Hamia kwenye habari

APRILI 21, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Mwadhimisho wa Ukumbusho wa 2020—JW.ORG

Watu Wengi Zaidi Watembelea Tovuti Yetu Rasmi

Mwadhimisho wa Ukumbusho wa 2020—JW.ORG

Kadiri ugonjwa wa virusi vya corona unavyozidi kuenea ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova wanaongeza utendaji wao wakati wa majira haya ya ukumbusho, idadi kubwa zaidi ya watu wanatembelea tovuti yetu ya jw.org ili kupata faraja ya kiroho, habari za Kimaandiko, na habari. Katika mwezi wa Machi, idadi ya watu waliotembelea tovuti hiyo iliongezeka kwa asilimia 50 zaidi ya mwezi uliotangulia na maombi ya watu wanaotaka kujifunza Biblia ilifikia kilele kipya.

Ugonjwa huo ulipoanza, watu wengi zaidi walianza kutembelea tovuti ya jw.org. Mwezi wa Februari, watu milioni mbili hivi waliitembelea kila siku, jambo la kawaida kwa tovuti hiyo. Mwezi wa Machi, idadi hiyo iliongezeka kufikia zaidi ya watu milioni tatu kwa siku. Lakini siku ambazo kulikuwa taarifa za pekee za habari kuhusiana na ugonjwa wa corona, idadi hiyo ilifikia zaidi ya watu milioni nne na nusu. Aprili 7, siku ya Ukumbusho wa 2020, kulikuwa na watu milioni 7 hivi waliotembelea tovuti hiyo, na wengi wao walifanya hivyo ili kutazama programu ya pekee ya ibada ya asubuhi na hotuba ya Ukumbusho.

Idadi ya waliotembelea jw.org imeongezeka sana wakati wa ugonjwa huu, siku ya ukumbusho ikiwa na idadi kubwa zaidi ya zaidi ya milioni saba

Ndugu Clive Martin, anayesimamia Idara ya MEPS Programming kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova yaliyoko Warwick, New York anaeleza hivi: “Wakati huu wa mwaka watu wengi hutembelea jw.org ili kufahamu mahali na wakati wa kuhudhuria Ukumbusho. Lakini mwaka huu, kwa kuwa watu wengi wanaopendezwa wasingeweza kuhudhuria kwenye makutaniko ya eneo lao, tuliweka hotuba ya pekee ya 2020 na hotuba ya Ukumbusho kwenye jw.org katika zaidi ya lugha 500. Mamilioni ya watu walipakua au kutazama programu hizo. Idadi kubwa ya watu waliotembelea tovuti hiyo wakati wa kipindi hiki cha hali ngumu ulimwenguni inaonyesha kwamba jw.org inatimiza sehemu muhimu katika kuandaa mwongozo wa kiroho na faraja kwa watu wengi katika jamii mbali na Mashahidi wa Yehova.”

Idadi ya watu waliopakua hotuba ya pekee (rangi ya chungwa) na idadi ya waliopakua hotuba ya Ukumbusho (bluu)

Si ajabu kwamba watu wengi waliotembelea tovuti hiyo walikuwa wakitafuta habari kuhusu afya na kuzuia magonjwa, kutia ndani habari zinazohusiana na mkazo na kuhangaika. Pia imeonekana kwamba watu wengi walitembelea tovuti hiyo ili kutafuta habari ya Kimaandiko inayohusiana na ishara ya siku za mwisho na wale wapanda-farasi wanne wa Ufunuo sura ya 6.

Jambo muhimu kuhusu utendaji ulioongezeka kwenye tovuti hiyo ni idadi ya watu wanaoomba kujifunza Biblia. Kwa kawaida wastani wa watu 250 huomba kila siku. Katika mwezi wa Machi, maombi yaliongezeka kwa asilimia 40. Watu 350 hivi kila siku au 11,000 kwa mwezi walituma maombi. Katika muda wa saa 48 za siku ya Ukumbusho na siku iliyofuata, zaidi ya maombi 1,000 ya kuomba funzo la Biblia mtandaoni yalipokewa.

Yesu alisema kwamba watu wanaotambua uhitaji wao wa kiroho watakuwa na furaha. (Mathayo 5:3) Tunafurahi kwamba watu wengi sana wanamtafuta Yehova na tengenezo lake ili kupata faraja na utegemezo wa kiroho katika nyakati hizi ngumu.—2 Wakorintho 1:3, 4.