Hamia kwenye habari

Wahitimu wa Gileadi wakiwapungia mkono wahudhuriaji waliokuwa wakitazama programu hiyo

MACHI 20, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mahafali ya Kipekee ya Gileadi

Mahafali ya Kipekee ya Gileadi

Mahafali ya kuhitimu kwa darasa la 148 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower hayakuwa tofauti na mahafali mengine yaliyopita isipokuwa kwa jambo moja tu: hakukuwa na mhudhuriaji yoyote ukumbini. Wote waliohudhuria programu hiyo walisikiliza moja kwa moja kwa njia ya video. Katikati ya janga kubwa la kiafya la duniani kote, programu hii ya kiroho ni mfano wa hivi karibuni wa jinsi tengenezo la Yehova linavyobadilika kulingana na hali mbalimbali.

Programu hii ya mahafali ilifanyika Machi 14, 2020, katika kituo cha elimu kilichopo Patterson, New York. Ndugu Stephen Lett, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikuwa mwenyekiti wa programu hiyo. Jumla ya wanafunzi 55 walihitimu katika mahafali hayo. a

Majuma kadhaa kabla ya mahafali hayo, habari zinazohusu ugonjwa wa mapafu unaosababishwa na virusi vya corona (COVID-19), zilitapakaa katika vyombo vya habari duniani pote. Kama ilivyotajwa kwenye sehemu ya Habari ya jw.org, makao makuu ya duniani pote ya Mashahidi wa Yehova yalikuwa yakifuatilia kwa ukaribu hali hiyo na kutoa mwongozo kwa makutaniko yote kwa kutegemea mapendekezo yanayotolewa na wenye mamlaka.

Moja ya mapendekezo yaliyotolewa ni kudhibiti idadi ya watu wanaokusanyika pamoja. Kwa kuzingatia hili pamoja na mambo mengine, Baraza Linaloongoza lilitoa mwongozo kwamba wageni hawatahudhuria programu hiyo. Vilevile, hakungekuwa na wahudhuriaji wowote watakaokuwepo ukumbini. Familia ya Betheli pamoja na wanafunzi wote waliweka mfano mzuri wa kuunga mkono mwongozo huo.—Yohana 13:34, 35.

Hata hivyo, wageni wote wa wanafunzi wa Gileadi pamoja na familia ya Betheli, waliwezeshwa kutazama programu hiyo moja kwa moja kwa njia ya video. Hili liliwawezesha ndugu na dada zaidi ya 10,000 duniani pote, kutia ndani marafiki na familia ya wahitimu, kutazama programu hii moja kwa moja.

Baraza Linaloongoza lingependa kuona programu zote za kiroho, hususa ni mikutano ya kutaniko, zikiendelea kuwa sehemu ya kawaida ya ibada yetu licha ya ugonjwa uliosambaa duniani pote wa COVID-19. Kwa sababu hiyo, hivi karibuni Baraza Linaloongoza limetoa mwongozo hususa kwa ofisi za tawi ulimwenguni pote wa jinsi ya kubadili mikutano ya kutaniko kulingana na hali katika maeneo yao. Katika maeneo fulani, hili linatia ndani wahubiri kukutana katika vikundi vidogo au “kukutana” kwa njia ya kielektroni kama vile kwa njia ya video. Tuna hakika kwamba undugu wa ulimwenguni pote hautakosa chakula cha kiroho kutoka katika tengenezo la Yehova kwenda kwa makutaniko yote.

Ni wazi kwamba hakuna jambo lolote linaloweza kuzuia nguvu za Yehova kutusaidia, tukiwa kama tengenezo, kukabiliana na kizuizi chochote.—Zaburi 18:29.

a Programu nzima ya Mahafali ya Darasa la 148 la Shule ya Gileadi itapatikana katika tovuti ya jw.org, Juni 2020.