Hamia kwenye habari

Dada Mieko Yoshinari nchini Japani akiandika maelezo yake kwa herufi kubwa kwa sababu ya matatizo ya macho

APRILI 28, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Shule za Utumishi wa Painia Zafanywa Kupitia Mtandao kwa Mara ya Kwanza

Shule za Utumishi wa Painia Zafanywa Kupitia Mtandao kwa Mara ya Kwanza

Kutokana na janga la corona, Shule za Utumishi wa Painia duniani pote zilifanywa kwa mara ya kwanza kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao wakati wa mwaka wa utumishi wa 2021. Kwa sababu ya uthamini wao kwa uandalizi huo wa kiroho, wanafunzi walifanya yote waliyoweza ili kuhudhuria. Yafuatayo ni masimulizi yanayoonyesha jinsi Yehova alivyowasaidia baadhi ya mapainia kukabiliana na changamoto za pekee ili wafaulu kuhudhuria shule hiyo.

Dada Mieko Yoshinari nchini Japani ametumikia akiwa painia wa kawaida kwa miaka 30. (Ona picha ya kwanza.) Ingawa ni changamoto kwake kutumia vifaa vya kielektroni na pia ana matatizo ya kuona, aliazimia kuhudhuria shule ya upainia kupitia mtandao. Anasema hivi: “Nilitayarisha maelezo yangu kwa kuandika utafiti niliofanya kwa kutumia herufi kubwa ili iwe rahisi kwangu kusoma. Yehova alinitia moyo sana na kuniimarisha kupitia shule hiyo ya mapainia.”

Dada Anita Kariuki, anayeishi Thika, mji ulio karibu na Nairobi, Kenya, amejiajiri ili kujitegemeza anapoendelea na upainia. Ili aweze kuhudhuria shule hiyo, alihitaji kufunga biashara yake kwa juma zima. Mwanzoni Anita alikuwa na wasiwasi kuhusu hilo, lakini akamtegemea Yehova kikamili kwamba atamsaidia. Anaeleza hivi: “Nilitoa dua kwa Yehova, kisha nikaacha jambo hilo mikononi mwake na kuendelea na huduma yangu.” Mwisho-juma kabla ya shule hiyo kuanza, alifanya kazi na kupata pesa za kutosha kushughulikia nyingi kati ya gharama zake. Licha ya kupungukiwa dola 30 hivi (za Marekani), bado alihudhuria shule hiyo. Baada ya kipindi cha Jumatano, mteja mmoja alimpigia Anita simu na kumlipa deni la pesa ambazo hakuwa amelipa baada ya kuhudumiwa. Kiasi hicho kilikuwa kilekile ambacho Anita alihitaji ili kushughulikia gharama zake zote!

Nyumba ya Dada Laurenth Madrigales huko Yoro, Honduras, ilifurika na kujaa matope kufikia futi tatu baada ya Kimbunga Eta na Iota. Familia yake ilipoteza karibu mali zao zote na kwa muda hawakuwa na makao. Wakati huo Dada Laurenth alipokea mwaliko wake wa kuhudhuria shule ya mapainia. Alifurahi sana kualikwa, lakini alikuwa na wasiwasi kwamba familia yake haingeweza kusafisha nyumba yao kwa wakati kabla ya shule kuanza. Laurenth anasema: “Tulihitaji kuanza usafi mapema asubuhi na tulimaliza usiku sana kila siku. Tuliendelea kufanya hivyo kwa siku nyingi. Nilichoka sana. Nilihisi kwamba sikuwa na nguvu za kutosha kujifunza ili kutajitayarisha kwa ajili ya shule na hivyo nikakataa mwaliko.” Alisali na kumweleza Yehova jinsi hilo lilivyomhuzunisha sana. Siku kadhaa kabla ya shule kuanza, alishangaa sana Halmashauri ya Kutoa Msaada ilipoomba kusaidia kusafisha nyumba yao. Hilo lilimpa nafasi ya kutosha kutayarisha naye akafaulu kuhudhuria shule hiyo akiwa nyumbani kwake.

Dada Laurenth Madrigales nchini Honduras akiwa nje ya nyumba yao iliyoharibiwa na kimbunga kabla ya kusafishwa

Ndugu Spencer Stash na mke wake, Alexandra, ni mapainia wa kawaida wanaotumikia huko Cleveland, Ohio, Marekani. Kabla ya shule kuanza, baba ya Spencer, Robert, ambaye ni mjane, alilazwa hospitalini. Wenzi hao wa ndoa hawakuwa na uhakika ikiwa wanapaswa kuhudhuria shule hiyo. Lakini Robert aliwatia moyo wasikose kuhudhuria. Kwa kusikitisha, siku mbili kabla ya shule kuanza, Robert alikufa. Ingawa walikuwa na huzuni nyingi, Spencer na Alexandra walikosa siku ya kwanza tu ya shule. Kusali kwa bidii kuliwapa nguvu za kuendelea. Spencer anasema kwamba walijihisi wakiwa na amani kwa sababu walifanya kama baba yake alivyowaomba wafanye. Spencer anaongezea hivi: “Tunatazamia wakati ambapo tutamweleza kwamba tulifaulu kuhudhuria shule hiyo na tumweleze baadhi ya mambo tuliyojifunza. Utegemezo wa wanafunzi wenzetu na walimu ulitusaidia sana.”

Ndugu Jung Dae-sik nchini Korea Kusini amekuwa akiishi katika makao ya kuwatunzia wazee kwa miaka kumi iliyopita. Anatumia gari lililo na magurudumu kwa sababu alipatwa na kiharusi kilichomfanya apooze upande mmoja. Alijaribu kuhudhuria shule za mapainia zilizopita, lakini kwa sababu ya hali ya afya yake, hakuweza kuhudhuria kwa zaidi ya siku moja. Alipopata mwaliko wa kuhudhuria shule hiyo kupitia mtandao, alishangilia sana. Anasema hivi: “Nilishukuru sana kwa mpango huo hivi kwamba nisingeweza kujizuia kulia. Nisingeweza kuhudhuria shule hiyo isipokuwa kwa njia hiyo tu. Nilikuwa na shangwe nyingi sana kushiriki katika mtaala huo.”

 

Ndugu Jung Dae-sik nchini Korea akihudhuria shule ya mapainia akiwa kwenye makao ya kuwatunzia wazee

Ndugu Eddy El Bayeh na mke wake, Cherise, mapainia wa kawaida nchini Australia

Ndugu Eddy El Bayeh na mke wake, Cherise, wanaishi New South Wales, Australia. Cherise anasema hivi: “Nilihisi kwamba sikuwa nikifanya maendeleo katika huduma yangu, kwamba sasa ilikuwa imeanza kuwa ya kidesturi tu na sikujua jinsi ya kubadili mambo.” Lakini shule ya mapainia ilikuja kwa wakati unaofaa kabisa. “Niliona njia nyingi ambazo ningeweza kupanua huduma yangu hata chini ya hali ngumu za sasa.”

Eddy anaeleza jinsi shule hiyo ilivyomtia moyo: “Ilikuwa ni kama Mwenye Enzi Kuu mwenyewe ananikumbatia, kana kwamba ananigusa kwa wororo begani na kuniambia: ‘Usiache! Niko pamoja nawe, ninakupenda, na ninakujali!’”

Shule nyingine kupitia mtandao zimepangwa kufanywa baadaye katika mwaka huu. Tunatiwa moyo sana kwamba watu wa Yehova wataendelea kuelimishwa licha ya changamoto zilizopo. Tunakumbushwa maneno haya ya Ayubu: “Tazama! Mungu amekwezwa katika nguvu zake; ni nani aliye mfundishaji kama yeye?”—Ayubu 36:22.

Picha zilizo hapo chini ni za walimu na wanafunzi katika nchi nyingine, ambao pia walinufaika na shule ya mapainia iliyofanywa kupitia mtandao.

 

ARGENTINA: Wanafunzi wakitumia picha ya nyuma kwenye mtandao ili kuonyesha mahubiri yasiyo rasmi kwenye usafiri wa umma

KAMERUN: Ndugu Guy Leighton, mwalimu wa shule ya mapainia na mmishonari ambaye ametumikia nchini Kamerun kwa miaka 12, akilionyesha darasa muundo wa Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi wakati wa somo kuhusu kutafsiriwa kwa Biblia

UGIRIKI: Ndugu Takis Pantoulas, mwangalizi wa mzunguko anayezungukia makutaniko ya katikati mwa Ugiriki, akifundisha shule ya mapainia

ITALIA: Mojawapo ya madarasa matano ya Kiingereza ya shule ya mapainia nchini Italia

MEXICO: Baadhi ya wanafunzi walihudhuria shule ya mapainia kwa kutumia kitabu kipya cha lugha ya Tzotzil, inayozungumzwa hasa katika jimbo la Chiapas. Pia, hilo ndilo darasa la kwanza kabisa kuongozwa kikamili katika lugha ya kienyeji ya Tzotzil

SRI LANKA: Ndugu Nishantha Gunawardana na mke wake, Shiromala, ambao wanatumikia wakiwa mapainia wa pekee, wakihudhuria shule hiyo

TANZANIA: Ndugu William Bundala, mzee katika eneo la Zanzibar, akiwa ameketi nje ya nyumba yake ambapo mawimbi ya Wi-Fi yanashika vizuri zaidi