Hamia kwenye habari

JW Stream–Studio inawawezesha wahubiri (kushoto) kuwatazama wasemaji wa eneo lao (kulia) wakitoa sehemu zao katika kusanyiko la mzunguko moja kwa moja

APRILI 1, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

JW Stream–Studio Yaanzishwa

JW Stream–Studio Yaanzishwa

Sasa Wahubiri Wanaweza Kutazama Moja kwa Moja Programu ya Kusanyiko la Mzunguko Wao

Hivi karibuni Mashahidi wa Yehova walitoa tovuti ya JW Stream-Studio, tovuti mpya iliyobuniwa kupeperusha moja kwa moja matukio ya mzunguko yanayofanywa na mwangalizi wa mzunguko. Machi 6 na 7, 2021, programu za makusanyiko 340 ya mzunguko yalifanywa ulimwenguni pote kwa kutumia mbinu hiyo. Zaidi ya watu 500,000 walitazama matukio hayo.

Fundi mitambo wa kuendesha studio akiandaa msaada wa kiufundi kwa ajili kusanyiko la mzunguko

Muda fulani baada ya janga la ugonjwa wa virusi vya corona kuanza, Halmashauri ya Ufundishaji ilielekeza Idara ya Utangazaji ya makao makuu ya ulimwenguni pote itokeze tovuti inayowezesha waangalizi wa mzunguko kupeperusha matukio ya mzunguko moja kwa moja kupitia mtandao. Lengo lilikuwa kutokeza kifaa ambacho kingewaruhusu maelfu ya watumiaji kutazama programu inayopeperushwa moja kwa moja.

Idara ya Utangazaji iliwapa mgawo kikundi kidogo cha ndugu na dada ambao wangeshughulikia mradi huo. Wakati wa kazi hiyo, kikundi hicho kilihitaji kushughulikia changamoto kadhaa.

Kwa mfano, tovuti ilihitaji kuwa rahisi kueleweka kwa kuwa baadhi ya akina ndugu ambao wangeitumia hawangekuwa na ustadi mkubwa wa kiufundi. Pia, ilipaswa kufanya kazi vizuri hata katika maeneo yaliyo na kiwango kidogo cha Intaneti. Isitoshe, Idara ya Utangazaji ilifanya kazi pamoja na Idara ya Kompyuta ya makao makuu ya ulimwenguni pote ili kupata sava za kutosha zitakazoweza kukidhi kiwango kikubwa cha watumiaji wa tovuti hiyo.

Alex Hernandez anayefanya kazi katika Idara ya Utangazaji anasema hivi: “Kazi ya kutokeza kifaa cha kushughulikia mamia ya makusanyiko kwa wakati uleule ilikuwa yenye kusisimua na yenye kutahini. Tulikuwa na kikundi kidogo cha wataalamu wa kubuni programu, na kwa wengi wao hii ilikuwa mara ya kwanza kutokeza tovuti kwa ajili ya mawasiliano ya moja kwa moja.”

Michoro ya kwanza ya muundo wa JW Stream-Studio ilikamilishwa mnamo Mei 2020. Miezi mitano tu baadaye, Oktoba 2020, Idara ya Utangazaji ilianza kujaribu tovuti hiyo kwa msaada wa waangalizi wa mzunguko katika nchi sita tofauti. Mchakato wa majaribio uliiruhusu Idara ya Utangazaji kutambua na kushughulikia changamoto zilizojitokeza kabla ya tarehe iliyowekwa ya kuanza kutumia tovuti hiyo. Kikundi cha ndugu na dada 17 walikuwepo ili kuandaa msaada wakati wa majaribio hayo.

Familia ya Amadiz nchini Marekani wapiga picha kabla ya kusanyiko la mzunguko kuanza. Kusanyiko hilo lilipeperushwa moja kwa moja kupitia JW Stream–Studio

Alex anaendelea kusema hivi: “Kila mara tulipokabili changamoto tulitua na kusali kuhusu jambo hilo. Tulipopata suluhisho, tulisadikishwa kwamba Yehova alitusaidia.”

Tayari ndugu na dada wengi wameshukuru sana kwa tovuti hii mpya.

Ndugu Jairo Espinosa nchini Kolombia anasema hivi: “Tulihisi kwamba programu ya kusanyiko lililofanywa kupitia JW Stream–Studio lilitusaidia kuimarisha umoja wetu wa Kikristo na kutusaidia tujihisi tukiwa karibu na ndugu zetu. Mbali na hilo, kujua kwamba programu hiyo ilikuwa ikipeperushwa moja kwa moja kulitusaidia kuwa makini kabisa hotuba zilipokuwa zikitolewa. Hatukutaka kukosa jambo lolote. Ilikuwa baraka kubwa sana!”

Dada Magaly Reymundo nchini Marekani anasema hivi: “Ninajua kwamba hata katika hotuba zilizorekodiwa ujumbe ni uleule, lakini nilifurahia sana kuona nyuso za watu ninaowafahamu wakitoa hotuba moja kwa moja.”

Tangu JW Stream–Studio ilipotolewa, tayari imetumiwa kupeperusha zaidi ya makusanyiko 800 ya mzunguko. Tunamshukuru Yehova kwa kutuandalia kifaa kingine cha kutusaidia kuendelea kuwa imara kiroho na wenye umoja.—Zaburi 133:1.