Hamia kwenye habari

APRILI 30, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Ndugu na Dada Ulimwenguni Pote Wawafariji Walioathiriwa na Ugonjwa wa Corona

Ndugu na Dada Ulimwenguni Pote Wawafariji Walioathiriwa na Ugonjwa wa Corona

Ingawa watu wa Yehova wamechukua tahadhari za kujikinga na ugonjwa huu, baadhi ya ndugu na dada zetu wamekufa kutokana nao. (Mhubiri 9:11) Inasikitisha kwamba kufikia sasa, ndugu na dada 872 ulimwenguni pote wamekufa kutokana na ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19). Waabudu wenzetu watenda kwa haraka kuwategemeza na kuwafariji wanaoomboleza. (1 Wakorintho 12:26) Jambo muhimu zaidi ni kwamba ndugu na dada zetu wanamtegemea Yehova, ambaye sikuzote hutenda kupatana na ahadi yake iliyo kwenye Wafilipi 4:7 kwa kutupatia “amani ya Mungu.”

Ndugu na Dada Unnützer

Dada Hannchen Unnützer, painia wa pekee katika jiji la Bolzano, kaskazini mwa Italia, ni mmoja kati ya wale wanaotegemezwa na tengenezo la Yehova. Kwa kusikitisha, Machi 28, 2020, mume wake Ndugu Manfred Unnützer alikufa kutokana na ugonjwa wa virusi vya corona. Ndugu Unnützer alitumikia katika utumishi wa wakati wote wa pekee kwa karibu miaka 58, na mke wake alitumikia pamoja naye kwa karibu miaka 54. Alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko kwa miaka 25 hivi. Ndugu na dada 1,000 hivi kutoka nchi kadhaa waliunganishwa kwenye hotuba ya mazishi kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao.

Dada Unnützer anasema hivi: “Ninawashukuru sana akina ndugu na dada. Hawakuniacha peke yangu, hata kwa saa moja. Nilihisi kwamba wananipenda sana. Walinitunza kihisia, kiroho, na kimwili. Ninawapenda ndugu zangu.”

Maria Jose Moncada na mume wake Darwin wanafarijiwa pia katika kipindi hiki wanapoomboleza. Wanatumikia katika eneo la lugha ya Kikwichua nchini Ekuado. Kwa kusikitisha, wazazi wa Dada Moncada—Dada Fabiola Santana Jordan, aliyekuwa na umri wa miaka 56, na aliyekuwa painia wa kawaida, na Ndugu Ricardo Jordan, aliyekuwa na umri wa miaka 60, aliyetumikia akiwa mtumishi wa huduma katika Kutaniko la Praderas katika jiji la Guayaquil—walikufa kutokana na ugonjwa huo. Vifo vyao vilipishana kwa siku sita tu. Pia, ndugu wawili wa Dada Moncada waliambukizwa ugonjwa huo wa virusi vya corona lakini walipona.

Ndugu na Dada Moncada wakiadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana

Akiwa ana huzuni nyingi, Dada Moncada alitaka kufunga safari hiyo ya saa nne ili kuwa pamoja na familia yake na kuwafariji na kuwasaidia katika mipango ya mazishi. Hata hivyo, kupitia sala waliamua kwamba si jambo la hekima kusafiri kwenda Guayaquil. Badala yake, waliwasiliana na watu wa ukoo kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao. Dada Moncada anaeleza: “Ikiwa tungeenda kuwa pamoja na watu wa familia, tungehatarisha afya yetu na ya wengine.”

Inaeleweka kwa nini Dada Moncada anasema alikuwa na “uchungu na wasiwasi” mwingi, lakini yeye na mume wake waliendelea kudumisha ratiba nzuri ya kiroho na ‘walisali kwa Yehova bila kuacha, wakimwomba mwongozo.’ Ndugu na dada Moncada waliendelea kufanya matayarisho kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu kwa kuwaalika wanafunzi wa Biblia na kusoma masimulizi kuhusu siku za mwisho za Yesu duniani. Pia waliendelea kushiriki katika huduma kwa kuandika barua na kuhudhuria mikutano ya kutaniko lao kupitia video iliyounganishwa kwenye Intaneti. Tisa kati ya watu wa ukoo wa Dada Moncada ambao si Mashahidi, walikubali mwaliko wake wa kuunganishwa kwenye Ukumbusho katika Kihispania kupitia video.

Dada Moncada anasema hivi: “Tulitiwa moyo sana kuona wanafunzi wa Biblia wakiunganishwa kwenye mikutano, ingawa si rahisi kufanya hivyo. Tulifurahi sana pia kuona washiriki wengine wa familia yetu wakiunganishwa ingawa wanaishi katika nchi nyingine.”

Dada Moncada anaendelea kusema hivi: “Jambo hili linatuonyesha kwamba ingawa hali zetu zinaweza kuwa zenye kuhuzunisha sana, kudumisha ratiba nzuri ya kiroho ndiyo njia bora zaidi ya kukabiliana na huzuni, kwa kuwa tunampa Yehova kitu cha kubariki.”

Ndugu na dada ulimwenguni pote wanaomboleza na wale ambao wamewapoteza wapendwa wao katika kifo kutokana na ugonjwa huu wa corona, na tutaendelea kusali kwa ajili yao. Tunatarajia wakati ujao kwa hamu ambapo Yehova ataondoa mambo yote yanayotuletea maumivu, kama vile, magonjwa, na kuwafufua watumishi wake waaminifu ambao wamekufa.—1 Wakorintho 15:21, 22.