Hamia kwenye habari

Kusanyiko lililofanyika Columbus, Ohio, Marekani, Julai 24-30, 1931

JULAI 23, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Miaka 90 ya Kuitwa Mashahidi wa Yehova

Miaka 90 ya Kuitwa Mashahidi wa Yehova

Jumapili, Julai 26, 1931, Ndugu Joseph F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, alitoa hotuba mbele ya wasikilizaji zaidi ya 15,000 katika kusanyiko lililofanyika Columbus, Ohio, Marekani. Sehemu fulani za programu hiyo zilipeperushwa na zaidi ya vituo 450 vya redio ulimwenguni. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa programu ya redio kupeperushwa na vituo vingi hivyo ulimwenguni pote. Ndugu Rutherford alisoma azimio la kihistoria lenye kichwa “Jina Jipya.” Sentensi moja ilisema hivi: “Tunatamani kujulikana na kuitwa kwa jina, Mashahidi wa Yehova.” (Ona sanduku “ Azimio.”) Wasikilizaji walikubali azimio hilo kwa kusema “Ndiyo!” kwa sauti kubwa kisha wakapiga makofi kwa shangwe.

Ndugu Arthur Worsley, ambaye simulizi lake la maisha lilichapishwa 1986, alisema hivi kuhusu tukio hilo: “Sitawahi kusahau jinsi watu walivyoshangilia na kupiga makofi kwa sauti kubwa.”

Vikundi vya watu wakiwa nje ya uwanja wa Ohio State Fair Grounds wakati wa mapumziko

Wengine waliokuwa katika nchi nyingine walisikia azimio hilo likisomwa kupitia redio. Ndugu na Dada Barber walioishi Australia walisema hivi: “Tuliposikia ndugu walio Marekani wakishangilia na kupiga makofi, ndugu walio Melbourne walisimama na kuendelea kupiga makofi kwa shangwe.” Nchini Japani, kikundi kidogo, kilichotia ndani Dada Matsue Ishii, kiliweza kusikiliza azimio hilo likisomwa. Baadaye aliandika hivi: “Tulipaza sauti zetu kwa shangwe pamoja na ndugu zetu waliokuwa Marekani.”

Gazeti The Messenger, chapisho la kwanza kuwa na jina Mashahidi wa Yehova

Baadhi ya watu walisema kwamba katika mji ambao kusanyiko hilo lilifanyika, Columbus, Ohio, wafanyabiashara ambao walikuwa wameandika mabango ya kuwakaribisha Wanafunzi wa Biblia, waliamua kubadili maneno hayo na kuandika, “Karibuni, Mashahidi wa Yehova.” Julai 28,1931, katika gazeti ambalo lilichapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society, lililoitwa The Messenger, ambalo liliandika habari mbalimbali kuhusu makusanyiko yetu, lilichapisha habari hiyo na kutumia jina Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza.

Muda mfupi baada ya kusanyiko, kampeni kubwa ya kutoa kijitabu The Kingdom, the Hope of the World ilifanyika katika lugha nyingi. Kijitabu hicho kilitia ndani azimio hilo na pia jina letu jipya. Baada ya miezi miwili na nusu tu, zaidi ya nakala milioni tano zilisambazwa, nyingi zilisambazwa kwa viongozi wa serikali, wa dini, na pia wafanyabiashara.

Kijitabu The Kingdom, the Hope of the World katika lugha mbalimbali, kutia ndani maandishi ya vipofu. Chapisho hilo, lililotia ndani azimio lililokuwa na jina jipya, lilisambazwa katika kampeni ya ulimwenguni pote

Ndugu Martin Poetzinger alisema hivi kuhusu kipindi hicho: “Nyuso za watu zilibadilika kwa kuwa walishangaa tulipojitambulisha kwa kusema: ‘Nimekutembelea leo nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.’ Wengi wangetingisha kichwa au wangeuliza: ‘Lakini nyinyi bado ni Wanafunzi wa Biblia, sivyo?’” (Ona sanduku “ Kadi za Kutambulisha Jina la Yehova.”) Lakini miaka mingi baadaye, Ndugu Poetzinger aliandika hivi: “Hali imebadilika sana! Kabla hata ya kujitambulisha, watu wengi wananiambia: ‘Bila shaka wewe ni Shahidi wa Yehova.’”

Programu ya kusanyiko ilikuwa na herufi “JW,” ambazo maana yake ilielezwa katika hotuba ya Ndugu Rutherford

Ndugu A. H. Macmillan, ambaye pia alihudhuria kusanyiko la mwaka 1931, baadaye alielezea kwa nini jina hilo lilifaa sana. Alisema hivi: “Nilijiambia kwamba hilo ni wazo zuri sana, kwa sababu jina hilo lilijieleza lenyewe na dunia yote ingeweza kujua tunachofanya na kusudi letu ni nini. Hapo awali tuliitwa Wanafunzi wa Biblia. Kwa nini? Kwa sababu tulikuwa wanafunzi wa Biblia. Kisha, mataifa mengine yalipojiunga nasi, tukaitwa International Bible Students, yaani, Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa. Lakini sasa, sisi tunatoa ushahidi juu ya Yehova Mungu, na jina hilo linaeleza watu wote sisi ni nani na tunafanya nini.”

Leo, mamilioni ya watu ulimwenguni wanajivunia kuitwa kwa jina Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10-12.