Hamia kwenye habari

FEBRUARI 19, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Biblia ya Kwanza Kamili ya Lugha ya Ishara Sasa Yapatikana

Biblia ya Kwanza Kamili ya Lugha ya Ishara Sasa Yapatikana

Februari 15, 2020, Ndugu Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kutolewa kwa kitabu cha mwisho cha Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Lugha ya Ishara ya Marekani (ASL). Hii ndiyo tafsiri ya kwanza ya Biblia iliyo kamili ya lugha ya ishara (alama) ulimwenguni. Tangazo hili la kihistoria ndilo lililokuwa jambo kuu katika programu ya kuweka wakfu majengo mapya ya Ofisi ya Utafsiri (RTO), huko Fort Lauderdale, Florida, Marekani. Majengo hayo yatatumiwa katika kazi ya kutafsiri ya Lugha ya Ishara ya Marekani. Programu hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Christian Convention Center of Jehovah’s Witnesses huko West Palm Beach, Florida.

Zaidi ya watu 2,500 walihudhuria programu hiyo na wengine 15,635 waliunganishwa kupitia Intaneti katika Majumba ya Ufalme huko Belize, Haiti, Jamhuri ya Dominika, Kanada, Marekani, na Trinidad na Tobago na hivyo kufanyiza jumla kuu ya zaidi ya wahudhuriaji 18,000.

Ndugu Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akiongoza mahojiano wakati wa programu

Baada ya kutoa hotuba ya wakfu, Ndugu Jackson alitangaza kutolewa kwa kitabu cha mwisho cha Biblia ya lugha hiyo ya ishara. Mwishoni mwa hotuba yake alisema hivi: “Tungependa kuwaambia jambo fulani—jambo la pekee sana. Kutolewa kwa kitabu cha Ayubu, sasa kumefanya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikamilike . . . Kulingana na kile tunachojua, Mashahidi wa Yehova ndiyo tengenezo la kwanza au kikundi cha watu kutoa Biblia kamili ya Lugha ya Ishara ya Marekani. Na huenda hilo likamaanisha kwamba hii ndiyo Biblia ya kwanza kamili kupatikana katika lugha ya ishara ulimwenguni pote [na] katika historia ya wanadamu.”

Kutolewa kwa kitabu cha Ayubu kumekamilisha kazi ya miaka 15 ya kutafsiri. Baraza Linaloongoza liliidhinisha Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ianze kutayarishwa katika Lugha ya Ishara ya Marekani mwaka wa 2004. Miaka miwili baadaye, kitabu cha Mathayo kilitolewa, na vitabu vingine vya Maandiko ya Kigiriki vilitolewa hatua kwa hatua hadi mwaka wa 2010. Imechukua miaka 10 kutafsiri Maandiko ya Kiebrania.

Kutolewa hatua kwa hatua kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Lugha ya Ishara ya Marekani kumekuwa na matokeo mazuri kwa viziwi. Isias Eaton, mhubiri aliyehudhuria programu hiyo alisema hivi: “Nilipoitazama tafsiri hii kwa mara ya kwanza, nilianza kulia. Nilipokuwa nikisoma Biblia katika Kiingereza haikunigusa moyo, lakini nilipoanza tu kutazama Biblia hii katika lugha ya ishara, nilianza kutokwa na machozi.

Tafsiri hii imebadili sana huduma ya wahubiri wengi katika makutaniko ya lugha ya ishara. David Gonzalez, mtafsiri wa Biblia ya ASL katika Ofisi ya Utafsiri anasema hivi: “Imenisaidia kuelewa kweli vizuri zaidi na hivyo kuwa jasiri na hodari ninapokuwa utumishini. Kabla ya kuwa na Biblia hii ya ASL, sikujiamini na nilisali kwamba mwenye-nyumba asiniulize maswali magumu. Lakini kwa kuwa sasa Biblia yote inapatikana katika Lugha ya Ishara ya Marekani, niko tayari. Ninajiamini!”

Ndugu Nicholas Ahladis, anayesaidia kuratibu shughuli za Idara ya Huduma za Tafsiri katika makao makuu ya Warwick, New York anasema hivi: “Mradi wa kutafsiri Biblia katika ASL umefungua njia kwa ajili ya lugha nyingine za ishara. Sasa, sehemu mbalimbali za Biblia zinapatikana katika lugha za ishara 17, na nyingine nyingi zinaendelea kuandaliwa.”

Bila shaka, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyo kamili katika Lugha ya Ishara ya Marekani itawasaidia wengi zaidi kumkaribia Yehova mioyo yao inapoendelea kusukumwa na Neno lake katika lugha yao wenyewe.—Matendo 2:6.