Hamia kwenye habari

Ndugu na dada wengi wakijitayarisha kuwakaribisha wajumbe wengi wa kimataifa waliofika katika mji wa Guadeloupe

JUNI 3, 2024
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Makusanyiko ya Pekee ya “Tangaza Habari Njema!” ya 2024 Yaanza Nchini Guadeloupe

Makusanyiko ya Pekee ya “Tangaza Habari Njema!” ya 2024 Yaanza Nchini Guadeloupe

Kusanyiko la Pekee la “Tangaza Habari Njema!” litafanyika kwa mara ya kwanza katika Vélodrome Amédée Détraux in Baie-Mahault, Guadeloupe, kuanzia Juni 7 hadi 9, 2024. Jumla ya makusanyiko ya pekee 15 yatafanywa kati ya Juni na Oktoba 2024. a Hii ndiyo mara ya kwanza kwa makusanyiko ya pekee kufanywa tangu yalipoahirishwa kwa sababu ya janga la COVID-19 mwaka wa 2020.

Ndugu na dada kutoka mataifa mbalimbali wamealikwa wakiwa wajumbe ili wahudhurie makusanyiko hayo ya pekee. Programu hizo zitafanywa katika lugha mbalimbali, na hilo litaongeza ladha ya matukio hayo ya kimataifa. Kwa mfano, nchini Guadeloupe, programu ya kusanyiko itaendeshwa wakati uleule katika Kifaransa, Kihispania, Kiingereza, na Kikrioli cha Guadeloupe.

Kushoto: Familia ikitengeneza kadi na ishara kwa ajili ya kuwakaribisha wajumbe kwenye kusanyiko. Kulia: Akina dada wakishona vitambaa vikiwa na nembo ya kusanyiko la pekee la Guadeloupe

Kazi nyingi inafanywa kabla ya wajumbe kutoka mataifa mbalimbali kuwasili. Kwa mfano, nchini Guadeloupe, zaidi ya nusu ya ndugu na dada 8,546 wanaotumikia katika eneo hilo walijitolea kusaidia kufanya matayarisho kwa ajili ya ndugu na dada 1,500 watakaosafiri kwenda huko kutoka nchi 11. Dada mmoja ambaye alijitolea pamoja na mume wake alisema hivi: “Huu umekuwa mwaka bora zaidi maishani mwangu! Nitaukumbuka maisha yangu yote. Kutumia wakati mwingi nikifanya kazi bega kwa bega pamoja na ndugu na dada zangu kunanisaidia kuelewa jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya. Kwa kweli ninajivunia kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova!”

Pamoja na undugu wetu wa ulimwenguni pote, tuna uhakika kwamba Makusanyiko ya Pekee ya “Tangaza Habari Njema!” ya 2024 yatawaunganisha zaidi watu wa Mungu na kumletea utukufu Baba yetu wa mbinguni, Yehova.​—Wafilipi 1:27.

a Makusanyiko ya pekee yatafanyika katika maeneo yafuatayo: Sofia, Bulgaria; Santiago, Chile #1; Santiago, Chile #2; Prague, Jamhuri ya Cheki; Santo Domingo, Jamhuri ya Dominika; Suva, Fiji; Helsinki, Finland; Lyon, Ufaransa; Baie-Mahault, Guadeloupe; Budapest, Hungaria; Reykjavík, Iceland; Asunción, Paraguai; Zurich, Uswisi; Philadelphia, Marekani; na Tampa, Marekani.