Hamia kwenye habari

Ijumaa, Agosti 4, 2017, kikundi maalumu cha kuzuia magaidi pamoja na wanajeshi na polisi walivuruga mikutano ya kidini ya Mashahidi wa Yehova jijini Alchevsk na Luhansk, kwa madai ya tishio la bomu

DESEMBA 13, 2017
UKRAINIA

Uhuru wa Ibada Uko Hatarini Mashariki mwa Ukrainia

Uhuru wa Ibada Uko Hatarini Mashariki mwa Ukrainia

Mgogoro ambao umeendelea kwa miaka minne sasa katika baadhi ya maeneo ya Luhansk na Donetsk, mashariki mwa Ukrainia, umesababisha kuzorota kwa hali ya maisha na kusababisha hali ngumu kwa wakazi wengi. Mkazo ni mkali zaidi kwa Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika eneo hilo kwa sababu ya kuongezeka kwa ubaguzi wa kidini. Inaonekana kwamba wenye mamlaka wanachochewa na maamuzi ya hivi karibuni ya mahakama nchini Urusi ambayo yalipiga marufuku ibada ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo. Wakiiga nchi ya Urusi, baadhi ya wenye mamlaka wanatumia njia zisizo za haki kuwakandamiza Mashahidi wanaoishi katika maeneo yao kwa kuwashtaki kuwa ni wahalifu na kutishia uhuru wao wa ibada.

Uthibitisho wa Uwongo

Wakifuata mbinu zilizotumiwa na waendesha-mashtaka wa Urusi, wenye mamlaka katika maeneo hayo wamekuwa wakitumia uthibitisho wa uwongo kuwashtaki Mashahidi wa Yehova.

  • Mnamo Julai 2017, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Watu wa Donetsk iliweka makala mbili za magazeti ya zamani ya kidini ya Mashahidi kwenye Orodha Jamhuri ya Machapisho Yenye Msimamo Mkali. Mashahidi hawakupewa taarifa ya jinsi kesi hiyo ilivyoendeshwa, wala hawakuweza kupata nakala ya hukumu iliyotekelezwa haraka ili waweze kukata rufaa.

  • Mnamo Agosti 2017, ofisi ya mwendesha-mashtaka ya Novoazovsk na Debaltsevo ilituma barua za kuwaonya Mashahidi wa maeneo hayo, ikiwaamuru wasisambaze magazeti yao ya kidini ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! bila kupata kibali cha serikali. Kwa njia hiyo, wenye mamlaka wanazuia kusambazwa kwa machapisho ya kidini hata yale ambayo hayakutangazwa kuwa na msimamo mkali na wametishia kuwawajibisha kisheria wazee wa kutaniko ikiwa chapisho lolote la Mashahidi litasambazwa. Barua kama hiyo ya onyo ilitumwa baadaye kwa Mashahidi walioko jijini Makeyevka.

  • Agosti 4, 2017, kikundi maalumu cha kuzuia ugaidi, pamoja na wanajeshi na polisi, walivuruga mikutano ya kidini ya Mashahidi wa Yehova jijini Alchevsk na Luhansk, wakidai kwamba kulikuwa na tishio la bomu. Baada ya kuwaondoa watu wote waliofika kwa ajili ya ibada, maofisa walikagua hati za kila mtu aliyehudhuria. a

Mkutano wa kidini uliovamiwa jijini Alchevsk

Katika eneo la Alchevsk, maofisa walirekodi video ya upekuzi waliofanya katika jengo hilo kwa madai ya kutafuta bomu. Kwenye upekuzi huo walipata machapisho machache ya kidini ya Mashahidi na kisha “walipata” majarida yenye habari ya kuipinga Jamhuri ya Watu wa Luhansk (LPR b) ambayo maofisa waliingia nayo kimagendo na kuyapandikiza.

Mashtaka Yasiyo na Msingi ili Kutetea Uhalali wa Kuzuia Utendaji wa Kidini

Majuma kadhaa baada ya uvamizi wa Jumba hilo la Ufalme, wenye mamlaka jijini Luhansk walitangaza bila kuwa na msingi wowote kwamba Mashahidi wa Yehova ni maadui wa serikali. Agosti 28, 2017, msaidizi wa Waziri wa Ulinzi katika Jamhuri ya watu wa Luhansk, Oleksandr Basov, alitoa maelezo rasmi ya kuwakashifu Mashahidi wa Yehova. Alirejelea yale machapisho yenye habari zisizo za kweli ambayo yalipandikizwa na “kupatikana” katika Jumba la Ufalme la Alchevsk kuwa uthibitisho wa madai yake kwamba Mashahidi wanaunga mkono vikundi ambavyo vinajulikana kuwa vya kigaidi katika eneo la Luhansk.

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia, Ivan Riher, alisema hivi: “Chapisho lolote la aina hiyo ambalo Msaidizi wa Waziri Basov anaeleza kwamba ‘lilipatikana’ katika Jumba la Ufalme lazima lilipandikizwa na mtu fulani katika kikundi kilichogundua jarida hilo. Machapisho hayo huenda yalisambazwa katika jiji la Alchevsk, lakini kwa hakika hayakusambazwa na Mashahidi wa Yehova. Mashahidi wa Yehova hawaungi upande wowote, kama inavyothibitishwa na mamia ya Mashahidi ambao sasa wamefungwa duniani pote kwa kukataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Hakuna Shahidi wa Yehova yeyote ambaye amepigana katika mapigano yanayoendelea nchini Ukrainia.” c

Kuongezeka kwa Mkazo kwa Mashahidi wa Yehova

Mashahidi wa Yehova kadhaa katika eneo hilo wameripoti kwamba wenye mamlaka wamewazuia wasizungumze na wengine kuhusu imani yao na ingawa hakuna hata mmoja wao ambaye ameshtakiwa polisi, wameonywa wasiendelee kuwaeleza wengine kuhusu imani yao. Mashahidi wengi wameripoti pia kwamba watumishi wa Usalama wa Taifa wamewaita ili kufanya mikutano na maofisa. Wakati wa mikutano hiyo, Mashahidi walihojiwa, walitishwa, na kushinikizwa wataje majina ya watu wanaoongoza utendaji wao wa kidini. Pia, wenye mamlaka katika maeneo hayo wamevamia na kuvuruga ibada.

Kuongezeka kwa ubaguzi wa kidini na mkazo kwa Mashahidi wa Yehova katika baadhi ya maeneo ya Luhansk na Donetsk ni kubaya zaidi kuliko kusumbuliwa—hayo ni mateso ya kidini na tishio kwa uhuru wa ibada. Mashahidi wa Yehova wamekuwa na tahadhari zaidi na wanatafuta msaada wa kisheria ili waweze kuendelea kufanya utendaji wao wa kidini kwa amani.

a Katika jiji la Alchevsk, wazee wawili walihojiwa siku nzima. Walieleza kwamba wakati wote wa mgogoro, kutaniko lilikuwa likiendelea kufanya mikutano ya ibada bila kusumbuliwa katika Jumba lao la Ufalme ambalo liko karibu na ofisi ya kamanda wa jeshi. Hata hivyo, mzee mmoja alitozwa faini ya dola 83 za Marekani kwa kupanga mikutano wakati wa vita na dola 48 za Marekani kwa kukiuka utaratibu wa mfumo wa kuzima moto katika Jumba la Ufalme.

b LPR, au Jamhuri ya Watu wa Luhansk, inadhibiti baadhi ya maeneo katika eneo la Luhansk.

c Katika kiangazi cha mwaka wa 2014, rais wa Ukrainia alitoa agizo la kuandikishwa kwa wanajeshi ili kukabiliana na mgogoro katika maeneo ya Donestsk na Luhansk. Vitaliy Shalaiko, aliyekuwa mwanajeshi wa jeshi la Ukrainia, ambaye sasa ni Shahidi wa Yehova, alijibu taarifa hiyo ya kuitwa jeshini kwa kueleza kwamba yeye hawezi kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Juni 23, 2015, Mahakama Kuu ya Ukrainia inayoshughulikia Kesi za Kiraia na Uhalifu iliunga mkono haki yake ya kutojiunga na utumishi wa kijeshi hata watu wanapoandikishwa kwenda jeshini. Maelfu ya Mashahidi wengine nchini Ukrainia wamekuwa na msimamo thabiti kama huo.