Hamia kwenye habari

DESEMBA 3, 2020
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Wenye Mamlaka Watoa Shukrani kwa Kampeni ya Kutangaza Ufalme ya 2020

Wenye Mamlaka Watoa Shukrani kwa Kampeni ya Kutangaza Ufalme ya 2020

Katika mwezi wa Novemba, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote waligawanya gazeti la Mnara wa Mlinzi Na. 2 2020 toleo la watu wote, katika maeneo ya biashara, washiriki wa familia na watu wanaopendezwa na ujumbe wao. Jambo la pekee katika kampeni hiyo lilikuwa kwamba maofisa wengi wa serikali walipewa gazeti hilo. Kufikia sasa, ofisi za tawi zimepokea majibu mengi yenye kutia moyo.

Nchini Sierra Leone, Rex Bhonapha, Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, na Mipango, aliandika barua akiwashukuru akina ndugu kwa kumtumia gazeti hilo. Aliongezea hivi: “Ningependa kukiri kuwa gazeti letu limegusa moyo wangu na kunielimisha sana; sasa nina kawaida ya kulisoma kila siku.”

Nchini Samoa, Waziri Mkuu alituma barua ya shukrani inayotaja pia jinsi anavyothamini Sala ya Bwana. Kwa kuongozea, Rais wa Nchi hiyo, Tuimalealiifano Vaaletoa Sualauvi II, alisema kwamba anathamini sana kazi ya kutoa elimu ya Biblia. Alisema kazi hiyo “inawasaidia watu, inawafundisha kuhusu Biblia ili waweze kubadili maisha yao.” Aliwapongeza akina ndugu kwa kusitisha kukutana na watu na kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa sababu ya ugonjwa wa COVID-19.

Osvaldo Cartagena García, Katibu Mkuu wa Manispaa nchini Chile, alisema hivi: “Ni matumaini yangu kwamba kampeni yenu njema itawasaidia watu wote walio na mamlaka nchini na kuwachochea kufanya mambo mema kwa ajili ya jamii nzima, hasa ikizingatiwa hali tunazokabili nchini na dunia nzima.”

Mbunge mmoja wa bunge la Ujerumani (Deutscher Bundestag) aliandikia ofisi ya tawi ya Ulaya ya Kati iliyopo Ujerumani na kusema hivi: “Ninaijua vizuri sana dini yenu. Kwa heshima kubwa, ninatambua kwamba washiriki wa dini yenu hutangaza kwa ujasiri kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova. . .  Ninajua pia kwamba washiriki wa dini yenu waliteswa kikatili wakati wa utawala wa Wanazi.”

Pia, Wizara moja nchini Ujerumani iliwashukuru Mashahidi kwa kuwafariji watu wakati wa ugonjwa wa virusi vya corona. Ilisema hivi: “Mmetoa mchango wenye thamani sana kwa kuwasaidia wananchi kudumisha umoja.”

Nchini Kolombia, mshiriki mmoja wa Bunge na mwingine wa Baraza la Wawakilishi, waliandikia ofisi ya tawi barua ya shukrani baada ya kupokea gazeti, wakisema kwamba watawapa watu wengine pia magazeti hayo. Ofisa mmoja wa Wizara ya Mazingira aliandika hivi pia: “Asanteni sana kwa kunitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi, lina ujumbe unaookoa uhai!”

Balozi wa Ghana nchini Japani, Frank Okyere, alisema hivi: “Gazeti hili lina habari nzuri kwa kuwa linataja suluhisho la changamoto nyingi wanazokabili wanadamu.”

Pia, balozi kutoka Azerbaijan alisema hivi: “Asanteni sana kwa kutuma gazeti hili la pekee la Mnara wa Mlinzi katika ofisi za ubalozi. Nimefurahia sana kulisoma gazeti hilo.”

Tunakubaliana na maneno haya ya Ndugu Amaro Teixeira, anayesimamia Dawati la Habari za Umma katika ofisi ya tawi ya Msumbiji: “Kampeni hii imefanikiwa kwa kiwango kikubwa ambacho hatukuwazia. Ujumbe wa Ufalme umewafikia hata wale ambao kwa kawaida ni vigumu kuwafikia.”

Bila shaka tutapokea shukrani nyingi kutoka kwa wenye mamlaka na watu wengine kadiri ujumbe wa Biblia unavyozidi kuwafikia “wote wenye vyeo vya juu.”—1 Timotheo 2:2.