Hamia kwenye habari

JULAI 1, 2019
UKRAINIA

Mashahidi wa Yehova Wafanya Maonyesho ya Biblia Nchini Ukrainia

Mashahidi wa Yehova Wafanya Maonyesho ya Biblia Nchini Ukrainia

Mashahidi wa Yehova wanaoishi nchini Ukrainia wamekuwa na maonyesho ya pekee ya Biblia yanayokazia kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Lugha ya Ishara ya Kirusi (RSL), jambo ambalo ni hatua kubwa sana katika kazi yetu ya utafsiri. Maonyesho hayo yalianza Oktoba 7, 2018, jijini Lviv na yakaendelea mpaka Juni 7, 2019. Majiji mengine yaliyofanya maonyesho hayo pia ni Kharkiv, Kyiv, Odesa, na Dnipro.

Kabla ya kila tukio, makutaniko ya lugha ya ishara ya eneo husika yaligawa mialiko iliyochapishwa na kuwaonyesha video viziwi na watu wenye matatizo ya kusikia. Kwa kuongezea, Dawati la Habari za Umma la tawi ya Ukrainia liligawa mialiko kwa waelimishaji, vyombo vya habari, na wakuu wa serikali.

Wahudhuriaji wa maonyesho ya kwanza, katika Klabu ya Viziwi ya Jiji la Lviv, walionyeshwa programu mbalimbali za kielektroni ambazo viziwi wanaweza kutumia ili kujifunza Biblia kama vile JW Library Sign Language® app. Wageni walifurahia kuona maonyesho ya kihistoria kuhusu jinsi Biblia zilivyotokezwa katika karne zilizopita, kuanzia vitabu vya kukunjwa hadi vitabu vya kisasa. Jambo la kipekee katika maonyesho hayo lilikuwa toleo la mwaka wa 1927 la Biblia.

Tunafurahi kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Lugha ya Ishara ya Kirusi (RSL) sasa inapatikana. Tuna uhakika kwamba itawasaidia wale wanaotumia Lugha ya Ishara ya Kirusi (RSL) kupata ujuzi sahihi wa Maandiko.—Mathayo 5:3.