Hamia kwenye habari

NOVEMBA 4, 2019
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mashahidi wa Yehova Wafanya Maendeleo Makubwa Katika Kazi ya Kuhubiri—Sasa JW.ORG Ina Habari Katika Lugha 1,000

Mashahidi wa Yehova Wafanya Maendeleo Makubwa Katika Kazi ya Kuhubiri—Sasa JW.ORG Ina Habari Katika Lugha 1,000

Baraza Linaloongoza linafurahi kutangaza kwamba sasa tumefanya maendeleo makubwa katika jitihada zetu za kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. JW.ORG ina makala, video, na rekodi za sauti katika lugha 1,000, kutia ndani lugha 100 za ishara.

Agosti 2010, Ndugu Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, katika lugha ya Ishara ya Kiitaliano (inapatikana kwenye jw.org)

Ndugu Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza anasema hivi: “Kazi yetu ya kutafsiri ina historia ndefu tangu miaka ya 1800 na imeongezeka kwa kasi sana katika miaka ya hivi karibuni.” Ndugu Geoffrey Jackson, ambaye pia ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza anaongezea hivi: “Kufikia Januari 2013 tulikuwa tukitafsiri katika lugha 508, ilituchukua zaidi ya miaka mia moja kufikia hatua hiyo. Lakini inashangaza kwamba katika kipindi kisichozidi miaka saba, kazi ya kutafsiri imeongezeka maradafu—kutoka lugha 508 hadi lugha 1,000.”

Tovuti hiyo ina habari nyingi sana zinazoweza kupakuliwa katika lugha 1,000. Kati ya lugha hizi, ukurasa wa mwanzo wa jw.org na kurasa nyingine zinapatikana katika lugha 821, na hivyo kufanya iwe tovuti inayotafsiriwa kwa wingi zaidi ulimwenguni. Kazi nyingi ya kutafsiri hufanywa na wajitoleaji waliozoezwa vizuri katika ofisi 350 za utafsiri ulimwenguni pote.

“Kutafsiri na kuchapisha katika lugha nyingi kunatokeza changamoto,” anaeleza Ndugu Izak Marais, ambaye anasimamia Idara ya Utafsiri katika makao makuu huko Warwick, New York, nchini Marekani. “Wakati mwingine tulitaka kutafsiri lugha ambayo haizungumzwi na watu wengi, lakini lugha hiyo haikuwa na herufi zote. Basi, kwa miaka mingi, tumetokeza michoro ya maandishi na herufi, na hivyo kutuwezesha kuchapisha machapisho katika mamia ya lugha. Vivyo hivyo, tumeshinda changamoto nyingi ili kutokeza machapisho yetu katika lugha nyingi sana kwenye jw.org. Kwa kweli, nyingi kati ya lugha hizo 1,000 hazina machapisho mengine kwenye mtandao.”

Ndugu Clive Martin, ambaye anasimamia idara ya Programu ya MEPS anaongezea hivi: “Mojawapo ya changamoto ambazo tumekabili ni jinsi ya kutokeza makala moja katika mamia ya lugha, ikiwa na maandishi na mpangilio tofauti, katika tovuti ileile. Kwa mfano, lugha 21 kati ya lugha tunazotafsiri huandikwa kutokea kulia kwenda kushoto. Na kuhusu lugha 100 za ishara tunazotafsiri, tulilazimika kutokeza muundo wa pekee ambao ungekuwa rahisi kutumiwa na viziwi.”

Kwa kawaida, tovuti za kibiashara huelekeza jitihada zao hasa kwenye lugha zinazowaletea faida kubwa. Hata hivyo, lengo la Mashahidi wa Yehova si kupata faida. Lengo letu ni kutangaza ujumbe wa Biblia kwa wote wanaotamani kuusikia ujumbe huo katika lugha rahisi na inayoeleweka.

Tunamsifu na kumtukuza Yehova kwa kubariki jitihada zetu za moyo wote za kufanya “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” Tunaamini kwamba hadi Yehova atakaposema kazi hiyo imekwisha, ataendelea kutupatia nguvu na rasilimali tunazohitaji kuwatangazia ujumbe wa Ufalme watu wenye mioyo minyoofu ulimwenguni pote.—Mathayo 28:19, 20.