Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 11, 2024
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Biblia Saba Zatolewa Katika Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni Agosti 2024

Biblia Saba Zatolewa Katika Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni Agosti 2024

Kiibinda

Agosti 2, 2024, Ndugu Carlos Hortelão, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Angola, alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pamoja na vitabu vya Biblia vya Mwanzo, Ruthu, Esta, na Yona katika Kiibinda. Tangazo hilo lilitolewa katika siku ya kwanza ya Kusanyiko la Eneo la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” jijini Cabinda, Angola. Jumla ya watu 953 walihudhuria programu hiyo. Wale waliohudhuria walipata nakala iliyochapishwa ya Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Vitabu vya Maandiko ya Kiebrania na pia Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vilikuwa tayari kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library.

Kuna zaidi ya watu 716,000 wanaozungumza Kiibinda wanaoishi nchini Angola. Hii ni tafsiri ya kwanza kabisa ya Biblia katika Kiibinda. Sasa ndugu na dada 335 wanaotumikia katika makutaniko 13 ya Kiibinda pamoja na kikundi kimoja nchini Angola, wanafurahia kusoma Neno la Mungu katika lugha yao.

Lugha ya Ishara ya Zimbabwe

Agosti 9, 2024, Ndugu Energy Matanda, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zimbabwe, alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Lugha ya Ishara ya Zimbabwe katika Kusanyiko la Eneo la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” jijini Harare, Zimbabwe. Kwa jumla, watu 405 walihudhuria kusanyiko hilo. Baada tu ya kutolewa, Biblia hiyo ilipatikana kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library Sign Language.

Kitabu cha Mathayo kilitolewa katika Lugha ya Ishara ya Zimbabwe mwaka wa 2021. Tangu wakati huo, vitabu vingine vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vimetafsiriwa pia. Inakadiriwa kuwa watu milioni moja hivi hutumia Lugha ya Ishara ya Zimbabwe, kutia ndani ndugu na dada 377 wanaotumikia katika makutaniko 11 ya Lugha ya Ishara na vikundi 11 nchini Zimbabwe.

Kibulgaria

Agosti 11, 2024, Ndugu Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kwamba toleo lililorekebishwa la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya linaendelea kutafsiriwa katika Kibulgaria, na alitoa vitabu vya Biblia vya Mathayo, Marko, na Luka katika hotuba ya mwisho ya Kusanyiko la Pekee la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” jijini Sofia, Bulgaria. Jumla ya watu 5,418 walihudhuria. Baada ya kutolewa, vitabu vyote vitatu vya Biblia vilikuwa tayari kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library.

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa kwa mara ya kwanza katika Kibulgaria mwaka wa 2009. Leo, ndugu na dada 3,000 hivi wanatumikia katika makutaniko 57 nchini Bulgaria.

Kiaja

Agosti 16, 2024, Ndugu Bois Sylvain, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Afrika Magharibi, alitangaza kutolewa kwa vitabu vya Biblia vya Mathayo na Marko katika Kiaja kwenye Kusanyiko la Eneo la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” jijini Djakotomey, Benin. Kusanyiko hilo lilihudhuriwa na watu 631. Zaidi ya hilo, wengine 435 waliohudhuria kusanyiko hilo kwenye Jumba la Kusanyiko jijini Abomey-Calavi, Benin, waliunganishwa kupitia video mtandaoni kwa ajili ya hotuba hiyo ya kutolewa kwa Biblia. Baada ya kutolewa, vitabu hivyo viwili vya Biblia vilikuwa tayari kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library.

Kuna zaidi ya watu milioni 1.2 nchini Benin na Togo wanaozungumza Kiaja. Kuna tafsiri nyingine mbili za Maandiko ya Kigiriki katika Kiaja. Hata hivyo, si rahisi kuzipata na zinatumia lugha ambayo ni ngumu kuelewa. Isitoshe, tafsiri hizo hazitumii jina la kibinafsi la Mungu, Yehova. Leo, kuna ndugu na dada 1,300 hivi wanaotumikia katika makutaniko 25 ya Kiaja na kikundi kimoja nchini Benin, na pia makutaniko 12 na vikundi 2 nchini Togo. Wote wanafurahi sana kuwa na Biblia ambayo ni rahisi kuelewa na inayotumia jina la Mungu mahali panapofaa.

Kinyarwanda

Agosti 16, 2024, Ndugu Jeffrey Winder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kutolewa kwa toleo lililorekebishwa la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kinyarwanda. Ndugu Winder alitoa tangazo hilo katika siku ya kwanza ya Kusanyiko la Eneo la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” jijini Kigali, Rwanda. Kusanyiko hilo lilihudhuriwa na watu 9,908. Wengine 1,141 waliohudhuria kusanyiko hilo katika maeneo mengine mawili waliunganishwa kwenye programu hiyo. Wote walipata nakala zilizochapishwa za Biblia. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika mfumo wa kielektroni na pia rekodi za sauti za Biblia hiyo zilipatikana kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library.

Kuna watu zaidi ya milioni 13 wanaozungumza Kinyarwanda nchini Rwanda. Pia, Kinyarwanda kinazungumzwa katika nchi nyingine kama vile, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Tanzania, na Uganda. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa ikiwa nzima kwa mara ya kwanza katika Kinyarwanda mwaka wa 2010. Sasa, kuna ndugu na dada zaidi ya 35,500 wanaotumikia katika makutaniko 634 ya Kinyarwanda nchini Rwanda.

Kisinhala

Agosti 16, 2024, Ndugu David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kutolewa kwa toleo lililorekebishwa la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kisinhala, siku ya kwanza ya Kusanyiko la Eneo la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” jijini Colombo, Sri Lanka, lililokuwa na hudhurio ya watu 4,273. Isitoshe, watu 1,045 waliohudhuria Kusanyiko hilo la Eneo jijini Chilaw, Sri Lanka, waliunganishwa kusikiliza programu hiyo kupitia video mtandaoni. Wote waliohudhuria kusanyiko hilo katika maeneo hayo walipata nakala zilizochapishwa za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kisinhala. Biblia hiyo pia ilitolewa katika mfumo wa kielektroni na ilikuwa tayari kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library.

Mashahidi wa Yehova walianza kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika Kisinhala zaidi ya miaka 75 iliyopita. Leo, kuna zaidi ya watu milioni 15 wanaozungumza Kisinhala nchini Sri Lanka, kutia ndani ndugu na dada 4,808 wanaotumikia katika makutaniko 62 ya Kisinhala nchini humo.

Kiwalisian

Agosti 30, 2024, Ndugu Martin Décousus, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya New Caledonia, alitangaza kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa nzima katika Kiwalisian kwenye Kusanyiko la Eneo la 2024 la “Tangaza Habari Njema!” Kusanyiko hilo lilifanywa katika jiji la Nouméa, New Caledonia, na pia katika kijiji cha Mala’e, kwenye visiwa vya Wallis na Futuna. Maeneo hayo yaliunganishwa kupitia video mtandaoni. Watu 317 waliohudhuria walipata nakala zilizochapishwa za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Biblia hiyo pia ilipatikana kwa ajili ya kupakuliwa kwenye jw.org na programu ya JW Library.

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kiwalisian mwaka wa 2018. Ndugu na dada 153 wanaozungumza Kiwalisian wanaotumikia katika makutaniko mawili huko New Caledonia na kwenye visiwa vya Wallis na Futuna wanatazamia kwa hamu kutumia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kushiriki habari njema na zaidi ya watu 35,000 wanaozungumza Kiwalisian katika maeneo hayo.