Hamia kwenye habari

Akina ndugu na dada kutoka nchini Ukrainia wakiwa katika nchi nyingine

JUNI 9, 2022
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Wakimbizi Kutoka Nchini Ukrainia Waanza Maisha Mapya Kwenye Mataifa Mengine

Wakimbizi Kutoka Nchini Ukrainia Waanza Maisha Mapya Kwenye Mataifa Mengine

Iryna Makukha sasa anaishi katika Jamhuri ya Cheki

Vita vilipoanza nchini Ukrainia, Iryna Makukha, dada mseja mwenye umri wa miaka 46, alielekea kwenye kituo cha treni huko Kharkiv. Aliamua kwamba ingekuwa salama zaidi kwake ikiwa angehama nchini humo. Kwa sababu ya vurugu watu walipanda treni bila kujua zilikuwa zikielekea wapi. Treni ambayo Iryna alipanda iliondoka kituoni madirisha yakiwa yamefunikwa ili kupunguza uwezekano wa kushambuliwa. Baada tu ya kuondoka ndipo alipogundua kwamba treni hiyo ilikuwa ikielekea Slovakia.

Sasa dada Iryna anaishi katika Jamhuri ya Cheki, na alifika kwenye mji wake mkuu unaoitwa Prague, Machi 3, 2022. Anafanya kazi mbalimbali za usafi na anaishi kwenye nyumba moja na akina dada wengine wawili ambao pia ni wakimbizi kutoka Ukrainia. Dada Iryna anajifunza lugha ya Cheki na amerudia utumishi wa wakati wote, ambao ameufanya kwa miaka 20.

Iryna anasema: “Nimejionea kwa macho yangu jinsi Yehova anavyotutunza kupitia watu wake. Hilo limeimarisha sana imani yangu.”

Karibu ndugu na dada 23,000 wamefanya uamuzi wa kuhamia nchi nyingine. Wale ambao wameamua kuhamia nchi nyingine wameepuka madhara ya vita, lakini bado wanahitaji kutafuta kazi, mahali pa kuishi, kupata vibali vya uhamiaji, kuwahamishia watoto wao kwenye shule mpya na wakati huohuo kujifunza lugha mpya. Wametambua kwamba ratiba yao ya kumtumikia Yehova na upendo wa undugu wa ulimwenguni pote umewasaidia sana katika wakati huu mgumu.

Anatoli, Olena na Alina Perceac sasa wanaishi nchini Romania

Washiriki watatu wa familia ya Perceac, Anatoli, Olena, na mtoto wao, Alina mwenye umri wa miaka 17, wameanza maisha mapya nchini Romania baada ya milipuko iliyoharibu sehemu mbalimbali za jiji la Mykolaiv Oblast, nchini Ukrainia walimokuwa wanaishi. Familia hiyo ilihama Machi 6, 2022. Kwa kuwa alikuwa raia wa Moldova, Anatoli aliruhusiwa kuhamia Romania pamoja na familia yake. Olena anasema kwamba kuhamia nchi nyingine ni kama “kuung’oa mti na mizizi yake kutoka ardhini na kuuhamishia mahali pengine.”

Kwa msaada wa akina ndugu nchini Romania, familia ya Perceac sasa imepata mahali pa kuishi. Kwa kuongezea, Anatoli na Olena wamepata kazi, na Alina anasoma katika shule iliyo Ukrainia kupitia mtandao.

Akina ndugu na dada wa Romania wanawasaidia ndugu na dada zao si kimwili tu, bali pia kiroho na kihisia. Akina ndugu na dada wanatumia wakati na familia hizo hivi kwamba hawahisi wakiwa peke yao kwenye nchi ya kigeni. Olena na Alina wanajifunza Kiromania kwa kutumia programu ya JW Language na pia kupitia kushiriki utumishi pamoja na ndugu na dada katika kutaniko lao jipya. Anatoli alijua Kiromania tangu utotoni.

Anatoli anasema kwamba “Tumejionea mkono wa Yehova tangu mwanzo. Kupitia tengenezo na upendo kutoka kwa ndugu na dada, tunahisi Yehova anatupenda sana.”

Vladyslav na mama yake, Alina, sasa wanajitahidi kuzoea maisha mapya nchini Poland

Alina Havryliuk dada aliyekuwa mjane hata kabla ya vita, pamoja na mwana wake mwenye umri wa miaka 16 anayeitwa Vladyslav, walifika Suwalki nchini Poland, kutoka Vinnystia, nchini Ukrainia, Februari 27. Alina anasema: “Mwanzoni nilijiuliza nitaishi wapi na mwanangu na tutajitegemeza jinsi gani, lakini nilikuwa na uhakika kwamba Yehova atatutunza.”

Alina mwenye umri wa miaka 37, alianza kutafuta haraka kazi ambayo haitaingilia ratiba yake ya mikutano. Alipata kazi ya kufanya usafi shuleni. Alina anasema: “Jambo muhimu zaidi ni kwamba kazi hii inanipa fursa ya kushiriki utumishi hata zaidi na kuitegemeza familia yangu.”

Alina na Vladyslav wanajifunza lugha ya Kipolandi na wanaendelea kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida katika kutaniko la lugha ya Kipolandi. Vladyslav pia amejiunga na shule ya sekondari.

Ndugu na dada zetu nchini Ukrainia wanapitia changamoto na mabadiliko mengi sana, ingawa hivyo Yehova anaendelea kuwapa nguvu zinazopita zile za kawaida. Wamejionea ukweli wa maneno ya andiko la 2 Wakorintho 4:8 linalosema: “Tunakandamizwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kushindwa kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa.”