Hamia kwenye habari

JANUARI 8, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Kampeni ya Kutangaza Ufalme ya 2020: Ndugu na Dada Ulimwenguni Pote Walitiwa Moyo na “Tukio la Pekee”

Kampeni ya Kutangaza Ufalme ya 2020: Ndugu na Dada Ulimwenguni Pote Walitiwa Moyo na “Tukio la Pekee”

Mashahidi wa Yehova watakumbuka mwezi wa Novemba 2020 kwa njia ya pekee katika historia yao. Wengi wetu tumelazimika kukaa katika nyumba zetu kwa sababu ya ugonjwa wa virusi vya corona. Tumeacha kwa muda kutumia njia za kuhubiri tunazotumia kwa ukawaida. Licha ya hayo, watumishi wa Yehova walifanikiwa kumaliza kampeni ya ulimwenguni pote ya kutangaza Ufalme wa Mungu. Ulimwenguni pote, mamilioni ya wahubiri walifanya kazi kwa bidii ya kusambaza gazeti Mnara wa Mlinzi Na. 2 2020 kwa wafanyabiashara, maofisa wa umma, walimu, marafiki, watu wa ukoo, na watu wengine. Jitihada hizo ziliwatia moyo watu wote waliokuwa tayari kusikiliza. Lakini pia, ziliwaletea shangwe na kuwachochea kiroho wale wote walioshiriki.

Haya ni baadhi ya mambo yaliyoonwa kutoka ndugu na dada zetu ulimwenguni pote:

AUSTRALASIA

Dada Lucinda Furkin

Lucinda Furkin, dada mwenye umri wa miaka kumi na nane, aliyebatizwa hivi karibuni kutoka Australia aliandika hivi: “Ingawa afya yangu ilikuwa mbaya sana katikati ya kampeni, nilihisi Yehova akinitia moyo, akinishika mkono, na kunipa nguvu nilizohitaji ili kuvumilia.”

Baba mmoja nchini New Zealand anafafanua jinsi kampeni hiyo ilivyosaidia familia yake: “Tukiwa wazazi wa mabinti wanne wenye umri wa miaka 7, 9, 11 na 13, tuligundua kwamba kuona kampeni ya ulimwenguni pote kama mgawo binafsi kutoka kwa Baba yetu mwenye upendo, Yehova, kulisaidia familia yetu kudumisha ratiba yetu ya kuhubiri kila siku wakati wa kampeni.”

BOTSWANA

Kagiso na Lydia Marumo, walio katika kazi ya mzunguko, walituma nakala za kielektroni za gazeti hilo kwa watu wao wa ukoo ambao si waamini. Baadhi yao walituma jumbe za kuwashukuru. Mtu mmoja wa ukoo wa Kagiso, ambaye ni daktari, alitaja kwamba gazeti lilifika kwa wakati unaofaa. Alisema baadhi ya wagonjwa wake walikuwa na maswali kumhusu Mungu na kuihusu Biblia na hata watoto wake walikuwa wakiwasiliana na pepo. Ndugu na Dada Marumo waliwasiliana naye na kuanza kujifunza Biblia pamoja naye jioni hiyo. Sasa wanajifunza naye mara mbili kwa juma.

Ndugu Kagiso Marumo pamoja na mke wake, Lydia

KANADA

Dada Soroya Thompson

Soroya Thompson, dada painia anayeishi katika jiji la Ontario, aliandika hivi: “Kampeni ilinisaidia kukazia fikira zaidi mambo muhimu na kuchanganua ni kiasi gani kilichobaki cha kazi tunayopaswa kufanya. Pia, kilikuwa kikumbusho cha upendo wa Yehova na uthibitisho uhakika kwamba kwa kweli hataki yeyote aangamizwe. Kudumisha mtazamo na maoni hayo kumenifanya nitamani kutia bidii hata zaidi wakati wa kampeni.”

Dada kutoka jiji la British Columbia alisema hivi: “Katika nyakati hizo ngumu, niliamua kufanya upainia msaidizi ili nipambane na hisia za kushuka moyo. Kufanya hivyo kulinisaidia mimi na familia yangu tuhisi vizuri.”

Ofisi ya tawi ya Kanada inaripoti kwamba kampeni hiyo ilisaidia familia nyingi kuwa pamoja. Iliwasaidia watoto wadogo wahisi kwamba wanaweza kushiriki katika huduma kwa kuandika barua wao wenyewe au kwa kuwasaidia wengine katika familia kuandika anwani kwenye bahasha, kuweka stempu, na kutafuta anwani.

FINLAND

Ndugu na Dada Tuomisto, walio katika kazi ya mzunguko, walisema hivi: “Novemba ni mwezi wenye giza sana katika eneo hili la kaskazini. Hivyo ndugu na dada, hasa mapainia, walithamini sana kuwa na kampeni iliyowasaidia wasishuke moyo.”

Ndugu Timo Tuomisto pamoja na mke wake, Eeva

Baada ya kumtumia mtu fulani wanayemfahamu gazeti, wenzi fulani wa ndoa walipokea barua ya shukrani iliyosema hivi kwa sehemu: “Leo, [nilikuwa nasoma kitabu cha Biblia] cha Yakobo. Kinasema kwamba imani bila matendo imekufa. Mashahidi wa Yehova sikuzote wamezungumza na watu uso kwa uso, wakieleza na kuwafundisha watu mambo yaliyo katika Biblia. Wanafanya matendo yanayoimarisha imani.”

UGIRIKI

Ofisi ya tawi ya Ugiriki ilisema hivi: “Wengine wamechoshwa na ugonjwa huu wa corona, vizuizi vyake, na amri za kutotoka nje. Kampeni ilikuwa kitia moyo walichohitaji sana. Wengi walisema kwamba kampeni hii ilikuwa kama ‘chemchemi ya kiroho!’”

Dada Suzie Kontargiri

Dada Suzie Kontargiri aliamua kufanya upainia msaidizi licha ya kukabili matatizo ya afya na kuwa na mume asiye mwamini. Alisema hivi: “Niliacha kushuka moyo niliposhiriki katika kampeni. Asubuhi ningeamka nikiwa na shangwe, ningefanya kazi za nyumbani, ningepika chakula, ningemtayarishia mume wangu mahitaji yake, kisha ningeanza kuhubiri. Mume wangu ambaye si mwamini aliniuliza hivi mara nyingi: ‘Leo hufanyi kazi ya kuhubiri?’ kwa sababu alikuwa amezoea kuniona nikihubiri kwa shangwe pamoja na akina dada wengine.”

JAPANI

Dada Tamaki Hirota aliandika barua na kuzituma kwa maofisa wa serikali. Alisema hivi: “Yehova ndiye wa kwanza kutumia barua ili kuwahubiria wanadamu. Aliandika barua 66 ambazo wanadamu wamezisoma tena na tena kwa miaka mingi ili kumkaribia Yeye. Yehova anajua vizuri jinsi mbinu hii ilivyo na matokeo. Kampeni hii ilikuwa tukio la pekee sana.”

Dada Tamaki Hirota

SRI LANKA

Dada Meharaja Vijaya na Dada Imayanathan Amutha waliambiwa kimakosa kwamba waandike barua kwa anwani ileile. Mtu aliyeandikiwa barua hizo aliitupa barua ya kwanza bila kuifungua. Kisha akaiona barua ya pili. Alijiambia kwamba ikiwa barua hizo zimetumwa mara mbili, lazima ujumbe uliomo uwe muhimu sana. Alisoma gazeti, akampigia simu dada aliyemtumia barua ya pili, na akakubali funzo la Biblia.

Kushoto hadi kulia: Dada Meharaja Vijaya na Imayanathan Amutha

Ofisa mmoja aliipigia simu ofisi ya tawi ya Sri Lanka baada ya kupata gazeti. Alisema kwamba hajawahi kuonana na Mashahidi wa Yehova ingawa alikuwa Mkristo. Baada ya kusifu habari zilizo katika gazeti na tovuti yetu, aliuliza hivi: “Ninawezaje kuwa Shahidi wa Yehova?” Mara moja ziara ya kurudia ikapangwa.

MAREKANI

Mhubiri mwenye umri wa miaka 13 anayesoma shule ambayo watu huzungumzia sana siasa, alitaja jinsi kampeni ya Novemba ilivyomsaidia: “Nilipata ujasiri zaidi wa kuwaeleza walimu wangu kwa nini siungi mkono upande wowote. Jambo hilo liliimarisha sana imani yangu.”

Dada Margit Haring

Dada Margit Haring alihisi hivyo pia. Aliandika hivi: “Niliweza kuimarisha ujasiri na bidii yangu. Mwanzoni, kufikiria tu kuzungumza na wafanyabiashara na maofisa wa serikali kuliniogopesha sana. Kujifunza kutetea imani yangu kwa upole ni mazoezi mazuri ya wakati ujao.”

Mzee mmoja alisema: “Niliguswa moyo hasa na waliofanya upainia licha ya kuwa na matatizo mabaya ya afya. Wangeweza kuamua kutofanya upainia. Badala yake, walitumia nafasi hiyo kushiriki katika kampeni. Shangwe na shukrani walizotoa kwa Yehova na ndugu zao mara nyingi ziliwafanya watu wengi watokwe na machozi.”

Kuna mambo mengi yaliyoonwa na yaliyosemwa na ndugu na dada ulimwengu pote—ambayo hatuwezi kuandika yote hapa. Ilikuwa shangwe kubwa kuwatangazia ujumbe wa Ufalme mamilioni ya watu.—Yohana 15:11.