Hamia kwenye habari

Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia sasa wanaweza kukusanyika kwenye majengo ya kukodi bila kuingiliwa

MACHI 24, 2017
UKRAINIA

Mahakama Kuu ya Ukrainia Yaimarisha Uhuru wa Kukusanyika kwa Amani

Mahakama Kuu ya Ukrainia Yaimarisha Uhuru wa Kukusanyika kwa Amani

Septemba 8, 2016, Mahakama ya Katiba ya Ukrainia iliunga mkono haki ya kukusanyika kwa amani bila kuingiliwa na maofisa wa serikali. Mahakama ilibatilisha sehemu ya sheria ya Ukrainia ya mwaka wa 1991 iliyohusu Uhuru wa Dhamiri na Mashirika ya Kidini (Sheria ya Dini), ambayo ilisema kwamba taasisi za kidini zinapaswa kupata “kibali” cha Serikali ili kuendesha mikutano ya kidini kwenye majengo ya kukodi. Mahakama ya Katiba ilieleza kwamba sheria hiyo inapingana na katiba ya nchi ambayo inatoa uhuru wa kukusanyika kwa amani. Uamuzi huo umepokelewa kwa furaha na Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia, ambao wamekabili hali ngumu sana walipokodi majengo ili kufanya ibada.

Maofisa Wakataa Kutoa Kibali cha Kufanya Ibada

Tangu Sheria ya Dini ianze kufanya kazi, maofisa wenye chuki wametumia sheria hiyo kwa manufaa yao ili kujitetea wanapofuta mikataba ya Mashahidi ya kutumia majengo ya kukodi kwa ajili ya ibada. Katika tukio moja lililotukia katika majira ya kiangazi ya mwaka wa 2012 ambapo maelfu ya Mashahidi wa Yehova katika eneo la kaskazini-mashariki mwa Ukrainia walipanga kufanya kusanyiko la kidini la siku tatu katika jiji la Sumy. Mkataba wa kukodi uwanja wa manispaa ulikuwa umetiwa sahihi, na mipango ya kufanya mkutano huo ilikuwa ikiendelea vizuri. Mashahidi waliwapa taarifa wenye mamlaka kuhusu mipango ya kusanyiko kama katiba inavyosema. Kisha, mwezi mmoja tu kabla ya kusanyiko hilo, Halmashauri ya Jiji la Sumy kwa kutegemea Sheria ya Dini ilieleza kwamba taarifa tu haitoshi. Kulingana na maoni ya halmashauri hiyo, Mashahidi walihitaji kupata kibali cha kutumia uwanja huo. Halmashauri hiyo ilikataa kutoa kibali hicho.

Wakiwa na muda mfupi sana, Mashahidi wa Yehova walilazimika kufanya mipango kuwa na kusanyiko hilo jijini Kharkiv, lililoko kilomita 200 kutoka jiji la Sumy. Kubadilishwa kwa eneo la kufanyia kusanyiko kuliwalazimisha Mashahidi zaidi ya 3,500 warekebishe mipango yao haraka sana. Wengi walishindwa kusafiri mpaka Kharkiv ili kuhudhuria tukio hilo muhimu kwa sababu ya umri au afya. Wengine walishindwa kuhudhuria kwa sababu hawakuweza kupata ruhusa kazini au kwa sababu hawakuwa na pesa za kutosha kwa ajili ya safari hiyo ya kwenda Kharkiv. Mwaka uliofuata, kwa mara nyingine Halmashauri ya Jiji la Sumy ilitumia Sheria ya Dini kukataa kuwapa kibali Mashahidi ili wafanye kusanyiko kwenye uwanja huo.

Illia Kobel, kutoka kwenye ofisi ya Mashahidi wa Yehova nchini huko iliyoko jijini Lviv, alisema hivi: “Kuna matukio mengine mengi ya kufutwa kwa makusanyiko zaidi ya yale yaliyotukia jijini Sumy. Katika visa vingine kadhaa, imekuwa vigumu kukodi majengo kwa ajili ya kufanya ibada yetu.” Kwa mfano, mnamo Machi 2012, maofisa wa jiji la Vinnytsia walikataa kuwaruhusu Mashahidi kufanya ibada kwenye jumba la kukodi, na kuwalazimisha wafanye mipango mingine muda mfupi kabla ya kufanya mkutano huo. Miezi michache baadaye, maofisa walikataa kutoa kibali kwa kutaniko lililopo kwenye mji wa Mohyliv-Podilskyi ili wafanye ibada yao ya kila juma kwenye jengo la kukodi, ingawa tayari walikuwa wakilitumia jengo hilo kwa ajili ya ibada kwa miaka mitatu. Kwa kuwa hawana jengo lingine linalofaa, washiriki wa kutaniko hilo walilazimika kukusanyika pamoja wakiwa wamesongamana kwenye nyumba za watu binafsi.

Hivi karibuni mnamo Februari 2015, Mamlaka ya Mkoa wa Vinnytsia ilisisitiza kwamba Mashahidi wa Yehova wanakiuka sheria katika visa vingi. Serikali hiyo ya mkoa ilidai kwamba Mashahidi wamekuwa wakikiuka sheria kwa kukosa kutafuta kibali cha kufanya ibada kwenye majengo ambayo si majengo yao ya ibada. Haikutosha tu kutoa taarifa ili kupata ruhusa ya kufanya mikutano hiyo.

Mashahidi Watafuta Suluhisho la Kisheria

Katika miaka ya karibuni, kwa ujumla Mashahidi wa Yehova wameweza kukusanyika pamoja kwa uhuru katika majengo yao ya ibada bila kuingiliwa na serikali. Hata hivyo, wanahitaji kukodi majengo makubwa ambayo yana nafasi ya kutosha watu wengi kwa ajili ya mikutano ya pekee au makusanyiko ya eneo. Katiba ya Ukrainia inaruhusu taasisi za dini kukusanyika kwa amani kwenye majengo ya kukodi ikiwa maofisa wa serikali wanapewa taarifa mapema kuhusu mpango huo. Bw. Kobel alisema hivi: “Chanzo cha tatizo tulilokabili lilitokana na Sheria ya Dini, ambayo ilitofautiana na katiba. Katiba haisemi kwamba dini inapaswa kupata kibali cha kufanya mikutano ya dini kutoka kwa wenye mamlaka. Katika jitihada za kusuluhisha tatizo hili, tulipeleka maombi ya kushughulikia tatizo kwa Mkuu wa Bunge la Ukrainia wa Haki za Kibinadamu, ambaye pia anaitwa Mchunguzi wa Malalamiko ya Wananchi.”

Kazi ya Mchunguzi huyo ni kuhakikisha kwamba raia wote wa Ukrainia wanafurahia haki zinazotolewa na sheria na katiba ya nchi hiyo. Baada ya kuchunguza changamoto wanazokabili Mashahidi wa Yehova, Mchunguzi huyo alikubali kwamba katiba na Sheria ya Dini zilikuwa zikipingana. Katiba inatoa haki ya kukusanyika pamoja baada ya kutoa taarifa kwa maofisa wa serikali kwamba mkutano wa ibada wa hadharani utafanywa kwenye jengo la kukodi. Hata hivyo, Sheria ya Dini ilikataza kufanya mikutano ya kidini kwenye majengo ya kukodi bila kupata kibali kutoka kwa maofisa wa serikali siku kumi hivi kabla ya kufanya tukio hilo.

Oktoba 26, 2015, ofisi ya Mchunguzi wa Malalamiko ya Wananchi ilifungua kesi kwenye Mahakama ya Katiba ya Ukrainia ikitaka sehemu ya Sheria ya Dini itangazwe na mahakama kuwa inapingana na katiba. Hoja zilizohusiana na kesi ni kwamba kukusanyika pamoja kwa amani ni haki ya msingi inayotolewa kwa kila raia. Kwa kuongezea, alisema hivi: “Nchi haipaswi kufanya mambo yasiyo na msingi ambayo yanaingilia haki ya kukusanyika kwa amani.” Kwa kuunga mkono hoja za Mchunguzi huyo, Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia waliwasilisha ushahidi wao kwenye Mahakama ya Katiba na kueleza changamoto wanazokabili wanapokodi majengo kwa ajili ya ibada.

Mahakama ya Katiba Yabatilisha Sheria Inayochanganya

Katika uamuzi wake uliotolewa Septemba 8, 2016, Mahakama ya Katiba ilithibitisha kwamba hakuna sheria inayoweza kupinga haki ya kikatiba ya kukusanyika pamoja kwa amani baada ya kutoa taarifa kwa maofisa wa serikali. Zaidi ya kuchunguza sheria ya nchi, mahakama hiyo pia ilieleza kuhusu Kifungu cha 9 cha Mkataba wa Ulaya Kuhusu Haki za Kibinadamu, ambacho kinatoa haki ya uhuru wa ibada, na Kifungu cha 11, ambacho kinatoa haki ya uhuru wa kukusanyika pamoja bila kuingiliwa isivyo haki na Serikali. Mahakama iliitangaza Sheria ya Dini ya mwaka 1991, Kifungu cha 21, sehemu ya 5 kuwa haipatani na katiba. Kifungu hicho cha sheria kinasema kwamba lazima vikundi vya kidini vipate kibali kutoka kwa maofisa wa serikali kabla ya kuendesha ibada kwenye majengo ya kukodi.

Watiwa Moyo na Uamuzi

Kufanya ibada katika majengo ya kukodi hakutegemei tena uamuzi wa maofisa wa serikali ambao huenda wakaamua kutotoa kibali. Kama katiba inavyotoa haki, Mashahidi wanahitaji kutoa taarifa kwa maofisa kuhusu mipango ya kukodi jengo kwa ajili ya mkutano wa kidini, ombi hilo halitabatilishwa.

Bw. Kobel alizungumza kwa niaba ya Mashahidi wa Yehova zaidi ya 140,000 nchini Ukrainia, alisema hivi: “Uamuzi huu wa karibuni wa Mahakama ya Katiba umeimarisha haki ya kukusanyika kwa amani. Tunafurahi kwamba hatutasumbuliwa tena na maofisa tunapokodi majengo kwa ajili ya ibada.”