Hamia kwenye habari

JULAI 6, 2015
UKRAINIA

Mashahidi wa Yehova Warusha Matangazo ya Mkutano wa Pekee Katika Eneo la Vita Nchini Ukrainia

Mashahidi wa Yehova Warusha Matangazo ya Mkutano wa Pekee Katika Eneo la Vita Nchini Ukrainia

LVIV, Ukrainia—Mnamo Februari 14, 2015, Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia walifanya mkutano wa pekee, uliokusudiwa kuwapa msaada wa kiroho waabudu wenzao zaidi ya 17,000 wanaoishi katika eneo lenye vita la mashariki mwa Ukrainia. Programu hiyo ya saa mbili iliunganishwa kwa mfumo wa video kutoka katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova iliyo katika jiji la Lviv na matangazo hayo kurushwa mpaka mashariki mwa Ukrainia na maeneo mengine ya nchi hiyo. Mkutano huo ulifaa sana kwa kuwa mnamo Januari 24, 2015, katika jiji lenye bandari la Mariupol, roketi ya kivita ilishambulia na kuharibu nyumba 3 na ghorofa 58 za Mashahidi. Katika shambulizi hilo, Shahidi mmoja alijeruhiwa vibaya na mwingine aliyekuwa na umri wa miaka 16, aliuawa.

Washiriki wa kutaniko wakiwa wamekusanyika katika Jumba la Ufalme la Makiyivka lililopo katika eneo la vita ili kusikiliza mkutano uliounganishwa kwa mfumo wa video kutoka ofisi ya tawi ya Ukrainia.

Ofisi ya tawi ya Ukrainia ilishirikiana na ofisi ya tawi ya Urusi, kurekodi programu nzima ya mkutano huo katika mfumo wa video na kuionyesha kwa Mashahidi wanaoishi nchini Belarus na Urusi. Matokeo ni kwamba, programu hiyo ilitazamwa na Mashahidi 186,258 wa nchini Belarus na Urusi ukiongeza idadi ya Mashahidi 150,841 wa nchini Ukrainia, na kufanya jumla ya Mashahidi waliotazama programu hiyo kuwa 337,099.

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia, Gustav Berki alisema hivi: “Ripoti kuhusu jitihada zetu za kutoa misaada zimewapa faraja wote walio katika eneo la vita. Tulitiwa moyo sana tulipopata taarifa ya jinsi halmashauri ya kutoa misaada ya Rostov-on-Don, Urusi, inavyotunza rafiki zetu ambao ni wakimbizi.”

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Urusi, Yaroslav Sivulskiy, alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa kuwa wenye kufanya amani na kutounga mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa. Mkutano huo ulitia ndani hotuba zilizozungumzia sababu zinazopatikana katika Biblia zinazofanya tusiunge mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa. Ulisaidia kueleza kwa nini hatuungi mkono upande wowote katika vita hata iwe sisi ni Warusi, Waukrainia, au raia wa taifa lolote lile.”

Mashahidi wawili wa Yehova katika eneo la Horlivka, mkoa wa Donetsk, walipona shambulio la roketi lililopiga nyumba yao wakiwa ndani.

Kufikia sasa, ofisi ya tawi ya Ukrainia imeunda Halmashauri 14 za Kutoa Misaada ili kuwasaidia waathirika wa vita. Halmashauri hizo zimetoa msaada wa tani 149 za chakula na tani 21 za nguo kwa waabudu wenzao na wengine ambao si Mashahidi katika eneo hilo. Pia, halmashauri hizo zimeandaa makazi kwa ajili ya wakimbizi zaidi ya 7,600 na zimeweza kurekebisha au kujenga nyumba zilizoharibiwa na Majumba ya Ufalme (majengo ya ibada). Kwa mfano, siku mbili tu baada ya shambulio katika jiji la Mariupol, Halmashauri ya Kutoa Misaada ilipanga wajitoleaji 160 waanze kazi ya kurekebisha nyumba 34 zilizoharibiwa.

Eneo la maegesho ya magari lililoshambuliwa na roketi lililo karibu na Jumba la Ufalme (halijaonyeshwa kwenye picha) jijini Mariupol.

Bwana Berki anafafanua zaidi kwa nini halmashauri hizo zinazosimamiwa na ofisi ya tawi ya Ukrainia hazitoi tu msaada wa kimwili. Anasema hivi: “Zaidi ya mkutano huo wa pekee, wahudumu wanaosafiri wanaendelea kutembelea vikundi 136 ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo la vita. Kama ilivyo kawaida katika makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova duniani kote, wazee wa makutaniko wanajitahidi kutoa faraja na msaada wa kiroho kwa washiriki wenzao.”

Wanahabari wanaweza kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya habari za umma, simu. +1 718 560 5000

Belarus: Pavel Yadlouski, simu. +375 17 292 93 78

Urusi: Yaroslav Sivulskiy, simu. +7 812 702 2691

Ukrainia: Gustav Berki, simu. +38 032 240 9323