Hamia kwenye habari

OKTOBA 11, 2019
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Muhtasari wa Mkutano wa Kila Mwaka wa 2019

Muhtasari wa Mkutano wa Kila Mwaka wa 2019

Jumamosi, Oktoba 5, 2019, shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania lilifanya mkutano rasmi wa kila mwaka kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Newburgh, New York, Marekani. Baada ya mkutano huo rasmi, washiriki wa Baraza Linaloongoza waliandaa programu ya kiroho iliyokuwa na wahudhuriaji 20,679, kutia ndani wale waliokuwa kwenye maeneo yaliyounganishwa. Ufuatao ni muhtasari wa kila sehemu. a

“Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”

Ndugu Gerrit Lösch, aliyekuwa mwenyekiti wa programu hiyo, alitoa hotuba ya kwanza ambayo ilitegemea andiko la Mathayo 23:10, linalotukumbusha kwamba Yesu Kristo ndiye kiongozi wetu na si mwanadamu yeyote.

Huduma Yetu ya Kutoa Msaada, Inatumiwa na Yehova Kutoa Kitulizo

Ndugu Stephen Lett alifafanua umuhimu wa kuwa watoaji wachangamfu. Njia moja ambayo tunaweza kuwa wakarimu ni kwa kuunga mkono huduma yetu ya kutoa msaada. Ndugu Lett alitoa muhtasari wa uharibifu uliosababishwa na misiba ya asili na kazi ya kutoa msaada tuliyofanya katika mwaka wa utumishi wa 2018 na 2019. Zaidi ya ndugu na dada 900,000 waliathiriwa na misiba hiyo; zaidi ya Majumba ya Ufalme 700 na nyumba 15,000 za ndugu zetu zilihitaji marekebisho au ziliharibika kabisa. Mashahidi wa Yehova walitumia dola milioni 49 na nusu za Marekani katika kazi ya kutoa msaada.

Sehemu hii ilitia ndani video zilizoonyesha shukrani zinazotoka moyoni za wahubiri waliofaidika kutokana na huduma yetu ya kutoa msaada.

‘Mkono Mwema wa Mungu Wetu Uko Juu Yetu . . . Twendeni Tukajenge’ | Video

Video hii ilieleza kwamba Mashahidi wa Yehova hutunza zaidi ya majengo 80,000 ulimwenguni pote. Pia, ilikazia mbinu tunazotumia katika kudumisha, kurekebisha, na kujenga majengo ya kitheokrasi.

Historia ya Kununua Viwanja na Majengo | Video

Video hii ilitia ndani mahojiano yaliyohifadhiwa ya ndugu watatu waliosaidia zamani kuchagua na kununua viwanja na majengo kwa ajili ya ofisi ya tawi ya Marekani na makao makuu: Ndugu  Max Larson, George Couch, na Gilbert Nazaroff. Ndugu hao watatu walisimulia jinsi walivyoona waziwazi mkono wa Yehova katika ununuzi wa viwanja na majengo mbalimbali.

Mradi Mpya wa Ujenzi Unatayarishwa | Video

Video hii ilikuwa na tangazo lililosema kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanya mpango wa kuunganisha kazi ya kurekodi video na sauti ili ifanywe katika sehemu moja itakayojengwa huko Ramapo, New York. Sehemu hiyo iko kilomita 3 kutoka makao makuu yaliyo Warwick, New York. Lengo ni kuanza ujenzi mwaka wa 2022 na kuukamilisha kufikia Desemba 2026. Ujenzi huo utakaposhika kasi, inakadiriwa kwamba mradi huo utahitaji wajitoleaji 1,500 kwa siku.

Mchoro wa Betheli mpya itakayojengwa huko Ramapo, New York. Ramani inatia ndani sehemu ya studio, ofisi, makazi, na sehemu ya wageni

Programu Mpya ya Kupokea Maombi | Video

Video hii ilieleza kwamba kuanzia Januari 2020, wahubiri ambao wangependa kupanua huduma yao wataweza kujaza maombi yao kwenye jw.org na kuyawasilisha kwa baraza lao la wazee ili wayapitie.

Njia Mpya ya Kupata Sauti Kwenye JW.ORG

Sasa unaweza kutumia programu za Amazon Alexa au Google Assistant kupata makala zenye sauti kwenye jw.org.

Shambulizi Kutoka Kaskazini

Ndugu David Splane alifafanua upya uelewaji wetu wa unabii ulio kwenye Yoeli sura ya 2 na kufafanua kundi la nzige. Tunatazamia kwa hamu kujifunza kuhusu uelewaji huo mpya utakapochapishwa katika Mnara wa Mlinzi.

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya (Toleo la Funzo) linaloanzia Mathayo hadi Matendo

Jifunze Biblia kwa Kutumia Biblia ya Kujifunzia

Ndugu Samuel Herd alikazia faida za Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya (Toleo la Funzo) ambayo inapatikana mtandaoni katika Kiingereza. Kisha akatangaza kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya (Toleo la Funzo) iliyochapishwa yenye vitabu vya Mathayo hadi Matendo. Wahubiri wanaweza kuomba nakala kupitia makutaniko yao.

Tuna Kazi ya Kufanya!

Ndugu Anthony Morris alikazia kwamba Wakristo wa kweli wanaona kazi ya kuhubiri habari njema kuwa mgawo muhimu sana. Majengo ya kitheokrasi husaidia Baraza Linaloongoza kupanga kazi ya kuhubiri na kuwaandalia watu wa Yehova chakula cha kiroho. Ndugu Morris alinukuu maneno yenye kuchochea yaliyokuwa kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1976: “Wakati ‘dhiki kuu’ itakapotokea, kazi ya kuhubiri inapaswa kuwa ikisonga mbele kwa kasi ya juu zaidi, duniani kote. Bwana Yesu atakuja kutekeleza hukumu wakati usiotarajiwa—hata kwa watu wa Yehova, lakini bila shaka tukio hilo litawakuta wakiendelea na bidii zaidi katika kazi yao!”

Tunapaswa Kuogopa Nini?

Ndugu Mark Sanderson alifafanua kwamba, kama Yesu alivyotabiri, watu wa Mungu wanatarajia kuchukiwa na “mataifa yote.” (Mathayo 24:9) Hata hivyo, Ndugu Sanderson alitutia moyo tusiwaogope wanadamu, bali tumwogope Yehova.—Zaburi 111:10.

Video yenye kugusa moyo ilionyeshwa kuhusu akina ndugu na dada wanaoteseka nchini Urusi wakieleza jinsi wanavyoshinda woga wa kuteswa. Hotuba hii na video iliwatia moyo watu wote wa Yehova wasitawishe roho hiyohiyo.

Je, Una Akili Timamu Kabisa?

Ndugu Geoffrey Jackson alionyesha waziwazi matumizi ya mistari iliyo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambayo inatumia maneno ambayo kihalisi yanamaanisha “akili timamu.” Vilevile alikazia umuhimu wa kuendelea ‘kutunza akili zetu kikamili’ (kihalisi “kuwa na akili timamu kikamilifu”) katika siku hizi za mwisho.—1 Petro 1:13.

Je, Utatimiza Mgawo Huu?

Ndugu Kenneth Cook alitangaza andiko la mwaka wa 2020, Mathayo 28:19: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi . . . , mkiwabatiza.” Alikazia uhitaji wa kuwasaidia watu wenye mioyo inayofaa wajiweke wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

Programu za kiroho kama mkutano huu wa mwaka hutuchochea tuendelee kuongeza bidii katika utumishi wetu kwa Yehova.

a Programu nzima ya mkutano wa kila mwaka itawekwa kwenye jw.org mwezi wa Januari 2020.