Hamia kwenye habari

JULAI 8, 2022
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Rekodi Mpya ya Utafsiri Yafikiwa Baada ya Biblia 13 Kutolewa Katika Mwisho-juma Mmoja

Rekodi Mpya ya Utafsiri Yafikiwa Baada ya Biblia 13 Kutolewa Katika Mwisho-juma Mmoja

Katika mwisho juma wa Juni 25-26, 2022, jitihada zetu za utafsiri zilifikia kilele kipya baada ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kutolewa katika lugha 13. Kabla ya hapo idadi kubwa zaidi ya Biblia zilizotolewa katika mwisho juma mmoja ilikuwa sita. Ripoti ifuatayo inaeleza kile kilichotokea katika siku hiyo muhimu.

Lugha ya Tzeltal

Ndugu Armando Ochoa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Tzeltal. Programu hiyo ilipeperushwa kupitia mtandao, kwa watazamaji 1,400 hivi. Biblia ilitolewa katika mfumo wa kielektroni na nakala zilizochapishwa zinapatikana pia.

Mtafsiri mmoja wa lugha ya Tzeltal alisema hivi: “Ninapofikiria kuhusu mradi huu, ni wazi kwamba Yehova ametusaidia sana. Hata siamini kwamba mradi huu umekamilika. Tunajua kwamba iliwezekana tu kwa sababu ya msaada wa Yehova kupitia roho yake takatifu.”

Lugha ya Wayuunaiki

Ndugu Carlos Moreno, mwakilishi kutoka Halmashauri ya Tawi ya Kolombia, alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (Kitabu cha Mathayo hadi kitabu cha Matendo) katika lugha ya Wayuunaiki. Programu iliyorekodiwa mapema ilipeperushwa na kutazamwa na wahudhuriaji 2,000 hivi nchini Kolombia na Venezuela. Biblia hii ilitolewa katika mfumo wa kielektroni. Nakala zilizochapishwa zitapatikana baadaye.

Lugha ya Baoule

Ndugu Christophe Coulot, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Côte d’Ivoire, alitangaza kutolewa kwa toleo zima la Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Baoule kupitia programu iliyorekodiwa mapema, na kupeperushwa kwa zaidi ya watazamaji 12,000. Biblia hiyo ilitolewa katika mfumo wa kielektroni. Nakala zilizochapishwa zitapatikana mwezi wa Oktoba 2022. Hii, ni mara ya kwanza kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kutafsiriwa katika lugha ya asili kwenye eneo la ofisi ya tawi ya Côte d’Ivoire.

Mtafsiri mmoja anaeleza kilichowachochea walipokuwa wakifanya kazi hiyo: “Tulipokabili changamoto yoyote, tulifikiria kuhusu shangwe ambayo ndugu na dada na watu wengine katika eneo letu wangekuwa nayo kwa sababu ya kupata Biblia katika lugha yao wenyewe. Jambo hilo na pia, msaada wa Yehova, ulitupatia nguvu za kusonga mbele.”

Lugha ya Welsh

Ndugu Peter Bell, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Uingereza, alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Welsh kupitia programu iliyofanyika kwenye Jumba la Ufalme huko Wales. Wahudhuriaji 2,057, kutoka Wales na Argentina waliunganishwa kwenye programu hiyo kupitia mtandao. Biblia hiyo ilitolewa katika mfumo wa kielektroni. Nakala zilizochapishwa zitapatikana Desemba 2022.

Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Sitasahau kamwe, tulipotafsiri jina la Yehova kwa mara ya kwanza. Tulihisi ni pendeleo kubwa sana kuona jina la Mungu likirudishwa mahali ambapo linapaswa kuwa.”

Lugha ya Manyawa na Lugha ya Tewe

Ndugu Marcelo Santos, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Msumbiji, alitangaza kutolewa kwa Biblia—Kitabu cha Mathayo katika lugha ya Manyawa na lugha ya Tewe kupitia programu mbili zilizorekodiwa mapema. Programu hizo zilipatikana kupitia JW Stream. Pia, zilirushwa kupitia vituo vya redio na televisheni. Vitabu hivyo vilitolewa katika mfumo wa sauti na wa kielektroni. Nakala zilizochapishwa zitapatikana mwezi wa Septemba 2022.

Hiki ni kitabu cha kwanza cha Biblia kutafsiriwa katika lugha ya Manyawa, na ni vitabu vichache tu vya Biblia vilivyotafsiriwa katika lugha ya Tewe. Wasomaji na wasikilizaji watanufaika sana kwa kutumia toleo hili.

Lugha ya Quechua (Ancash), ya Quechua (Ayacucho), na ya Quechua (Cuzco)

Ndugu Marcelo Moyano, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Peru, alitangaza kutolewa kwa toleo la kielektroni la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Quechua (Ancash), lugha ya Quechua (Ayacucho), na lugha ya Quechua (Cuzco). Hizo ni lugha tatu kuu za Quechua zinazozungumzwa nchini Peru. Programu iliyorekodiwa mapema ilipeperushwa na kutazamwa na zaidi ya watu 7,000. Nakala zilizochapishwa zitapatikana mwezi wa Oktoba 2022.

Ingawa asili ya lugha za Quechua ni moja, lugha hizo zina lahaja mbalimbali ikitegemea eneo, na kwa sababu hiyo wazungumzaji wanahitaji tafsiri ya Biblia ya Kiquechua kinachozungumzwa katika eneo lao ili kuelewa vizuri. Kikundi cha watafsiri wa kila lahaja walichagua kwa uangalifu maneno ambayo wasomaji wa asili katika eneo lao wanatumia na kuelewa kwa urahisi.

Lugha ya Ndebele, lugha ya Sesotho (ya Lesotho), na lugha ya Sesotho (ya Afrika Kusini)

Ndugu Kenneth Cook, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Ndebele na lugha ya Sesotho (ya Afrika Kusini). Pia, alitangaza kutolewa kwa toleo lililorekebishwa la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Sesotho (ya Lesotho). Zaidi ya watu 28,000 walitazama programu hiyo iliyorekodiwa mapema, na kupeperushwa katika baadhi ya Majumba ya Ufalme na nyumba za akina ndugu kote nchini Afrika Kusini. Biblia hiyo ilitolewa katika mfumo wa kielektroni, na nakala zilizochapishwa zitapatikana mwezi Desemba 2022. Hii ni mara ya kwanza kwa Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kutafsiriwa katika lugha ya Ndebele na lugha ya Sesotho (ya Afrika Kusini).

Mtafsiri mmoja wa lugha ya Ndebele, alisema hivi: “Tafsiri hii kwa kweli ni baraka kwa watu wanaozungumza lugha ya Ndebele, kwa sababu inatumia jina Yehova. Kwa mara ya kwanza, sasa wataweza kulijua jina hilo kwa kulisoma moja kwa moja kwenye Biblia zao.”

Lugha ya Ndebele (Zimbabwe)

Ndugu Shingirai Mapfumo, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zimbabwe, alitangaza kutolewa kwa Biblia nzima Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha ya Ndebele nchini Zimbabwe, katika mfumo wa kielektroni. Nakala zilizochapishwa zitapatikana mwezi Julai 2022. Programu hiyo iliyorekodiwa mapema ilipeperushwa kote nchini Zimbabwe kwenye Majumba ya Ufalme na kutazamwa na zaidi ya wahudhuriaji 8,700.

Ingawa kuna tafsiri kadhaa za Biblia katika lugha ya Ndebele (ya Zimbabwe), kweli za Biblia zinaeleweka wazi katika tafsiri hii. Kwa mfano, kwenye Yohana 17:3, Biblia nyingine za lugha ya Ndebele zinamwita Yesu Kristo “Mungu wa Kweli.” Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inaonyesha wazi tofauti kati ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Tafsiri hii inatumia lugha ya kisasa ambayo wasomaji wataelewa kwa urahisi.”

Tunashangilia kuona watu wanaotaka kuijua kweli ulimwenguni pote, wakipata Neno la Mungu na hilo linawawezesha ‘kuchukua maji ya uzima bure’ katika lugha zao wenyewe.​—Ufunuo 22:17.