Hamia kwenye habari

FEBRUARI 26, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Licha ya Ugonjwa wa corona Mashahidi wa Yehova Watoa Msaada kwa Ajili ya Misiba Mingine Mikubwa

Licha ya Ugonjwa wa corona Mashahidi wa Yehova Watoa Msaada kwa Ajili ya Misiba Mingine Mikubwa

Mwaka wa utumishi wa 2020 ulikuwa mwanzo wa jitihada kubwa za tengenezo letu kutoa msaada ulimwenguni pote. Zaidi ya Halmashauri 950 za Kutoa Msaada (DRC) zilianzishwa ulimwenguni pote. Mbali na ugonjwa wa corona, katika mwaka wa 2020 kulikuwa na hali nyingine za dharura na misiba ya asili iliyotokeza uharibifu mkubwa. Halmashauri za Kutoa Msaada zilikabili changamoto ya kufanya kazi yao na wakati uleule kuzingatia miongozo ya kujilinda dhidi ya ugonjwa wa corona. Ndugu na dada walioshiriki katika kazi hiyo wamesema kwamba utendaji huo umeimarisha imani yao. Yafuatayo ni mambo yaliyowaathiri ndugu zetu:

Dhoruba zilizotokeza uharibifu

Katika mwaka wa utumishi wa 2020, kulikuwa na jumla ya dhoruba kubwa 126 ambazo ziliwaathiri ndugu na dada zetu. Hilo ni ongezeko la asilimia 11.5 kwa kulinganisha na mwaka wa utumishi wa 2019. Dhoruba nyingi zilisababisha mafuriko au maporomoko ya ardhi yaliyotokeza uharibifu.

Kwa mfano, vimbunga vingi viliikumba nchi ya Filipino na kuwaacha ndugu na dada wengi bila makao.

Mafuriko nchini Filipino baada ya Kimbunga Vamco, kilichotokea majuma machache tu baada ya Kimbunga Goni, kimbunga kikubwa zaidi kutokea katika historia

Mvua kubwa nchini Nigeria ziliharibu mashamba ya ndugu zetu.

Mafuriko katika Jimbo la Rivers baada ya mvua kubwa kutokea nchini Nigeria

Korea Kusini kulikuwa na majira ya mvua ndefu zilizoambatana na upepo.

Mafuriko nchini Korea Kusini katika majira ya mvua ndefu zaidi kunyesha nchini humo

Moto wa Msituni

Moto wa msituni uliwaka katika nchi nyingi, na kuchoma maeneo makubwa zaidi katika historia.

Kwa mfano, baadhi ya ndugu zetu waliathiriwa na moto mkubwa ulioteketeza maeneo yenye ukubwa wa ekari milioni moja hivi.

Hilo lilitokea nchini Marekani.

Moto wa msituni California, Marekani.

Hali hiyo iliwaathiri pia ndugu zetu nchini Australia.

Moto wa msituni nchini Australia

Kutoa Msaada kwa Njia Salama na Yenye Matokeo

Baada ya majanga hayo kutokea tengenezo liliweka miongozo ya usalama ili kuhakikisha usalama wa wale wanaotoa na kupokea msaada.

Ndugu Han Chan-hee

Ndugu Han Chan-hee, aliyetumikia katika Halmashauri ya Kutoa Msaada nchini Korea Kusini, anaeleza baadhi ya mambo aliyofanya ili kuwalinda ndugu na dada: “Kila asubuhi, tulimpima kila mtu joto la mwili, kila wakati tulidumisha umbali unaofaa kutoka kwa mtu na mwenzake, tukadhibiti idadi ya walitoleaji katika eneo la kazi, na tukaepuka kukusanyika pamoja wakati wa kula na mapumziko. Mbali na hilo, wajitoleaji walipaswa kusafisha vifaa vyao kwa kutumia ya dawa kabla na baada ya kazi.”

Ndugu Chris Shirah

Baadhi ya ndugu zetu walilazimika kuhama au walipoteza nyumba zao wakati wa misiba hii. Ndugu Chris Shirah, aliyesaidia katika Halmashauri ya Kutoa Msaada wakati kulipokuwa na moto wa msituni upande wa Magharibi wa Marekani, anaeleza hivi: “Tulizingatia idadi ya watu tuliowaweka katika nyumba moja ili kutii miongozo inayohusiana na COVID-19.”

Ndugu Philips Akinduro

Katika maeneo mengi, idadi ya watu ambao wangehusika katika jitihada za kutoa msaada ilidhibitiwa na sheria za kudumisha usalama na zilizozuia watu wasisafiri. Ndugu Philips Akinduro aliyetumikia katika Halmashauri ya Kutoa Msaada nchi Nigeria anaeleza hivi: “Changamoto kubwa tuliyokabili ni kwamba serikali ilidhibiti maeneo ambayo watu wangeweza kwenda. Kwa hiyo, haikuwa rahisi kupata wajitoleaji waliohitajika.”

Ndugu Kim Joon-hyeong

Ndugu Kim Joon-hyeong aliyetumikia katika Halmashauri ya Kutoa Msaada ya Korea Kusini anaeleza mtazamo wa wajitoleaji wa kutoa msaada: “Kwa kuwa tulifanya kazi hiyo ya kutoa msaada kwa sababu ya upendo wetu wa Kikristo na Mungu wetu, nyakati zote tulizingatia jinsi ambavyo tungelinda uhai na usalama wa watu wote. Kwa hiyo, licha ya tahadhari hizo za ziada, tulifaulu kudumisha shangwe yetu huku tukiendelea na kazi hiyo ya kutoa msaada.”

Jitihada za Kutoa Msaada Zaimarisha Imani

Mafanikio ya jitihada za kutoa msaada licha ya changamoto yalichochea imani na ujasiri wa wale walioshiriki.

Kwa mfano, Ndugu Han alikuwa na wasiwasi ikiwa Halmashauri ya Kutoa Msaada itaweza kupata wajitoleaji wa kutosha ili kuanza kazi hiyo ndani ya saa 24. “Baada ya saa chache tu, nilitambua wasiwasi wangu haukuwa na msingi. Mamia ya ndugu na dada walijitolea kutoka sehemu zote nchini. Wengi sana walijitolea hivi kwamba tulihitaji kukataa maombi fulani. Nilihisi kwamba Yehova alikuwa pamoja nasi, na hilo lilinitia moyo sana.”

Ndugu Brad Benner

Vivyo hivyo, Ndugu Brad Benner, nchini Honduras anaeleza jinsi alivyohisi baada ya kutoa msaada wakati wa kimbunga: “Licha ya kwamba hali ilikuwa mbaya, ndugu na dada zetu wamepata chakula, makao, na kitia-moyo walichohitaji. Nimejionea mwenyewe kwamba hata vimbunga viwili vikiambatana pamoja na ugonjwa wa corona, haviwezi kuzuia upendo ulio katika tengenezo letu.”

Ndugu Alquin Dayag

Ndugu Alquin Dayag aliyetumikia katika Halmashauri ya Kutoa Msaada nchini Filipino anasema hivi: “Hali hii yote imenisaidia kutambua hata zaidi kwamba Yehova anatupatia kwa ukarimu nguvu zinazopita zile za kawaida na hekima tunayohitaji ili kufanya kazi tuliyopewa.”—2 Wakorintho 4:7.

Tunathamini kazi yote ngumu iliyofanywa za ofisi za tawi, Halmashauri za Kutoa Msaada, na ndugu na dada wengi waliojitolea katika kazi ya kutoa msaada. Kazi ngumu ya upendo na michango yenye ukarimu iliyotolewa ilisaidia kutoa msaada katika mwaka uliokuwa na misiba mingi zaidi katika historia.—1 Wathesalonike 1:3.