Hamia kwenye habari

Dmitriy Dolzhikov ndiye Shahidi wa 100 kufungwa kati ya Mashahidi ambao kwa sasa wamefungwa chini ya sheria ya Urusi kwa sababu ya kushiriki katika utendaji wa Kikristo

OKTOBA 28, 2022
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Idadi ya Mashahidi Walio Gerezani Katika Urusi na Crimea Yazidi 100

Idadi ya Mashahidi Walio Gerezani Katika Urusi na Crimea Yazidi 100

Kufikia Oktoba 26, 2022, kulikuwa na ndugu 106 na dada 4 gerezani au kizuizini katika Urusi na Crimea. Wote hao wamefungwa kwa sababu ya imani yao. Ndugu Dmitriy Dolzhikov, mwenye umri wa miaka 44, amekuwa Shahidi wa 100 kufungwa kati ya ndugu na dada hao walio gerezani kwa sasa. Dmitriy alikamatwa Septemba 8, 2022. Anakabili shtaka la kushiriki katika utendaji wa shirika lenye msimamo mkali kwa sababu ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuwaeleza wengine kuhusu imani yake. Tangu marufuku ilipotangazwa mwaka wa 2017, Mashahidi 350 hivi wamefungwa gerezani kwa muda fulani.

Maofisa wa polisi walimkamata Dmitriy baada ya kuvamia nyumba yake katika Eneo la Chelyabinsk. Siku mbili baadaye, alipelekwa mahabusu katika Eneo la Novosibirsk, lililo umbali wa kilometa 1,500 hivi kutoka nyumbani kwake.

Dmitriy amewekwa katika chumba cha gereza pamoja na watu wengine 12. Marina ambaye ni mke wa Dmitriy, haruhusiwi kumtembelea lakini wanawasiliana kupitia barua.

Marina anaeleza: “Dmitriy alipokamatwa, mwanzoni sikulala vizuri na mara nyingi nilijipata nimeamka usiku baada ya usingizi kupotea. Rafiki zetu kutanikoni walinialika nikae nao, walinisaidia sana na walinitia moyo.”

Marina pia anaeleza kwamba Dmitriy amekuwa na utulivu na shangwe. Anasema, “Yehova anamtunza.”

Marina na Dmitriy Dolzhikov

Ndugu na dada zetu wameshtakiwa chini ya Sheria ya Uhalifu ya Shirikisho la Urusi kuhusu utendaji wenye msimamo mkali. Miongoni mwa dada zetu ni Anna Safronova, mwenye umri wa miaka 57, ambaye kwa sasa anatumikia kifungo cha miaka sita gerezani. Dada huyo ndiye aliyehukumiwa kifungo cha muda mrefu zaidi gerezani.

Kukamatwa kwa Dmitriy ni tukio lingine la aibu katika kampeni ya Urusi dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Kampeni hiyo imekuwa ikiendelea kwa zaidi ya miaka mitano licha ya kwamba mashirika mengi ya kimataifa yameikemea nchi ya Urusi kwa sababu ya mateso hayo. Mahakama Kuu ya Urusi ilipotoa uamuzi dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 2017, mamlaka ya Urusi ilidai ingefunga mashirika ya kisheria ya Mashahidi lakini haingeingilia utendaji wowote wa kiroho. Hata hivyo, wamekuwa wakifanya kinyume na hilo. Kufikia sasa, kesi 308 za uhalifu zimefunguliwa dhidi ya Mashahidi 700 hivi wa Yehova. Isitoshe, zaidi ya nyumba 1,851 za Mashahidi zimevamiwa.

Tunaendelea kusali kwa ajili ya Dmitriy na ndugu na dada zetu wote wanaoteswa kwa sababu ya imani yao. Tunajua kwamba Yehova ataendelea kuwapa nguvu wanazohitaji ili kuvumilia.​—Mathayo 24:13.