwa ajili ya ibada pamoja na waabudu wenzao.”

Mashahidi Warudi Kwenye Baadhi ya Majumba ya Ufalme

Mashahidi wa Yehova wanafurahi kwamba sasa wanaweza kutumia tena kwa ajili ya ibada majengo sita ambayo yalitekwa. Ingawa majengo hayo yaliharibiwa, Mashahidi wa eneo hilo walifanya kazi ya kurekebisha na kufanya Majumba hayo yafae kwa ajili ya mikutano ya kidini. Jengo la saba bado halitumiwi kwa ajili ya mikutano ya dini kwa sababu limeharibiwa sana.

Kutaniko lililolazimishwa kuacha kutumia Jumba la Ufalme katika eneo la Luhansk mnamo Septemba 2014, liliweza kulitumia tena kwa ajili ya ibada baada ya mwaka mmoja. Mzee katika kutaniko hilo, Anatoliy Danko, anaonyesha hisia ambazo wengi walikuwa nazo, aliposema hivi: “Katika pindi kama hizi, tunashukuru kwamba kutaniko letu ndilo familia yetu. Baada ya kutengana kwa muda mrefu, sasa tumerudi nyumbani kwetu.”

Kutounga Mkono Upande Wowote Licha ya Mapigano

Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa—hawaungi mkono upande wowote unaopigana. Mashahidi wanaoishi eneo la mashariki mwa Ukrainia wana msimamo huo pia. Wanatarajia kwa hamu wakati ambapo wataweza kuishi kwa amani na familia na majirani wao na kufanya shughuli za dini yao bila kuzuiwa.