Hamia kwenye habari

Washiriki wa Baraza Linaloongoza wakitoa hotuba ya Ukumbusho: (kushoto) Ndugu Anthony Morris akitoa hotuba iliyoonyeshwa kwa familia ya Betheli; (juu kulia) Ndugu Geoffrey Jackson na (chini kulia) Ndugu Mark Sanderson wakitoa hotuba kwa ajili ya makutaniko kwa njia ya video wakiwa katika vyumba vyao

APRILI 10, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mwadhimisho wa Ukumbusho wa 2020—Betheli ya Marekani

Mwadhimisho wa Ukumbusho wa 2020—Betheli ya Marekani

Aprili 7, 2020, licha ya ugonjwa wa virusi vya corona, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote waliadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Kama Ndugu Stephen Lett mshiriki wa Baraza Linaloongoza alivyosema: “Hakuna kirusi wala ugonjwa wowote duniani unaoweza kupunguza uthamini wetu kuelekea mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia au kulegeza azimio letu la kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana.” Maneno hayo yalitimizwaje mwaka huu?

Hii ni sehemu ya kwanza katika mfululizo wa makala katika kitengo cha Habari zitakazoonyesha jinsi ndugu zetu ulimwenguni pote walivyoadhimisha Ukumbusho katika kipindi hiki cha mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya corona. Katika makala hii ya kwanza tutaona jinsi Ukumbusho ulivyofanywa katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova na katika ofisi ya tawi ya Marekani.

Ili kutii amri ya serikali inayokataza mikusanyiko, Baraza Linaloongoza liliamua kwamba kungekuwa na programu moja ya Ukumbusho ambayo ingesikilizwa na wanabetheli wote. Ndugu Anthony Morris alitoa hotuba hiyo katika ukumbi wa Warwick. Washiriki wote wa familia ya Betheli ya Marekani walipata nafasi ya kutazama programu hiyo wakiwa vyumbani mwao. Ingawa kuna idadi ndogo ya wale wanaokula mkate na kunywa divai, Ofisi ya Betheli iliandaa mifano ya ukumbusho kwa ajili ya wote katika familia.

Mifano ya Ukumbusho iliyotayarishwa kwa ajili ya familia ya Betheli

Pia, wanabetheli walikuwa na nafasi ya kuunganishwa kupitia Intaneti na hivyo kuhudhuria programu hiyo pamoja na makutaniko yao. Vilevile, wanabetheli ambao ni wazee wa makutaniko walipewa nafasi ya kutoa hotuba ya Ukumbusho kupitia Intaneti.

Wenzi wa ndoa wanaotumika katika Betheli ya Wallkill wakifanya Ukumbusho katika chumba chao cha Betheli

Washiriki wengi wa familia hii ya Betheli walisema kwamba mwadhimisho huo wa Ukumbusho ulikuwa wa kipekee zaidi kuliko miadhimisho mingine yote ambayo wamewahi kuhudhuria. Ingawa hawakuwa kihalisi pamoja na waabudu wenzao, walihisi wameunganishwa na ndugu na dada zao ulimwenguni pote katika kukumbuka wonyesho mkubwa zaidi wa upendo ulioonyeshwa na Mungu wetu, Yehova, na mwana wake mpendwa, Yesu Kristo.—Yohana 3:16; Mathayo 20:28.