Hamia kwenye habari

Dada Fumiko Takehara pamoja na mwana wake, Naoki, wakichunguza makala za Habari za JW kama sehemu ya mradi wa Ibada ya Familia

MACHI 8, 2021
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Wazazi Wanatumia Makala za Habari za JW Kuwasaidia Watoto Wao Kukabiliana na Majaribu kwa Ujasiri

Wazazi Wanatumia Makala za Habari za JW Kuwasaidia Watoto Wao Kukabiliana na Majaribu kwa Ujasiri

Wazazi wengi Mashahidi wamekuwa wakitumia makala za Habari za JW kuimarisha imani za watoto wao.

Dada Fumiko Takehara, mama nchini Japani, husoma na kujadili pamoja na mwana wake Naoki, mwenye umri wa miaka 12, ripoti zilizo katika sehemu ya Habari za JW. Wao huchapisha picha za ndugu na dada wanaotajwa katika makala hizo na kuzibandika ukutani. Fumiko anasema: “Sisi huwataja kila mmoja wao katika sala zetu. Tunafarijika kujua kwamba Yehova huwapa shangwe watu wake licha ya kwamba wamefungwa gerezani. Tunaona shangwe katika nyuso za ndugu zetu. Mifano yao mizuri humsaidia mwana wangu kuwa mshikamanifu kwa Yehova anapokuwa shuleni.”

Familia ya Zannou hutumia makala za Habari za JW kujenga ujasiri wao katika kuhubiri

Ndugu Kilanko Zannou, baba wa watoto wawili nchini Côte d’Ivoire anasema hivi: “Mimi huchunguza kila siku jw.org ikiwa makala za Habari za JW zimetoka. Mara nyingi Kilanko hutia ndani ripoti hizo katika ibada yao ya familia. Amegundua kwamba familia yake, kutia ndani mwana wake mwenye umri wa miaka saba, Matthias, amejifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu zetu wanaovumilia mateso kwa ujasiri.

Matthias alikuwa anaogopa kuwahubiria wanafunzi wenzake. Kilanko anasema hivi: “Baada ya ibada ya familia, Matthias alisema hivi kwa shauku: ‘Siogopi tena kuhubiri!’”

Ndugu Holmes Simatupang, baba nchini Indonesia, alisoma pamoja na watoto wake wawili makala mbili kuhusu vijana Mashahidi wa Indonesia waliofukuzwa shule kwa sababu ya kukataa kusalimu bendera.

Familia ya Simatupang ikizungumzia makala za Habari za JW kuhusu vijana waliodumisha utimilifu wao shuleni

Ndugu Simatupang anasema: “Watoto wetu hupitia changamoto hiyo shuleni kwao. Wao hushinikizwa na walimu na wanafunzi wenzao kusalimu bendera, kuimba wimbo wa taifa, na kushiriki utendaji wa kidini. Kwa sababu hizo, kwa muda fulani, watoto wetu waliogopa kwenda shule.

“Baada ya kuzungumzia makala hizo mbili wakati wa ibada ya familia, sasa wanaweza kufafanua kwa ujasiri msimamo wao wa kutosalimu bendera. Hawaogopi tena kupita kiasi kwamba watafukuzwa shule.”

Dada Lady Nery Passos nchini Brazili anasema hivi: “Mwana wetu Pedro alipokuwa na umri wa miaka mitano au sita tu, alihitaji kueleza kwa nini hasherehekei sikukuu za kuzaliwa.” Alipokuwa akifikiria njia bora ya kumsaidia mwana wake, alikumbuka makala za Habari za JW zinazotaja ndugu na dada wengi waliojitayarisha mapema kwa ajili ya majaribu. Anasema hivi: “Tulitumia ibada ya familia ili kufanya mazoezi ya hali halisi, jambo lililomsaidia kujua mambo ya kufanya kunapokuwa na sherehe za kuzaliwa shuleni.” Mazoezi hayo yalimtayarisha vizuri Pedro kutetea imani yake.

Ndugu na Dada Passos hutumia Habari za JW kumfundisha mwana wao jinsi ya kutetea imani yake

Makala za Habari za JW zinatukumbusha jinsi ambavyo Yehova huwaimarisha na kuwatunza waaminifu wake. Tuna ushahidi mwingi wa kwamba tunapokabili majaribu tutaendelea “kujawa na shangwe na roho takatifu” ili tuweze kuvumilia.—Matendo 13:50-52.