Hamia kwenye habari

Ndugu Aleksandr Ursu

DESEMBA 4, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Ndugu Aleksandr Ursu Mwenye Umri wa Miaka 80 Anazungumza Kuhusu Mambo Aliyovumilia Maishani

Ndugu Aleksandr Ursu Mwenye Umri wa Miaka 80 Anazungumza Kuhusu Mambo Aliyovumilia Maishani

“Yehova alitutunza wakati huo, na ninajua ataendelea kututunza.”

Jioni ya Novemba 15, 2018, Ndugu Aleksandr Ursu, alitoka nje ya nyumba yake huko Dzhankoy, Crimea, kumsalimu mwana wake, Viktor. Wakati huo Ndugu Aleksandr alikuwa na umri wa miaka 78. Alishtuka kuona taa nje ya lango. Alisogea kwa tahadhari kuelekea taa hiyo. Ghafla akasikia mtu akisema kwa sauti kubwa: “Simama! Polisi!”

Aleksandr alifikiri ni akina ndugu waliokuwa wakifanya utani, lakini upesi aligundua haikuwa hivyo. Mwanamume aliyefunika uso alishika mikono ya Aleksandr na kuikunja mgongoni kwa uchungu. Mwanamume mwingine aliyefunika uso alimpiga Aleksandr ngumi kwenye taya. Maofisa sita wa Idara ya Usalama wa Taifa (FSB) waliokuwa na bunduki za kumimina risasi waliwapekua Aleksandr na Viktor kabla ya kuvamia nyumba yake.

Mke wa Aleksandr, Nina, alikuwa jikoni maofisa hao walipovamia. Ofisa mmoja alimnyang’anya kifaa chake cha kielektroni na kumuuliza alikuwa akitazama nini. Maofisa hao walipekua nyumba yote kwa saa kadhaa lakini hawakupata chapisho lolote lililokuwa kwenye orodha ya Urusi ya habari zenye msimamo mkali.

Ndugu Aleksandr Ursu na mke wake, Nina, mnamo 2020

Ndugu yetu Aleksandr, mwenye umri mkubwa hakukamatwa. Hata hivyo, Aleksandr na Mashahidi wengine wote nchini Urusi na Crimea wanaishi kila siku wakijua kwamba polisi wanaweza kuvamia nyumba zao na kuwakamata wakati wowote ule. Ili kukabiliana na ukweli huo, Aleksandr hutafakari kuhusu mifano mizuri ya watu waaminifu katika familia yake na mambo ambayo alivumilia chini ya utawala wa Sovieti.

Julai 6, 1949, Aleksandr alipokuwa na umri wa miaka tisa, maofisa wa Sovieti walivamia nyumba yao usiku kwa nguvu na kuipekua. Walitupa vitu vya familia yao sakafuni na kuwaambia waanze kufunga mizigo. Aleksandr anakumbuka hivi: “Mama alificha machapisho ya Biblia kati ya mizigo yetu, kutia ndani kitabu The Harp of God wakati ambapo askari hawakuwa wakiangalia.” Maofisa hao waliipeleka familia yote kwenye kituo cha gari-moshi.

Kwa ujasiri, familia ya akina Aleksandr, pamoja na Mashahidi wengine kwenye treni yao, waliimba nyimbo za Ufalme walipokuwa wakipelekwa Siberia, eneo ambalo lingekuwa makao yao mapya. Walikuwa kati ya maelfu ya ndugu na dada waliopelekwa uhamishoni Siberia kati ya mwaka 1949 na 1951.

Huko Siberia, katika miaka ya 1950, akina ndugu walikuwa wakikutana kwa siri kwenye mashamba ili kufanya mikutano. Familia fulani zilitembea umbali wa kilomita 20 ili kufika kwenye mikutano.

Aleksandr alinufaika kutokana na mifano mizuri ya watu wa familia yake waliokuwa waaminifu. Baba ya babu yake, Makar; babu yake Maksim; ndugu ya babu yake, Vladimir; na baba yake, Pyotr, wote ni mifano bora ya watu waliovumilia kwa ushikamanifu.

Picha iliyo kushoto, kuanzia kushoto kwenda kulia: Ndugu Aleksandr Ursu akiwa amemshika mwana wake Viktor; mke wake, Nina; mama yake, Nadezhda; baba yake, Pyotr, akiwa amemshika Dina (binti ya Aleksandr). Picha ya kulia: Ndugu Vladimir Ursu, ndugu ya babu ya Aleksandr, Maksim. Vladimir na Maksim walikuwa waaminifu walipokufa wakiwa gerezani

Baba ya Aleksandr alihukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani kwa kukataa utumishi wa kijeshi mnamo 1944. Alirudi nyumbani baada ya miaka mitatu akiwa amepooza kwa sababu ya kuvunjika uti wa mgongo. Aleksandr anakumbuka baba yake akimsimulia hadithi za Biblia kumhusu Daudi, Goliathi, na urafiki kati ya Daudi na Yonathani.

Aleksandr anakumbuka hivi: “Mjomba wangu Vladimir alisikiliza WBBR na kupokea machapisho ya Biblia. Wakati huo ilikuwa kinyume cha sheria kuwa na redio, kwa hiyo, mjomba wangu alitengeneza chumba fulani chini ya ardhi ambapo yeye na watu wanaopendezwa wangesikiliza matangazo ya kituo cha WBBR wakiwa salama.”

Katika miaka hiyo ya 1940, mtu fulani aliyejifanya kuwa anapendezwa aliwaambia maofisa mahali ambapo chumba hicho kilikuwa. Mjomba wa Aleksandr pamoja na babu yake walikamatwa na kufungwa huko Khotyn, magharibi mwa Ukrainia, kilomita 80 hivi kutoka kijijini kwao.

“Nyanya yangu alitembea umbali huo kwenda kuwatembelea gerezani. Alituambia imani yao ilikuwa ikiwasaidia kudumisha uchangamfu, hata hivyo, angeweza kutambua kuwa walikuwa wakipigwa.” Kwa kusikitisha, mjomba wa Aleksandr na babu yake walifia gerezani.

Aleksandr anasema: “Hatujui kilichowapata, jinsi walivyotendewa, jinsi walivyokufa, na mahali walipozikwa. Lakini tunatiwa moyo kujua kwamba waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova hadi kifo.”

Mfano huo mzuri wa watu wa familia yake na pia mambo ambayo yeye alijionea huko Siberia, yalimtayarisha Aleksandr kwa ajili ya mateso anayokabili leo. Anasema hivi: “Nimezoea upekuzi unaoendelea kwa sababu nimeuona tangu nilipokuwa mtoto. Yehova alitutunza wakati huo, na ninajua ataendelea kututunza.”

Aleksandr anaeleza hivi: “Mambo mengine yanayonitegemeza ni kujifunza Biblia kila siku na kutafakari, kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na kuwasiliana na ndugu na dada.”

Pia, yeye husoma kwa ukawaida majaribu ambayo ndugu na dada wengine wanakabili na ujasiri wao unamwimarisha. Anasema hivi: “Mimi husoma mambo ambayo baadhi ya ndugu walisema mahakamani katika maelezo yao ya kumalizia. Maneno yao yenye ujasiri hutimiza maneno ya Yesu ya kinabii: ‘Mtapelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.’”—Mathayo 10:18.

Ndugu na dada zetu huvumilia na kuendelea kuwa imara licha ya mateso, kwa msaada wenye upendo wa Mungu wetu, Yehova. Wao ni ushahidi ulio wazi wa ukweli wa maneno haya ya Daudi yaliyoongozwa na roho: “Wale wote wanaokukimbilia [Yehova] watashangilia; watapaza sauti kwa shangwe daima.”—Zaburi 5:11.