Hamia kwenye habari

Picha iliyopigwa kutoka juu wakati wa Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” kule Cleveland, Ohio, Marekani

AGOSTI 2, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Miaka 75 ya Kuadhimisha Kusanyiko Kubwa la Kwanza Kimataifa

Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” Liliweka Msingi kwa Ajili ya Makusanyiko ya Wakati Ujao

Miaka 75 ya Kuadhimisha Kusanyiko Kubwa la Kwanza Kimataifa

Agosti 4, 2021, utaadhimisha mwaka wa 75 tangu Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” (Mataifa Yenye Shangwe) lilipofanywa, kusanyiko kubwa la kwanza la kimataifa la Mashahidi wa Yehova. Kusanyiko hilo lilifanywa Agosti 4-11, 1946, kule Cleveland, Ohio, Marekani, katika Uwanja wa Michezo wa Manispaa na pia kwenye Ukumbi wa Manispaa ulio pembeni.

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, ndugu zetu walipanga kusanyiko ambalo lingekuwa tofauti kabisa na vita vya kijeshi vilivyokuwa vimeikumba dunia. Katika kusanyiko hilo, ndugu na dada kutoka ulimwenguni pote walikusanyika pamoja kwa amani. Watu wa rangi na malezi yote walichangamana kwa uhuru licha ya kwamba katika sehemu nyingi za Marekani wakati huo watu weusi na weupe hawakupaswa kuchangamana.

Kwa mara ya kwanza Mashahidi 80,000 walikutana mahali pamoja wakati wa kusanyiko hilo la “Mataifa Yenye Shangwe.” Baada ya kutenganishwa kwa muda kwa sababu ya vita, ndugu na dada zetu walifurahi sana kukutana pamoja. Kusanyiko hilo lilitia ndani wajumbe 302 kutoka nchi 32. Jumapili, iliyokuwa siku ya mwisho ya kusanyiko, Ndugu Nathan H. Knorr alitoa hotuba yenye kichwa “Mkuu wa Amani.”

Upande wa nje wa Uwanja wa Michezo wa Manispaa ukiwa na bango “Mkuu wa Amani,” hotuba ya watu wote iliyotolewa na Ndugu Knorr

Kusanyiko hilo lilifanikiwa, ingawa kulikuwa na changamoto. Siku ya kwanza ya kusanyiko, akina ndugu waliokuwa wakipanga mambo walikabili tatizo kubwa. Ukumbi wa Manispaa ulijaa watu waliohudhuria hivi kwamba hakukuwa na mahali pa kuketi. Akina ndugu walilazimika kutumia uwanja wa michezo ulikuwa pembeni ili watu wote waweze kuketi kwa ajili ya kipindi cha jioni kilichoanza saa 1:45 jioni. Lakini mechi mbili za mpira wa besiboli zilikuwa zimepangwa kuchezwa katika uwanja huo hadi saa 12:30 jioni.

Wakati wa mechi ya pili ya besiboli, mvua kubwa yenye radi kali iliwalazimisha mashabiki waondoke kwenye uwanja huo hata kabla ya mechi hiyo kwisha. Lakini baada tu ya hapo, dhoruba hiyo ilikwisha na Mashahidi 50,000 wakaingia kwenye uwanja huo wa michezo na kuanza kipindi cha jioni kwa wakati.

Ndugu Knorr akitoa kitabu “Mungu na Awe wa Kweli”

Kwenye kusanyiko hilo la “Mataifa Yenye Shangwe,” gazeti jipya lenye kichwa Amkeni! lilitolewa, pamoja na kitabu cha kujifunzia Biblia “Mungu na Awe wa Kweli.” Pia, Ndugu Knorr alitangaza mipango ya kupanua kiwanda cha uchapishaji kule Brooklyn, New York, Marekani, na ofisi za tawi katika nchi nyingine sita.

Sehemu yenye kufurahisha sana ilikuwa ubatizo uliofanywa katika Ziwa Erie lililokuwa karibu, na watu 2,602 walibatizwa—ndugu 903 na dada 1,699. Mambo mengine makuu yalikuwa maonyesho ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kutia ndani okestra ya wanamuziki 160.

Baadhi ya ndugu na dada zetu wakijiandaa kubatizwa

Kusanyiko hilo likawa kigezo cha makusanyiko ya wakati ujao. Kwa mfano, idara kadhaa za kusanyiko zilianzishwa, kama vile, Huduma ya Kwanza, Kujenga na Kubomoa, Ofisi ya Mwenyekiti, Ukaribishaji, na Vilivyopotea na Kupatikana.

Ndugu Ron Little, ambaye sasa ni mzee katika Kutaniko la McKeesport lililoko Pennsylvania, Marekani, alikuwa na umri wa miaka 11 alipohudhuria kusanyiko hilo pamoja na baba yake na ndugu yake. Wote watatu walilala katika gari la baba yake kwa siku nane za kusanyiko hilo.

Ndugu Little anakumbuka vizuri gazeti Amkeni! lilipotolewa. Anasema hivi: “Gazeti Amkeni! lilipotolewa, tulikimbia huku na huku tukiliinua. Sote tulikuwa tukijaribu kuhakikisha watu wote wanalipata.”

Ndugu Little, ambaye sasa ana umri wa miaka 86, anakumbuka pia jinsi alivyostaajabu kuwaona Mashahidi wengi sana wakiwa pamoja. Anasema: “Ninakumbuka nikijiambia sitaki kusanyiko hili liliishe. Lilipendeza sana.”

Tunamshukuru sana Yehova kwa baraka ya kuwa na “makusanyiko matakatifu.”—Mambo ya Walawi 23:2.

 

Programu ya Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” la Mashahidi wa Yehova lililofanyiwa Cleveland, Ohio, Marekani, kuanzia Agosti 4 hadi 11, 1946

Magari mawili yaliyo na vipaza sauti na mabango yanayosema “Soma Mnara wa Mlinzi na Consolation.” Bango kwenye mlango wa gari linatangaza hotuba ya watu wote “Mkuu wa Amani”

Wasichana wawili na mama yao wakiwa wamesimama mbele ya gari lenye vipaza sauti. Wasichana wameshika toleo la kwanza la gazeti Amkeni! lililotolewa kwenye Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” la 1946. Mama yao ameshika toleo la The Messenger, gazeti lililokuwa likichapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society

Ndugu akiwa na watoto wake wawili. Gari lao lina mabango yanayotangaza hotuba ya watu wote “Mkuu wa Amani”

Wajumbe wa kusanyiko wakiwa kwenye Kaunta ya Utumishi wa Shambani wakati wa Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” la 1946 wakipokea mabango ya kutangaza hotuba ya watu wote “Mkuu wa Amani”

Ndugu wakifanya kazi katika Idara ya Utumishi wa Chakula

Wahudhuriaji wa kusanyiko wakila kwenye kafeteria wakati wa Kusanyiko la Kitheokrasi la “Glad Nations” la 1946

Kikundi kikubwa cha wahudhuriaji wa kusanyiko wakiwa wameshika kitabu kipya kilichotolewa “Mungu na Awe wa Kweli”

Ndugu wakiwa nje ya eneo la kusanyiko, wengi wao walikuwa wamefungwa kwa sababu ya imani yao. Ndugu Daniel Sydlik (safu ya mbele, kulia kabisa), ambaye baadaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, yuko miongoni mwao

Wanaotaka kubatizwa wakiwa wameketi kwenye viti vya mbele

Picha iliyopigwa kutoka juu ya Ziwa Erie ambapo ubatizo ulifanyiwa