Hamia kwenye habari

Ndugu David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, na mke wake wakisalimiwa kwa uchangamfu walipowasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Lviv Danylo Halytskyi.

NOVEMBA 9, 2018
UKRAINIA

Kuonyesha Ukarimu na Umoja Wakati wa Kusanyiko la Pekee Nchini Ukrainia

Kuonyesha Ukarimu na Umoja Wakati wa Kusanyiko la Pekee Nchini Ukrainia

Mashahidi wa Yehova nchini Ukrainia waliwakaribisha maelfu wa ndugu na dada kwa ajili ya kusanyiko la pekee lililofanywa Lviv, Ukrainia, Julai 6-8, 2018. Wajumbe zaidi ya 3,300 kutoka nchi tisa walisafiri kwenda Ukrainia, hasa ili kunufaika na programu ya kiroho yenye kichwa “Uwe Jasiri”! Pia, walifurahia ukarimu walioonyeshwa na wenyeji wao wa Ukrainia.

Matayarisho kwa ajili ya kusanyiko yalianza Aprili 2017, na kwa miezi 15 iliyofuata Mashahidi wenyeji walijitolea kusaidia kupanga shughuli za kusanyiko na kuwatunza akina ndugu waliotembelea. Wajumbe walifurahia mambo ya pekee katika utamaduni wa Kiukrainia ambayo yalitia ndani kucheza dansi na kupiga muziki, na chakula cha kitamaduni. Walipangiwa kutembezwa katika jumba la makumbusho, makasri ya kale, na walienda kuona sehemu fulani ya milima yenye kuvutia ya Carpathia. Jambo moja la pekee lilikuwa fursa ya kuandamana na Mashahidi wa Ukrainia katika huduma ya shambani.

Programu ya kusanyiko ilifanywa kwenye uwanja mkubwa jijini Lviv, na kilele cha wahudhuriaji kilikuwa watu zaidi ya 25,000. Sehemu kuu za programu hiyo zilipeperushwa kwenye viwanja vingine 15 na Majumba mengi ya Ufalme kotekote nchini, jumla ya watu waliohudhuria ilikuwa zaidi ya 125,000 na watu 1,420 walibatizwa.

Ivan Riher, mshiriki wa ofisi ya tawi ya Ukrainia, alisema hivi: “Tulitazamia kwa hamu kubwa tukio hili la pekee na fursa ya kuwakaribisha ndugu na dada kutoka nchi nyingine. Tulifurahia kuwaonyesha wageni wetu ukarimu wa Waukrainia na tulihisi kwamba umoja na ujasiri wa familia yetu ya waabudu ulimwenguni pote umeimarishwa.”—Zaburi 133:1.

 

Kilele cha wahudhuriaji jijini Lviv kilikuwa watu 25,489.

Mmoja kati ya watu wenye umri mkubwa zaidi aliyebatizwa ambaye alikuwa miongoni mwa wale 1,420 waliobatizwa.

Mmoja kati ya vijana wengi waliobatizwa kwenye kusanyiko hilo.

Wahubiri wenyeji waliungana na wajumbe kwenye huduma ya shambani ili kuwakaribisha watu kwenye kusanyiko.

Ofisi ya tawi ilikodi Jumba la Opera la Lviv ambalo lina jukwaa kubwa zaidi jijini. Wajumbe walifurahia maonyesho mbalimbali kutia ndani nyimbo na dansi za Ukrainia. Programu ilimalizia kwa kuimba wimbo wenye kichwa “Jina Lako Ni Yehova.”

Mashahidi wenyeji wakiwatumbuiza wajumbe na dansi ya Kiromani katika Kasri la Svirzh.

Programu ilipomalizika, wahubiri walitumia mabango kuwaeleza ndugu na dada waliowatembelea kwamba wanawapenda.