Hamia kwenye habari

APRILI 20, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Kutoa Michango ya Kielektroni Wakati wa Ugonjwa wa Corona

Kutoa Michango ya Kielektroni Wakati wa Ugonjwa wa Corona

Ndugu na dada katika nchi nyingi wamebadili njia yao ya kufanya mambo ya kiroho wakati wa ugonjwa wa virusi vya corona. Katika visa vingi, badala ya kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme akina ndugu wanatumia programu zilizounganishwa kupitia Intaneti. Kwa sababu hiyo, wengi wamebadili njia yao ya kuunga mkono kazi ya kuhubiri ulimwenguni kwa kutoa michango mtandaoni.

Mashahidi wa Yehova katika zaidi ya nchi 112 wanaweza kutumia tovuti ya donate.pr418.com kutoa michango kielektroni, kama kwa kutumia kadi ya benki.

Kwa kuwa wahubiri wengi hawawezi kutoa michango kwenye Jumba la Ufalme, baadhi wameamua kutumia mbinu ya kielektroni katika donate.pr418.com inayowawezesha kutoa mchango wa kujirudia kila mwezi. Dada Susan Cohen, mhubiri aliye na umri wa miaka 74 nchini Marekani, anatumia njia hiyo kutoa michango. Anasema hivi: “Ni rahisi sana; ikiwa mimi ninaweza kuitumia, mtu yeyote anaweza. Ninafurahi kujua kwamba bado ninaweza kutoa michango.”

Ndugu Eduardo Paiva nchini Brazili anasema kwamba hapo awali aliona kutumia njia ya donate.pr418.com ni njia ya badala ya kutoa michango kihalisi. Anasema hivi: “Hivi karibuni, niligundua kwamba ndiyo njia bora zaidi ya kutoa michango ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote kunapokuwa na dharura na hali ngumu. Tunaweza kutumia njia hii ili kuendelea kuonyesha shukrani na upendo katika siku hizi za mwisho.”

Ndugu Gajus Glockentin, ambaye anasimamia Ofisi ya Mweka-Hazina kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Warwick, New York, anasema: “Inatia moyo sana kuona tamaa ya ndugu zetu ya kutegemeza kazi ya Ufalme. Tunathamini sana michango hiyo. Kila wakati tunachunguza utendaji wetu ulimwenguni pote kuona tunawezaje kupunguza gharama ili michango hiyo itumiwe kwa njia bora zaidi. Ingawa baadhi ya ndugu na dada wamehitaji kupunguza kiasi cha michango wanayotoa, utayari wao wa kutegemeza tengenezo la Yehova haujapungua.—2 Wakorintho 9:7.