Hamia kwenye habari

Mnara wa Mlinzi Na. 2 2020, lenye kichwa “Ufalme wa Mungu Ni Nini?,” likitolewa ulimwenguni pote wakati wa kampeni ya mwaka wa 2023

NOVEMBA 29, 2023
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Ujumbe wa Ufalme Wawafikia Watu Ulimwenguni Pote Wakati wa Kampeni ya Septemba 2023

Ujumbe wa Ufalme Wawafikia Watu Ulimwenguni Pote Wakati wa Kampeni ya Septemba 2023

Septemba 2023, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walishiriki katika kampeni ya pekee ya kutangaza kuhusu Ufalme wa Mungu. Gazeti Mnara wa Mlinzi Na. 2 2020, lenye kichwa “Ufalme wa Mungu Ni Nini?,” lilitolewa. a Mambo yafuatayo yaliyoonwa yanaonyesha jinsi kampeni hiyo ilivyowanufaisha watu ulimwenguni pote.

Uingereza

Wakati wa kampeni hiyo, Mark na mwana wake mwenye umri wa miaka kumi, Flynn, wanaoishi Southport, Uingereza, walikutana na mwanamke fulani kwenye mlango wa kwanza waliobisha. Kwa msisimuko mwanamke huyo alichukua gazeti hilo la Mnara wa Mlinzi kutoka kwenye mkono wa Mark, na akasema hivi kwa mshangao akirejelea swali lililokuwa kwenye jalada: “Siwezi kuamini kwamba mmekuja leo! Ninahitaji jibu la swali hilo sasa kuliko wakati mwingine wowote.” Huku akitokwa na machozi, alieleza kwamba mwana wake alikuwa amekufa hivi karibuni, na kwa sababu hiyo alikuwa akitafuta faraja. Mara moja, Mark alimweleza kuhusu ahadi ya ufufuo. Aliguswa moyo sana na akaomba habari zaidi. Mark na Flynn waliporudi tena, mwanamke huyo pamoja na mume wake walikubali mara moja broshua Furahia Maisha Milele! na funzo la Biblia likaanzishwa.

Indonesia

Ndugu anayeitwa Frederick nchini Indonesia alikuwa akingoja kwenye mstari katika kituo cha afya alipoanzisha mazungumzo na mwanamume mmoja aliyekuwa na mwana wake. Hatimaye, Frederick alimweleza ahadi ya Biblia kwamba hivi karibuni magonjwa na kuteseka hakutakuwepo tena. Baada ya kumwomba baba huyo asome maneno ya Yesu kuhusu Ufalme wa Mungu kwenye Mathayo 6:9, 10, Frederick alimuuliza hivi: “Umeona kuteseka kutaondolewa jinsi gani?” Mwanamume huyo alijibu hivi kwa usahihi: “Ni Mungu atakayeondoa kuteseka kupitia kwa Ufalme wake.” Kisha mwanamume huyo akauliza Ufalme wa Mungu ni nini, lakini wakati huohuo jina la mwana wake likaitwa ili kumwona daktari kwa hiyo wakaanza kuondoka. Upesi Frederick akampa mwanamume huyo anwani yake na nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi. Frederick alishangaa sana asubuhi iliyofuata, mwanamume huyo na mke wake walipofika mlangoni kwake wakiomba kujua mengi zaidi kuhusu manufaa yatakayoletwa na Ufalme wa Mungu. Akiwa na furaha, Frederick alifanya mipango ya kuendeleza mazungumzo.

Malawi

Nchini Malawi, dada wawili walimtolea chifu wa kijiji kimoja nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi na kumweleza jinsi Ufalme wa Mungu utakavyoitawala dunia nzima. Chifu huyo akauliza: “Je, hilo linamaanisha kwamba kuna wakati nitapoteza ufalme wangu?” Baada ya kuonyeshwa kwa nini Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee la matatizo ya wanadamu, chifu huyo alisema: “Hizi ni habari njema. Mimi ni chifu, lakini mimi pia ninatambua kwamba machifu hawataweza kamwe kufanya mambo ambayo Ufalme wa Mungu utawafanyia watu kila mahali.” Chifu huyo aliomba nakala nyingine tano za Mnara wa Mlinzi ili awape machifu wa vijiji vingine. Pia alisema kwamba alitazamia kwa hamu kuwa na mazungumzo ya Biblia wakati ujao.

Mexico

Dada mmoja huko Puebla, Mexico, alimuuliza mwanamume fulani mwenye umri mkubwa ikiwa anaweza kushiriki ujumbe wa tumaini pamoja naye alipokuwa akisafiri ndani ya basi. Mwanamume huyo alikubali, kwa hiyo alimsomea maneno ya Yesu kuhusu Ufalme wa Mungu yaliyo kwenye Mathayo 6:9, 10. Mwanamume huyo akauliza hivi: “Ufalme wa Mungu ni nini? Mimi sijawahi kuisoma Biblia au kuzungumza na Mashahidi wa Yehova.” Dada yetu alijibu swali hilo kwa kumwonyesha nakala ya Mnara wa Mlinzi kwenye kifaa chake cha kielektroni. Mwanamume huyo akaanza kuuliza maswali zaidi, kwa hiyo dada yetu akamweleza jinsi anavyoweza kutumia JW Library kupata majibu. Mwanamume huyo alipogundua kifaa chake hakikuwa na nafasi ya kutosha, alianza kufuta vitu vingine akisema hivi: “Kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu ni muhimu zaidi.” Kufikia wakati walipofika mwisho wa safari, alikuwa amemaliza kusoma gazeti lote la Mnara wa Mlinzi, kuzungumzia somo la kwanza la broshua Furahia Maisha Milele!, na akakubali kujifunza Biblia. Alimshukuru tena na tena dada yetu na akasema angependa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme.

New Zealand

Ndugu anayeitwa Ben nchini New Zealand alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, alimweleza mama mmoja kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utawaletea kitulizo watu wote wanaoteseka. Mwanamke huyo akasema hivi kwa msisimuko: “Inastaajabisha kwamba umekuja hapa! Jana usiku nimeshindwa kulala kwa sababu nilikuwa na wasiwasi mwingi kuhusu wakati ujao.” Ben aliposoma Ufunuo 21:4 na kueleza jinsi Ufalme utakavyokomesha magonjwa na kifo, mwanamke huyo alianza kutokwa na machozi. Kwa furaha, alikubali nakala ya Mnara wa Mlinzi na akasema alikuwa na hamu ya kusoma na kujifunza mengi zaidi.

Sudan Kusini

Katika kambi ya wakimbizi nchini Sudan Kusini, watu wengi walikuwa na hamu ya kujifunza mengi kuhusu Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, ndani ya saa mbili tu, karibu machapisho 1,000 kutia ndani Mnara wa Mlinzi, yalisambazwa. Mkimbizi mmoja alisema hivi: “Mmekuja kwa wakati unaofaa kabisa. Hili hasa ndilo tulilohitaji!” Mkimbizi mwingine aliwaambia ndugu zetu: “Asanteni sana kwa kutufikiria. Tunajua kwamba mnatoka mbali sana, lakini tafadhali msikose kuja tena.”

Taiwan

Dada wawili nchini Taiwan walikutana na mwanamume ambaye alikuwa amehuzunishwa sana na moto uliokuwa umetokea karibuni huko Hawaii. Dada mmoja alimwonyesha picha katika Mnara wa Mlinzi iliyoonyesha paradiso ya wakati ujao duniani. Mwanamume huyo akasema: “Itapendeza sana ikiwa dunia itafanana na picha hii. Katika ulimwengu uliojaa habari mbaya, inapendeza kusikia ujumbe huu wenye kufariji wa tumaini.”

Lilikuwa pendeleo kubwa kwetu sote kushiriki katika kampeni hiyo ya ulimwenguni pote na kuwaeleza watu kila mahali kwamba chanzo cha faraja na tumaini la kweli, ni Ufalme wa Mungu.​—Waroma 15:4.

Hapa chini kuna mkusanyo wa picha za ndugu na dada katika nchi mbalimbali wakishiriki kwa shangwe katika kampeni hiyo ya kuhubiri ulimwenguni pote

a Katika makala hii, kila mara Mnara wa Mlinzi linapotajwa linarejelea toleo la Mnara wa Mlinzi Na. 2 2020.

 

Burkina Faso

Kosta Rika

Ethiopia

Georgia

Indonesia

Italia

Kenya

Mexico

New Zealand

Panama

Poland

Scotland

Korea Kusini

Taiwan

Togo

Wales